Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Ni Mtu Halisi?

Je, Mungu Ni Mtu Halisi?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Ni Mtu Halisi?

WATU wanapovutiwa sana na uumbaji, wanalazimika kuamini kwamba kuna nguvu fulani zisizo za asili, yaani, mungu fulani. Je, unastaajabishwa na utata wa ulimwengu? Je, unastaajabu kuona maajabu ya asili katika sayari yetu na jinsi mwili wa binadamu ulivyobuniwa kwa njia ya ajabu?

Ikiwa ndivyo, basi huenda wewe pia umeshawishiwa kuamini kwamba kuna nguvu fulani inayozidi ile ya kibinadamu. Dini fulani zinafundisha kwamba nguvu kama hiyo inaishi milimani, kwenye miti, angani, na kwenye sehemu nyingine za ulimwengu. Wengine huamini kwamba roho nzuri za mababu waliokufa na nyingine mbaya, huungana katika mchanganyiko wa nguvu mbalimbali zisizoeleweka na kufanyiza Mtu Mkuu Kuliko Wote—Mungu!

Vyovyote vile, watu wengi huamini kwamba nguvu hiyo isiyo ya asili haina utu. Watu wengi huona ni vigumu kuamini kwamba Mungu ana mawazo, hisia, kusudi, na tamaa. Je, Mungu ni mtu halisi? Biblia, kitabu cha kale zaidi kati ya vitabu vitakatifu vinavyosambazwa sana leo, inatupa jibu la wazi.

Wanadamu Wanafunua Utu wa Mungu

Biblia inafundisha kwamba mtu aliumbwa ili aige sifa za Mungu. Mwanzo 1:27 inasema kwamba ‘Mungu alimuumba mtu kwa mfano wake.’

Kwa kweli, maneno hayo hayamaanishi kwamba wanadamu wa kwanza walifanana kihalisi na Mungu. Biblia inasema kwamba Mungu ni roho isiyoweza kuonekana, ilhali wanadamu wameumbwa kutokana na vitu vinavyoonekana vya dunia. (Mwanzo 2:7; Yohana 4:24) Hata ingawa kuna tofauti hiyo ya msingi kati ya Mungu na wanadamu, unapochunguza sifa za wanadamu kwa kina utaelewa kwa kiasi fulani utu wa Mungu.

Wanadamu wana uwezo wa kutawala na kutenda kama wanavyotaka. Wanaweza kutenda kwa njia hiyo wakiongozwa na sifa kama vile fadhili, uwezo wa kufikiri, hekima inayotumika, na haki. Wanadamu wana hisia zinazotofautiana kwa kuwa wanaweza kuonyesha upendo mwororo na pia wawe na chuki na hasira. Sisi hutofautiana ikitegemea tunaonyesha sifa hizo kwa kadiri gani. Ndiyo, kila mmoja wetu ana utu wa pekee.

Je, ingepatana na akili kwamba Mungu alituumba kwa njia ya ajabu ikiwa yeye ni nguvu isiyo na utu inayorukaruka ovyoovyo angani? Ikiwa wanadamu wameumbwa kwa mfano wa Mungu, basi huenda utu wa Mungu unafanana kwa njia nyingi na ule wa binadamu. Fikiria mambo yafuatayo.

Mungu ana jina la kibinafsi. Katika Isaya 42:8, Biblia inasema hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.” Mungu anataka jina lake lijulikane. Biblia pia inasema hivi: “Jina la Yehova na libarikiwe kutoka sasa mpaka wakati usio na kipimo. Kutoka mapambazuko ya jua mpaka kutua kwake jina la Yehova ni la kusifiwa.” (Zaburi 113:2, 3) Hivyo, waabudu wa Mungu wanapotumia jina lake kwa ukawaida, wao humwona kuwa mtu.

Mungu ni wa pekee. Biblia inafundisha kwamba Mungu ni mtu wa pekee sana. (1 Wakorintho 8:5, 6) Biblia inasema: “Wewe kwa kweli ni mkuu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova; kwa kuwa hakuna mwingine kama wewe, wala hakuna Mungu ila wewe.” (2 Samweli 7:22) Pia Maandiko yanamtaja Yehova kuwa “Mungu wa kweli mbinguni juu na duniani chini. Hakuna mwingine.”—Kumbukumbu la Torati 4:39.

Yehova Mungu anachukia uovu. Ni mtu tu anayeweza kuwa na hisia za chuki. Biblia inatueleza kwamba Muumba anachukia “macho ya majivuno, ulimi wa uwongo, na mikono inayomwaga damu isiyo na hatia, moyo unaotunga hila zenye kuumiza, miguu iliyo myepesi kukimbilia ubaya, shahidi wa uwongo anayesema uwongo, na yeyote anayetokeza magomvi kati ya ndugu.” (Methali 6:16-19) Ona kwamba Mungu anachukizwa na matendo ya wanadamu yanayowaumiza wanadamu wengine. Kutokana na hayo, tunajifunza kwamba Mungu anajali masilahi yetu na anachukizwa na mambo yanayotudhuru.

Yehova ni Mungu mwenye upendo. Biblia inasema kwamba Mungu anawapenda sana “watu wa ulimwengu huu.” (Yohana 3:16, Contemporary English Version) Inaonyesha kwamba ana utu kama ule wa baba mpole anayewatakia mema watoto wake wa kibinadamu. (Isaya 64:8) Wanadamu wanaweza kupata baraka nyingi wakimwona Mungu kuwa Baba yao mwenye upendo.

Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu

Ni wazi Biblia inafundisha kwamba Muumba ni mtu halisi, aliye na jina na utu. Ana uwezo wa kutumia nguvu zake na kutenda kwa njia hususa akichochewa na sifa za pekee kama vile fadhili, hekima, na haki. Anaweza kufikika. Pia, anasema hivi: “Mimi, Yehova Mungu wako, ninaushika mkono wako wa kuume, Mwenye kukuambia, ‘Usiogope. Mimi mwenyewe nitakusaidia.’”—Isaya 41:13.

Mungu ana kusudi kwa ajili ya wanadamu. Biblia inasema hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.” (Zaburi 37:29) Tunapojua kwamba Yehova ni wa pekee na ana utu wa kipekee inaweza kuwa rahisi kwetu kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye na kufurahia baraka anazowaahidi wale wanaokuwa rafiki zake.— Kumbukumbu la Torati 6:4, 5; 1 Petro 5:6, 7.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Je, Mungu ana jina la kibinafsi?—Isaya 42:8.

● Je, kuna miungu mingi?—1 Wakorintho 8:5, 6.

● Je, wanadamu wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wa kweli?—1 Petro 5:6, 7.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Je, inawezekana kwamba Mungu alituumba kwa njia ya ajabu ikiwa yeye ni nguvu isiyo na utu?