Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ngono Itaboresha Uhusiano Wetu?

Je, Ngono Itaboresha Uhusiano Wetu?

Vijana Huuliza

Je, Ngono Itaboresha Uhusiano Wetu?

Heather wamekuwa na uhusiano na Mike kwa miezi miwili tu, lakini anahisi ni kana kwamba amemfahamu kwa muda mrefu. Wao huandikiana ujumbe mfupi mara kwa mara, nao huzungumza kwa saa nyingi kwenye simu, na hata nyakati nyingine ni kama wanajua yule mwingine anataka kusema nini hata kabla hajalisema! Lakini sasa, wakiwa wameketi ndani ya gari lililoegeshwa na mwezi ukiwa unaangaza, Mike hataki tu wazungumze.

Katika miezi miwili iliyopita, Mike na Heather wamekuwa wakishikana mikono na kubusiana. Heather hataki mambo yazidi hapo. Lakini pia hataki Mike amwache. Ni yeye tu anayemfanya ajihisi kuwa mrembo na wa pekee. Heather anajiambia hivi: ‘Lakini, si mimi na Mike tunapendana, . . . ama?’

HUENDA tayari unajua mambo hayo yataishia wapi. Lakini huenda usitambue jinsi ambavyo uhusiano wa Mike na Heather utaharibika kwa sababu ya kufanya ngono. Fikiria hili:

Ukikiuka sheria ya asili, kama vile sheria ya uvutano, utapatwa na madhara. Ni hali moja na unapokiuka sheria za maadili, kama ile inayosema: ‘Jiepushe na uasherati.’ * (1 Wathesalonike 4:3) Kukosa kutii amri hiyo kuna matokeo gani? Biblia inasema: “Aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 6:18) Je, hilo ni kweli? Jaribu kuorodhesha madhara matatu yanayoweza kuwapata wale wanaofanya ngono kabla ya ndoa.

1. ․․․․․

2. ․․․․․

3. ․․․․․

Sasa tazama tena mambo uliyoandika. Je, ulitia ndani mambo kama vile magonjwa ya zinaa, mimba haramu, au kupoteza kibali cha Mungu? Bila shaka, hayo ni madhara mabaya ambayo yanaweza kumpata mtu yeyote anayekiuka sheria ya Mungu ya maadili kuhusu uasherati.

Hata hivyo, unaweza kushawishiwa. Unaweza kujiambia, ‘Sitapatwa na madhara yoyote.’ Si kila mtu anafanya ngono? Vijana wenzako shuleni wanajisifu kuhusu walivyofanya ngono, na ni kana kwamba wao hawajaumia. Huenda, kama Heather aliyetajwa mwanzoni, unahisi kwamba ngono itawafanya muwe na uhusiano wa karibu. Isitoshe, hakuna mtu anayependa kuchekwa kwa sababu yeye ni bikira. Je, si afadhali kukubali tu kufanya ngono?

Hebu tua na ufikiri. Kwanza kabisa, si kila mtu anayefanya ngono. Ni kweli kwamba unaweza kusoma takwimu zinazoonyesha kwamba vijana wengi sana wanafanya ngono. Kwa mfano, uchunguzi uliofanywa nchini Marekani ulionyesha kwamba kufikia wakati wanapomaliza shule, vijana 2 kati ya 3 nchini humo huwa wamefanya ngono. Lakini pia hilo linamaanisha kwamba 1 kati ya 3 hawafanyi, na hiyo ni idadi kubwa sana. Lakini, vipi kuhusu wale ambao wamefanya ngono? Wachunguzi wamegundua kwamba vijana wengi kati ya hao hupatwa na angalau moja kati ya matatizo yafuatayo.

Tatizo la 1: KUSHUKA MOYO. Vijana wengi ambao wamefanya ngono kabla ya ndoa wanasema kwamba walijuta baadaye.

Tatizo la 2: KUTOAMINIANA. Baada ya kufanya ngono kila mmoja huanza kujiuliza, ‘Amewahi kufanya ngono na nani mwingine?’

Tatizo la 3: KUKOSA USHIKAMANIFU. Baada ya kufanya ngono, kuna uwezekano mkubwa kwamba mvulana atamwacha msichana na kutafuta mwingine.

Tatizo la 4: KUKOSA KUONA MAMBO KIHALISI. Moyoni mwake, msichana angependa kuwa na mtu atakayemlinda, si mtu anayetaka tu kumtumia.

Mbali na mambo ambayo yametajwa kwenye ukurasa uliotangulia, fikiria hili: Wavulana wengi wamesema kwamba hawawezi kumwoa msichana ambaye wamefanya ngono naye. Kwa nini? Kwa sababu wangependa kuwa na mtu anayeshikilia maadili!

Je, hilo linakushangaza, au hata kukuudhi? Ikiwa ndivyo, iwe wewe ni msichana au mvulana, kumbuka jambo hili: Kufanya ngono kabla ya ndoa ni tofauti na vile inavyoonyeshwa kwenye sinema na televisheni. Vyombo vya habari huonyesha ngono kati ya vijana kuwa jambo zuri sana na kuifananisha na upendo wa kweli. Lakini usidanganyike! Wale wanaojaribu kukuchochea ufanye ngono wanatafuta faida zao wenyewe. (1 Wakorintho 13:4, 5) Je, mtu ambaye anakupenda kikweli anaweza kuhatarisha hali yako ya kimwili na ya kihisia? (Methali 5:3, 4) Na je, mtu anayekujali kikweli anaweza kukushawishi uhatarishe uhusiano wako pamoja na Mungu?—Waebrania 13:4.

Ukweli ni kwamba ukikubali kufanya ngono kabla ya ndoa, utakuwa unajishusha na kutoa kitu chenye thamani sana. (Waroma 1:24) Si ajabu kwamba watu wengi hujihisi hawafai wala hawana thamani, kana kwamba wameruhusu wanyang’anywe kitu fulani chenye thamani! Usiruhusu jambo hilo likupate. Mtu akijaribu kukushawishi ufanye ngono kwa kukuambia, “Ikiwa unanipenda, utakubali,” mjibu hivi, “Ikiwa unanipenda, hutaniomba nifanye hivyo!”

Mwili wako ni wenye thamani sana, usiache utumiwe ovyoovyo. Onyesha kwamba una nguvu za kutii amri ya Mungu ya kujiepusha na uasherati. Kisha, utakapofunga ndoa, unaweza kufanya ngono. Na utaifurahia kabisa, bila wasiwasi, kujuta, na mahangaiko ambayo mara nyingi yanakuja mtu anapofanya ngono kabla ya ndoa.—Methali 7:22, 23; 1 Wakorintho 7:3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Zaidi ya kufanya ngono, neno “uasherati” linalotajwa katika Biblia linatia ndani matendo mengine pia kati ya watu ambao hawajaoana kama vile kumpiga mtu mwingine punyeto na pia ngono ya kinywa na ulawiti au ufiraji. Kwa habari zaidi, ona kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, ukurasa wa 42-47.

MAMBO YA KUFIKIRIA

● Kwa nini hupaswi kufanya ngono kabla ya ndoa hata ingawa huenda ukashawishiwa kufanya hivyo?

● Utafanya nini mtu akikuomba mfanye ngono?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Kukataa tu mara ya kwanza hakutamzuia mtu asijaribu tena. Atazuiwa tu na jinsi unavyoonyesha msimamo wako. Ukikataa kwa unyonge lakini ni kama humaanishi hivyo, itaonekana wazi. Unahitaji kuwa imara!”

“Haitoshi kukataa tu. Huenda pia isitoshe kueleza kuhusu imani yako. Ninajua vijana fulani ambao hujigamba kwamba wamewahi kumshawishi Mkristo. Nyakati nyingine lazima uondoke. Ni vigumu kufanya hivyo lakini utafaulu.”

“Ukiwa Mkristo, una sifa zinazowavutia wengine. Kwa hiyo, unapaswa kuwa chonjo na kukataa unapoalikwa kujihusisha katika ukosefu wa maadili. Thamini sifa hizo. Usitende kijinga!”

[Picha]

Diana

James

Joshua

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

UWE MWANAMUME HALISI!

Ikiwa mmeanzisha urafiki wa karibu, je, unamjali msichana huyo? Basi onyesha kwamba una . . .

nguvu za kufuata sheria za Mungu

hekima ya kuepuka hali zenye kushawishi

upendo wa kujali faida zake

Ukifanya hivyo, huenda msichana huyo akahisi kama vile Mshulami aliyesema: “Mpenzi wangu ni wangu nami ni wake.” (Wimbo wa Sulemani 2:16) Bila shaka, utakuwa mwanamume halisi!

Ona Methali 22:3; 1 Wakorintho 6:18; 13:4-8.

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

PENDEKEZO

Inapohusu uhusiano na watu wa jinsia tofauti, ni vizuri kufuata sheria hii: Ikiwa ni jambo ambalo hungependa wazazi wako wakutazame ukifanya, basi hupaswi kulifanya.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kufanya ngono kabla ya ndoa ni kutumia vibaya zawadi uliyopewa na Mungu. Ni kama kuchukua mchoro mzuri uliopewa na mtu na kuutumia kama tambara la mlangoni