Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Amenifariji Katika Majaribu Yote

Mungu Amenifariji Katika Majaribu Yote

Mungu Amenifariji Katika Majaribu Yote

Limesimuliwa na Victoria Colloy

Daktari alimwambia mama yangu hivi: “Hatuwezi kufanya jambo lolote la ziada kwa ajili ya binti yako. Atalazimika kutumia mikongojo na kuvalia vifaa vya kutegemeza viungo maisha yake yote.” Nilihuzunika sana! Maisha yangu yangekuwaje ikiwa singeweza kutembea?

NILIZALIWA Novemba 17, 1949 (17/11/1949), huko Tapachula, Chiapas, nchini Mexico. Nilikuwa mtoto mwenye furaha na afya, nami ndiye niliyekuwa wa kwanza katika familia ya watoto wanne. Lakini kwa ghafula nilipokuwa na umri wa miezi sita singeweza tena kutambaa na nilisonga kwa shida. Baada ya miezi miwili singeweza kusonga hata kidogo. Madaktari walishangaa, kwa kuwa watoto wengine huko Tapachula walikuwa na dalili hizo pia. Kwa hiyo, daktari wa matatizo ya mifupa alikuja kutoka Mexico City na akatuchunguza. Alisema kwamba tulikuwa na polio, yaani, ugonjwa unaowafanya watoto wapooze.

Nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, nilifanyiwa upasuaji wa nyonga, magoti, na vifundo vya miguu. Baadaye, bega langu la kulia liliathiriwa pia. Nilipokuwa na umri wa miaka sita, nilipelekwa huko Mexico City ili nikatibiwe katika hospitali ya watoto. Mama alifanya kazi katika shamba fulani huko Chiapas, kwa hiyo niliishi na nyanya yangu huko Mexico City. Hata hivyo, kwa muda mrefu nilikuwa hospitalini.

Nilipokuwa na umri wa miaka minane hivi, nilipata nafuu kidogo. Lakini baadaye hali yangu ikawa mbaya zaidi, na nikapoteza uwezo mdogo wa kusonga niliokuwa nao. Hapo ndipo madaktari walisema ningelazimika kutumia mikongojo na vifaa vya kutegemeza viungo maisha yangu yote.

Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilikuwa nimefanyiwa upasuaji mara 25. Nilifanyiwa upasuaji kwenye uti wa mgongo, miguu, magoti, vifundo vya miguu, na vidole vya miguu. Baada ya kila upasuaji, nilipitia kipindi cha kufanya mazoezi. Baada ya upasuaji mmoja, miguu yangu ilifungwa kwa plasta. Ilipoondolewa nilihitaji kufanya mazoezi yenye maumivu sana.

Napata Faraja ya Kweli

Nilipokuwa na umri wa miaka 11, Mama alinitembelea baada ya upasuaji. Alikuwa amejifunza kwamba Yesu aliwaponya wagonjwa na hata kumfanya mtu aliyepooza aweze kutembea. Alinipa nakala ya gazeti Mnara wa Mlinzi, linalochapishwa na Mashahidi wa Yehova, ambalo alikuwa amejifunza mambo hayo. Nilificha gazeti hilo chini ya mto wangu, lakini siku moja likapotea. Wauguzi walikuwa wamepata gazeti hilo na wakalichukua. Walinigombeza sana kwa kulisoma.

Mwaka mmoja hivi baadaye, Mama alinitembelea tena kutoka Chiapas. Wakati huo alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi. Aliniletea kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana. * Mama aliniambia, “Ukitaka kuishi katika ulimwengu mpya ulioahidiwa ambako Yesu atakuponya, lazima ujifunze Biblia.” Kwa hiyo, licha ya upinzani wa Nyanya, nilianza kujifunza na Mashahidi nilipokuwa na umri wa miaka 14 hivi. Mwaka uliofuata nililazimika kuondoka hospitali hiyo kwa sababu ilikuwa ya watoto wadogo peke yao.

Kukabiliana na Hali Ngumu

Nilishuka moyo sana. Kwa sababu ya upinzani wa nyanya yangu, nililazimika kurudi Chiapas nikaishi na wazazi wangu. Hata hivyo, kulikuwa na matatizo nyumbani kwa kuwa Baba alikuwa akitumia kileo vibaya. Wakati fulani niliona hakukuwa na sababu ya kuendelea kuishi. Hata nilifikiria kujiua. Lakini kadiri nilivyoendelea kujifunza Biblia, maoni yangu yalibadilika. Ahadi ya Biblia ya dunia paradiso ilinifurahisha sana.

Nilianza kuwaambia wengine kuhusu tumaini la ajabu ambalo Biblia inatoa. (Isaya 2:4; 9:6, 7; 11:6-9; Ufunuo 21:3, 4) Mwishowe, Mei 8, 1968 (8/5/1968) nilipokuwa na umri wa miaka 18, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Tangu mwaka wa 1974, nimekuwa nikitumia zaidi ya saa 70 kila mwezi kuwaeleza wengine kuhusu tumaini lililonichochea kuendelea kuishi.

Nimekuwa na Maisha Yenye Utendaji na Uradhi

Baada ya muda, mimi na Mama tulihamia kwenye jiji la Tijuana, karibu na mpaka wa Mexico na Marekani. Mimi na Mama tuliishi pamoja katika nyumba iliyofaa mahitaji yetu. Bado ninaweza kutembea ndani ya nyumba kwa kutumia vifaa vya kutegemeza viungo na mikongojo, na ninatumia kiti cha magurudumu kinachoniwezesha kupika na hata kufua na kupiga pasi nguo zangu. Ninapokuwa katika utumishi, ninatumia gari linaloendeshwa kwa umeme ambalo limeundwa ili lifae hali zangu.

Mbali na kuzungumza kuhusu mafundisho ya Biblia na watu barabarani na nyumbani kwao, mimi huenda kwenye hospitali fulani iliyo karibu na kuwa na mazungumzo ya Biblia pamoja na wale walio nje wakisubiri kutibiwa. Ninapomaliza kuzungumza nao, ninaendesha gari langu hadi sokoni ambako ninanunua chochote tutakachohitaji kisha ninarudi nyumbani nikamsaidie Mama kupika na kufanya kazi za nyumbani.

Ili kushughulikia mahitaji ya kimwili, mimi huuza nguo za mitumba. Sasa Mama ana umri wa miaka 78 na hawezi kufanya mengi kwa kuwa amepatwa na mshtuko wa moyo mara tatu. Kwa hiyo, mimi humnunulia dawa na chakula. Licha ya kwamba hatuna hali nzuri ya afya, tunajitahidi kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Zaidi ya watu 30 ambao nimejifunza nao Biblia tangu zamani sasa wanashiriki katika huduma ya Kikristo.

Nina hakika kwamba ahadi hii ya Biblia mwishowe itatimia: “Wakati huo [katika ulimwengu mpya wa Mungu] kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya.” Kwa sasa, maneno haya ya Mungu hunifariji: “Usiogope, kwa maana mimi nipo pamoja nawe. Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli. Nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.”—Isaya 35:6; 41:10. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 1958 lakini sasa hakichapishwi tena.

^ fu. 18 Victoria Colloy alikufa Novemba 30, 2009, akiwa na umri wa miaka 60. Mama yake alikufa Julai 5, 2009 (5/7/2009).

[Picha katika ukurasa wa 12]

Nikiwa na vifaa vya kutegemeza viungo nikiwa na umri wa miaka saba

[Picha katika ukurasa wa 13]

Ninapokuwa katika utumishi mimi hutumia gari linaloendeshwa kwa umeme ambalo limeundwa ili lifae hali zangu