Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ishi Maisha Rahisi, Yenye Usawaziko

Ishi Maisha Rahisi, Yenye Usawaziko

Ishi Maisha Rahisi, Yenye Usawaziko

KUISHI maisha rahisi, yenye usawaziko kunathawabisha kwelikweli. Lakini hilo linahusisha nini? Kwanza, huenda ukahitaji kufikiria mambo unayotanguliza. Unaweza kufanyaje hivyo?

Jiulize: ‘Nimetimiza nini kufikia sasa? Ni mambo gani yanahitaji kufanywa?’ Andika miradi yako muhimu hapa chini:

1. ․․․․․

2. ․․․․․

3. ․․․․․

Leo watu wengi wana mtazamo wa kufuatilia vitu vya kimwili kwa kuwa hawafikirii wakati ujao. Ni kana kwamba wanasema: “Na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.” (1 Wakorintho 15:32) Wanaamini kwamba maisha bora zaidi ni kufanya kazi na kununua vitu. Hata hivyo, Biblia inapinga maoni hayo.

Katika moja ya mifano yake, Yesu alizungumza kuhusu mtu ambaye alijikusanyia vitu lakini akafa kabla ya kuvifurahia. “Hivyo ndivyo huwa kwa mtu anayejikusanyia mwenyewe hazina lakini si tajiri kwa Mungu.” (Luka 12:16-21) Je, mtu huyo alifanya makosa kwa kufanya kazi kwa bidii ili kujiruzuku? Hapana. Tatizo lake lilikuwa kukazia fikira sana vitu vya kimwili. Hakufikiria maoni ya Mungu alipofanya mipango yake. Kwa sababu hiyo, mali yake yote—kila kitu alichokuwa amefanyia kazi—haingemfaidi mwishowe. Inasikitisha kama nini!—Mhubiri 2:17-21; Mathayo 16:26.

Tofauti na hilo, Yesu anatuambia tufanye kazi ili tupate zawadi ya milele. “Fanyeni kazi, si kwa ajili ya chakula ambacho huharibika,” akahimiza, “bali kwa ajili ya chakula ambacho hudumu kufikia uzima wa milele.” (Yohana 6:27) Mapema Yesu alikuwa amesema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Hiyo ni zawadi nzuri kama nini!

Unaweza Kukabilianaje na Mahangaiko?

Yesu alitambua kwamba wanadamu wana mwelekeo wa kuhangaikia vitu vya kimwili. Kwa hiyo, aliwahimiza wanafunzi wake hivi: “Acheni kutafuta mnachoweza kula na mnachoweza kunywa, na acheni kuhangaika kwa wasiwasi; kwa maana mataifa ya ulimwengu yanafuatilia kwa bidii mambo yote hayo, lakini Baba yenu anajua mnahitaji mambo hayo. Hata hivyo, utafuteni ufalme wake sikuzote, na mambo hayo mtaongezewa.”—Luka 12:29-31.

Maneno hayo yenye kutia moyo yamewachochea Wakristo wengi kurahisisha maisha yao. Juliet, anayeishi nchini Malasia anasema hivi: “Kazi yangu ilinifanya nijihisi mchovu na nikate tamaa. Kwa hiyo mimi na mume wangu tulisali Yehova atusaidie kurahisisha maisha yetu. Alijibu haraka. Kabla ya mwezi mmoja kwisha, nilipata kazi ambayo haikuwa ya wakati wote ya kuwafundisha watoto walemavu.” Steve, ambaye hufanya kazi ya kuezeka paa huko Australia, alirekebisha ratiba yake ya kazi ili aweze kutumia wakati mwingi zaidi pamoja na familia yake katika utendaji wa kiroho. Mke wake, Maureen, anaeleza hivi: “Sasa sisi sote tuna furaha zaidi. Watoto wanafurahia sana mpango huo! Mimi pia ninaufurahia! Ukifanya maisha yako yawe rahisi, familia yote itasitawi.”

Hata hivyo, ikiwa umepoteza kazi na unakaribia kupoteza nyumba yako, unahitaji imani yenye nguvu kufuata himizo hilo la Yesu. Lakini, ukitanguliza mambo ya kiroho na kumtegemea Mungu, wewe pia unaweza kuishi maisha rahisi, yenye usawaziko. Kufanya hivyo kutakusaidia kufikia “uzima ulio wa kweli,” yaani, uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu, ambamo kazi yote itafurahisha na haitakuwa ya bure.—1 Timotheo 6:17-19; Isaya 65:21-23.

Je, ungependa kujifunza mengi kuhusu “uzima ulio wa kweli” ambao Biblia inaahidi? Ikiwa ndivyo, wasiliana na Mashahidi wa Yehova wa eneo lenu, au waandikie barua ukitumia anwani inayofaa kati ya zile zilizoorodheshwa kwenye ukurasa wa 5 wa gazeti hili.

[Blabu katika ukurasa wa 9]

Katika ulimwengu mpya wa Mungu, kazi zote zitakuwa zenye kufurahisha na kuridhisha

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

KAZI UNAZOWEZA KUJIBUNIA

Madokezo yafuatayo yanaweza kusaidia katika sehemu za ulimwengu ambapo kuna ukosefu wa kazi:

● Kutunza nyumba za watu (wakati watu wameenda likizo na wanataka nyumba yao itunzwe)

● Kusafisha: maduka; ofisi; nyumba baada ya ujenzi, baada ya msiba wa moto, baada ya watu kuhama; kufanya kazi za nyumbani; kusafisha madirisha (katika maofisi na nyumba)

● Urekebishaji: baiskeli; vifaa vya kila aina.

● Kazi ndogo-ndogo: kutengeneza kabati, milango, varanda; kupaka rangi; kutengeneza ua; kuweka paa

● Kazi za shambani: kupanda na kuvuna, kuchuma matunda

● Kupanda na kutunza mimea ndani ya: ofisi, benki, maduka makubwa, kumbi, na sebule

● Kusimamia majengo: Kutunza na kusafisha majengo (nyakati nyingine utapewa nyumba ya kuishi bila malipo)

● Kuweka na kuosha zulia na sakafu ya mbao iliyopakwa rangi

● Kupeleka magazeti kwa ukawaida na huduma nyingine za kupeleka vitu kama vile matangazo, bili za manispaa

● Kuhamisha watu, kuwahifadhia watu wanaohama vitu vyao

● Kutengeneza mandhari, kupogoa miti, kutunza bustani, kukata mbao

● Dereva wa basi la shule

● Upigaji picha (watu mmojammoja na sherehe za umma)

● Kuwauzia wavuvi chambo

● Kubadilishana huduma: lipia huduma za kurekebisha gari kwa kurekebisha vifaa vya umeme, kushona nguo ili urekebishiwe mabomba ya maji

Kwa habari zaidi ona gazeti Amkeni! la Machi 8, 1996 (8/3/1996), ukurasa wa 3-11.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

KAZI UNAZOWEZA KUFANYIA NYUMBANI

Chunguza mahitaji ya eneo unamoishi. Uliza majirani. Chukua hatua ya kwanza.

● Kuwatunza watoto

● Kuuza mboga au maua yaliyokuzwa nyumbani; maji ya matunda

● Kushona na kurekebisha nguo

● Kuoka na kupika chakula

● Kushona mfarishi, kufuma kroshia, ufumaji; ufinyanzi; na ufundi mwingine

● Kushona vitambaa kwenye viti na sofa

● Uhasibu, kupiga chapa, huduma za kompyuta za nyumbani

● Huduma za kujibu simu

● Kutengeneza na kunyoa nywele

● Kukodisha vyumba

● Kuandika anwani na kujaza bahasha kwa ajili ya watangazaji wa bidhaa

● Kuosha magari na kung’arisha kwa kemikali (mteja analeta gari nyumbani kwako)

● Kuosha wanyama vipenzi na kuwatembeza

● Utengenezaji kufuli na funguo (karakana ikiwa nyumbani)

Taarifa: Matangazo kuhusu kazi zilizotajwa hapa juu yanaweza kuwekwa kwenye karatasi za kutangaza bidhaa au kwenye ubao wa matangazo wa maduka makubwa bila malipo au kwa bei nafuu.