Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Inamaanisha Nini Kugeuza Shavu Lile Lingine?

Inamaanisha Nini Kugeuza Shavu Lile Lingine?

Maoni ya Biblia

Inamaanisha Nini Kugeuza Shavu Lile Lingine?

KATIKA Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu Kristo alisema: “Msimpinge yeye aliye mwovu; bali yeyote anayekupiga kofi kwenye shavu lako la kuume, mgeuzie lile lingine pia.”—Mathayo 5:39.

Alimaanisha nini? Je, alikuwa akiwahimiza Wakristo wakae kimya wanaposhambuliwa? Je, Wakristo wavumilie mateso bila kutafuta msaada wa kisheria?

Yesu Alimaanisha Nini?

Ili kuelewa Yesu alimaanisha nini, lazima tuchunguze muktadha na pia tuwafikirie wasikilizaji wake. Yesu alianza shauri lake lililonukuliwa hapo juu kwa kuwaambia wasikilizaji wake mambo ambayo tayari waliyajua kutoka katika Maandiko Matakatifu. Alisema: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Jicho kwa jicho na jino kwa jino.’”—Mathayo 5:38.

Mistari ambao Yesu alitaja inapatikana kwenye Kutoka 21:24 na Mambo ya Walawi 24:20. Inafaa kuzingatia kwamba kupatana na Sheria ya Mungu, adhabu ya “jicho kwa jicho” inayotajwa katika maandiko hayo ilitekelezwa tu baada ya mkosaji kuletwa mbele ya makuhani na waamuzi ambao walichunguza hali zilizohusika na ikiwa kosa lilifanywa kimakusudi.—Kumbukumbu la Torati 19:15-21.

Baada ya muda, Wayahudi walipotosha sheria hiyo. Kitabu kinachofafanua Biblia kilichoandikwa katika karne ya 19 na Adam Clarke kinasema hivi: “Inaonekana kwamba Wayahudi walikuwa wakitumia sheria hii [jicho kwa jicho, jino kwa jino] ili kujitetea kwamba wanaweza kuwachukia wengine na kulipiza kisasi. Mara nyingi matendo ya kulipiza kisasi yalipita mipaka, na yule aliyelipiza kisasi alitenda maovu yaliyopita yale aliyotendewa.” Hata hivyo, Maandiko hayakutoa idhini ya kulipizia kisasi mambo ya kibinafsi.

Mafundisho ambayo Yesu alitoa katika Mahubiri yake ya Mlimani kuhusu ‘kugeuza shavu lile lingine’ yanaonyesha maana halisi ya Sheria ya Mungu kwa Israeli. Yesu hakumaanisha kwamba ikiwa wafuasi wake wangepigwa kofi kwenye shavu moja, walipaswa kujikakamua na kugeuza shavu lile lingine pia lipigwe kofi. Katika nyakati za Biblia, sawa na ilivyo leo, kofi halikukusudiwa kumwumiza mtu bali lilikuwa kama kumdharau mtu ili kumfanya akasirike na kupigana.

Basi ni wazi kwamba Yesu alimaanisha kwamba mtu akijaribu kumchochea mwingine apigane naye iwe ni kwa kumpiga kofi kihalisi, au kwa maneno ya kejeli yenye kuumiza, mtu aliyechokozwa anapaswa kuepuka kulipiza kisasi. Badala yake, anapaswa kuepuka kutenda katika njia ambayo itatokeza matendo mengine ya kulipiza kisasi.—Waroma 12:17.

Maneno ya Yesu yalifanana sana na yale ya Mfalme Sulemani: “Usiseme: ‘Nitamtendea kama vile tu alivyonitendea. Nitamlipa kila mtu kulingana na tendo lake.’” (Methali 24:29) Mfuasi wa Yesu atageuza shavu lile lingine kwa kutoruhusu wengine wamlazimishe kupigana.—Wagalatia 5:26.

Namna Gani Kutumia Nguvu ili Kujilinda?

Kugeuza shavu lile lingine hakumaanishi kwamba Mkristo hatajilinda anaposhambuliwa vikali. Yesu hakuwa akisema kwamba hatupaswi kamwe kujilinda, badala yake, hatupaswi kushambulia wala kujiruhusu kuchochewa kulipiza kisasi. Ingawa ni jambo la hekima kuondoka ikiwezekana ili kuepuka kupigana, inafaa kuchukua hatua za kujilinda na kutafuta msaada wa polisi ikiwa tumetendewa uhalifu.

Wafuasi wa Yesu wa mapema walitumia kanuni hiyo walipokuwa wakitetea haki zao za kisheria. Kwa mfano, mtume Paulo alitumia mfumo wa sheria uliokuwapo wakati wake ili kutetea haki yake ya kuhubiri kupatana na agizo ambalo Yesu aliwapa wafuasi wake. (Mathayo 28:19, 20) Alipokuwa akihubiri katika jiji la Filipi, Paulo na mmishonari mwenzake Sila walikamatwa na wenye mamlaka na kushtakiwa kwamba walivunja sheria.

Walipigwa viboko hadharani kisha wakatupwa gerezani hata bila kesi kufanywa. Alipopata nafasi, Paulo alitumia haki yake akiwa raia wa Roma. Walipogundua kwamba Paulo alikuwa Mroma, wenye mamlaka waliogopa na wakawasihi Paulo na Sila waondoke bila fujo. Kwa hiyo, Paulo aliweka kielelezo cha “kutetea na kuithibitisha kisheria habari njema.”—Matendo 16:19-24, 35-40; Wafilipi 1:7.

Kama Paulo, mara kwa mara imebidi Mashahidi wa Yehova waende kortini ili kutetea haki yao ya kumtumikia Mungu. Wamefanya hivyo hata katika nchi zinazodai kuwapa raia wake uhuru wa kidini. Wanapopatwa na uhalifu au usalama wao unapokuwa hatarini, Mashahidi wa Yehova hawatarajiwi kugeuza lile shavu lingine kwa kubali kuteswa bila kujilinda. Wanachukua hatua za kisheria ili kujilinda.

Hivyo, wakiwa Wakristo, Mashahidi huchukua hatua zinazopaswa kuchukuliwa ili kutetea haki zao za kisheria ingawa wanajua kwamba hatua hizo huwa na mafanikio madogo. Kwa hiyo, kama Yesu, wao humwachia Mungu mambo yote, wakiwa na uhakika kwamba atatenda kwa kuzingatia mambo yote na atalipiza kisasi kwa kutumia njia itakayoonyesha haki kamilifu. (Mathayo 26:51-53; Yuda 9) Wakristo wa kweli hukumbuka kwamba kisasi ni cha Yehova.—Waroma 12:17-19.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Wakristo wanapaswa kuepuka kutenda kwa njia gani?—Waroma 12:17.

● Je, Biblia inakataza mtu kutumia sheria kujilinda?—Wafilipi 1:7.

● Yesu alikuwa na uhakika gani katika Baba yake?—Mathayo 26:51-53.