Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilichagua Kazi Bora Zaidi

Nilichagua Kazi Bora Zaidi

Nilichagua Kazi Bora Zaidi

Limesimuliwa na Plamen Kostadinov

NILIAMKA karibu saa sita mchana. Chupa tupu zilikuwa zimetapakaa kila mahali sakafuni, na visahani vya kuwekea majivu ya sigara vilikuwa vimejaa na vinavunda. Msisimuko wa karamu tuliyofanya usiku uliotangulia ulikuwa umekwisha. Nilijihisi nikiwa nimekata tamaa na nikiwa mpweke sana. Kila kitu maishani kilionekana kuwa hakina maana! Acheni nieleze jinsi nilivyojipata katika hali hiyo yenye kusikitisha.

Katika mwaka wa 1980, nilipokuwa na umri wa miaka 14, nilianza kujifunza usanii. Baba yangu aliniambia kwamba nilikuwa nimepata mwaliko wa kujiunga na chuo cha usanii katika mji wa Troyan, Bulgaria. Nilifurahi sana, kwani baadaye katika mwaka huo, nilitoka katika mji wa nyumbani wa Lovech na kuhamia Troyan.

Nilifurahia kuishi mbali na wazazi wangu na kufanya chochote nilichotaka. Nilianza kuvuta sigara na mara kwa mara ningelewa pamoja na marafiki wangu wa shuleni. Hatukuruhusiwa kuvuta sigara wala kunywa pombe. Lakini kuvunja sheria kulinisisimua hata zaidi.

Nilizidi kupenda kazi ya usanii. Niliboresha sana ustadi wangu wa kuchora, na tamaa ya kuwa maarufu ilizidi kuongezeka ndani yangu. Baada ya kujifunza kwa miaka mitano katika shule ya Troyan, nilitamani sana kuendeleza masomo yangu katika Chuo cha Sanaa cha Sofia, mji mkuu wa Bulgaria. Chuo hicho ndicho kilichokuwa maarufu zaidi nchini Bulgaria. Mnamo 1988, nilialikwa kwenye chuo hicho nikiwa mmoja kati ya wanafunzi wanane tu waliochaguliwa katika nchi yote. Nilijivunia sana mafanikio yangu! Siku moja nilijitazama kwenye kioo na kujiambia hivi kwa majivuno, ‘Plamen, sasa hakuna shaka kwamba utakuwa msanii maarufu!’

Utu Wangu Kabla ya Kujifunza Kweli

Nilianza kuvalia mavazi meusi na nikaachilia nywele na ndevu zangu. Watu wengi waliona kuwa hivyo ndivyo wasanii walivyopaswa kuonekana. Nilianza kuishi kwa njia hiyo ya ajabu-ajabu niliyofikiri kuwa inawafaa wasanii. Hilo lilitia ndani kukodisha chumba katika eneo la wasanii na kuliacha likiwa shaghala-baghala. Kisha nikaanza kufuga mbwa mdogo na paka aliye na watoto watatu. Pia lilikuwa jambo la kawaida kwangu kutumia pesa ovyoovyo.

Hata hivyo, tamaa yangu ya usanii ilizidi kuongezeka. Nilikuwa nikichora wakati wote, nikiuchora ulimwengu kwa njia niliyokuwa tu nikiwazia. Hata niliuchora ukuta wa chumba changu. Nilifikiri kwamba huo ndio mwanzo wa kazi ya maisha yangu yenye mafanikio.

Ilikuwa kawaida ya maisha yangu kufanya karamu pamoja na wanafunzi wenzangu. Mara nyingi tulikusanyika katika chumba changu, tukisikiliza muziki na kunywa sana, hata tulipokuwa tukijitayarishia mtihani. Mazungumzo yetu yalihusu hasa muziki, sanaa, na kusudi la maisha. Mara nyingi, tulizungumza kuhusu nguvu zisizo za asili na viumbe kutoka sayari nyingine. Mazungumzo hayo yalichochea akili yangu na kunipa mawazo mapya ya mchoro unaofuata. Nilitaka kuendelea kuwa na hisia hizo za msisimuko, lakini zilikuwapo tu nilipokuwa nimelewa. Kwa kawaida, siku iliyofuata, hakukuwa hata na masalio ya msisimuko huo.

Baada ya kuishi maisha hayo kwa miaka kumi hivi, nilihisi kwamba maisha yangu hayakuwa yenye kuridhisha. Tofauti na rangi nyangavu nilizotumia katika michoro yangu, maisha yangu yalizidi kuwa na giza na kujaa upweke. Ndoto yangu ya kuwa msanii maarufu ilianza kudidimia. Nilikuwa nimeshuka moyo na sikujua la kufanya. Hiyo ndiyo hali niliyotaja mwanzoni mwa hadithi yangu.

Kujua Kweli Kuliniokoa

Mnamo 1990, niliamua kufanya maonyesho ya michoro yangu katika mji wa Lovech. Nilimwalika Yanita, ambaye alikuwa rafiki yangu chuoni huko Sofia, ashiriki katika maonyesho hayo, kwa kuwa yeye pia alikuwa ametoka Lovech. Maonyesho hayo yalipokwisha, mimi na Yanita tulienda kwenye mkahawa wa karibu kusherehekea. Wakati wa mazungumzo yetu, alianza kunieleza mambo aliyokuwa akijifunza katika Biblia na Mashahidi wa Yehova. Aliniambia kuhusu ulimwengu mpya uliotabiriwa katika Biblia. Hilo lilichochea upendezi wangu.

Yanita aliendelea kujifunza Biblia huko Sofia, na mara kwa mara, aliniletea vichapo vya Biblia. Sitawahi kusahau jinsi nilivyosoma upesi broshua “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya” na nikamaliza kusoma kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani baada ya siku chache. * Haikuwa vigumu kwangu kukubali kwamba Mungu yuko, na mara moja nikataka kujua jinsi ya kusali. Ninakumbuka sala yangu ya kwanza. Nikiwa nimepiga magoti, nilimmwagia Yehova mahangaiko yangu kwa unyoofu. Nilisadiki kabisa kwamba alikuwa akinisikiliza. Shangwe na amani ya ndani ilianza kuchukua mahali pa upweke wangu.

Yanita alinijulisha kwa wenzi wa ndoa ambao walikuwa Mashahidi wa Yehova katika mji wa Sofia. Waliniuliza ikiwa ningependa kujifunza Biblia pamoja nao na wakanikaribisha kwenye mikutano yao. Ninakumbuka mkutano wa kwanza niliohudhuria mnamo Juni (Mwezi wa 6) 1991. Nilifika saa mbili mapema kabla ya mkutano huo na nikasubiri katika bustani fulani ndogo. Nikiwa na wasiwasi na mashaka, nilijiuliza ikiwa ningepokewa vizuri. Nilishangaa kwamba kila mtu alinikaribisha kwa uchangamfu licha ya sura yangu ya ajabu. Tangu wakati huo, nilihudhuria mikutano kwa ukawaida na nilijifunza Biblia mara mbili kwa juma.

Nilifurahi sana nilipopokea Biblia yangu ya kwanza. Sikuwa nimewahi kusoma kitu chochote chenye kuvutia na chenye hekima kama maneno yanayopatikana katika Mahubiri ya Mlimani! Nilipoendelea kujifunza, niliona jinsi Neno la Mungu lina nguvu za kubadili maisha kama inavyoelezwa kwenye Waefeso 4:23: “Mnapaswa kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yenu.” Niliacha kuvuta sigara na nikabadili sura yangu ya ajabu-ajabu. Badiliko hilo lilikuwa kubwa sana hivi kwamba siku moja baba yangu alipokuja kunilaki kwenye kituo cha gari la moshi cha Lovech, alinipita bila kunitambua.

Nilianza kufikiria kuhusu mazingira yangu. Sikuchochewa tena na chumba changu kilichokuwa shaghala-baghala, kuta zilizokuwa na michoro, na harufu mbaya ya sigara. Nilihisi tamaa ya kusafisha kila kitu. Nilipaka rangi nyeupe kwenye kuta na kuondoa picha ya kiumbe kutoka anga za juu aliye na macho matatu niliyekuwa nimechora ukutani.

Ni wazi kwamba rafiki zangu waliniacha, lakini watu wengi niliokutana nao kwenye mikutano ya Kikristo wakawa rafiki zangu wapya hadi leo. Nilifanya maendeleo upesi kwa sababu ya ushirika huo wenye kujenga. Nilibatizwa Machi 22, 1992 (22/3/1992), kwenye kusanyiko la kwanza la Mashahidi wa Yehova nchini Bulgaria, lililofanyiwa kwenye jiji la Plovdiv.

Ninarudi Lovech

Ingawa nilijua kwamba si jambo rahisi kwa msanii kujiruzuku katika mji mdogo, niliamua kwamba baada ya kuhitimu ningerudi kwenye mji wa Lovech. Nilitambua kwamba itakuwa vigumu kwangu kufanya kazi ya usanii kwa mafanikio na wakati huohuo kutanguliza Ufalme wa Mungu maishani mwangu. Kwa hiyo, niliamua kubadili kazi na kujitolea kuwa mwalimu wa Biblia. Nilipokuwa bado katika Chuo cha Sanaa, tayari Yanita, aliyekuwa amehitimu miaka mitatu kabla yangu, alikuwa akifundisha kweli za Biblia kwa bidii huko Lovech. Yeye ndiye aliyekuwa Shahidi pekee huko.

Kufikia wakati nilipohamia tena Lovech, kulikuwa na kikundi kidogo cha watu waliokuwa wakijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Nilifurahia kabisa kuwatembelea watu nyumba kwa nyumba na kuwapa tumaini la wakati ujao nililokuwa nimepata. Niliamua kufanya kazi hiyo wakati wote.

Hata hivyo, matatizo yalianza kutokea. Mnamo 1994, usajili wa kisheria wa tengenezo letu la kidini ulifutwa na vyombo vya habari vikaanzisha kampeni kubwa sana ya kueneza uvumi. * Mara nyingi, Mashahidi walifikishwa kwenye kituo cha polisi na vichapo vyetu vikachukuliwa. Wakati huo mgumu, hatungeweza kukutana katika mahali pa umma. Isitoshe, tulifanya mikutano yetu katika chumba chenye ukubwa wa mita 12 za mraba kando ya nyumba ya Yanita. Pindi moja tulikuwa watu 42 katika chumba hicho kidogo. Ili tusiwasumbue majirani, tulifunga dirisha tulipokuwa tukiimba nyimbo za Ufalme. Wakati mwingine, nje kulipokuwa na joto sana, huwezi kuwazia ndani ya chumba hicho kulikuwa na joto kadiri gani! Lakini tulifurahi sana kuwa pamoja.

Baraka za Yehova

Nilipendezwa sana na bidii ya Yanita kuelekea ibada ya kweli, na baada ya muda uchumba ukaanza. Tulifunga ndoa Mei 11, 1996 (11/5/1996). Ijapokuwa tuna nyutu tofauti, tunakamilishana kwa njia ya ajabu. Yeye ndiye msaidizi na rafiki yangu wa karibu zaidi. Ninamshukuru sana Yehova kwa kunipa mke ambaye “thamani yake inapita sana ile ya marijani.”—Methali 31:10.

Baadhi ya rafiki zangu wa zamani wamekuwa wasanii maarufu, kama nilivyotamani hapo zamani. Hata hivyo, ninashukuru kwamba nilichagua kazi nzuri zaidi. Nimewasaidia watu wengi kupata kusudi maishani, nao sasa ni ndugu na dada zangu wa kiroho. Umaarufu wowote ambao ningepata nikiwa msanii hauwezi kulinganishwa na baraka ambazo nimefurahia katika utumishi wa Yehova. Ninafurahi sana kwamba nilipata kumjua vizuri yule Msanii mkuu zaidi, Yehova Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Vichapo hivyo vimechapishwa na Mashahidi wa Yehova. Kitabu Kuishi Milele sasa hakichapishwi tena.

^ fu. 22 Mnamo mwaka wa 1998, baada ya kukata rufaa kwa Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu huko Strasbourg, tengenezo la Mashahidi wa Yehova liliandikishwa tena kisheria nchini Bulgaria.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nikiwa na mke wangu, Yanita