Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uzuri na Umaridadi Wenye Kustaajabisha

Uzuri na Umaridadi Wenye Kustaajabisha

Uzuri na Umaridadi Wenye Kustaajabisha

“Nilivutiwa upesi sana na farasi. Ni wanyama maridadi na wenye madaha ya kipekee.”—TOMASZ, MFUGAJI STADI WA FARASI.

WATU wengi husema kwamba farasi ndio wanyama maridadi zaidi, na wanapendwa kwa sababu ya madaha na nguvu zao zisizoweza kuzuiwa wanaposimama kwa miguu ya nyuma pekee, wanapopiga ardhi kwa kwato zao, wanapopiga kelele kwa majivuno, na kusonga kwa ujasiri. Kwa kweli, wao ni wanyama maridadi sana.

Kwa karne nyingi, farasi wa aina mbalimbali wamezalishwa katika maeneo tofauti-tofauti. Farasi wa Arabia ndiye anayesemwa kuwa farasi maridadi kati ya wote. Anasemwa kuwa mwenye damu moto, kwa kuwa ana nguvu, mbio, hachoki upesi, na ana akili, sifa ambazo humfanya afae sana katika michezo.

Kwa kushangaza, nchi ya Poland, iliyo katika Ulaya ya Kati, inazalisha farasi wengi sana wa aina hiyo. Wafugaji na wataalamu vilevile wanasema kwamba nchi ya Poland ndiyo chanzo cha farasi wa Arabia ambao chembe zao za urithi hazijachanganywa na za farasi wengine. Kwa nini inasemwa hivyo? Tuliwauliza wafugaji na wataalamu wengine wa farasi swali hilo na maswali mengine.

Maoni ya Wanaompenda Farasi Huyo

Acha tuanze kwa kuchunguza zaidi kuhusu farasi huyo wa Arabia. Watu humhusianisha na Mashariki ya Kati. Tomasz, mfugaji stadi wa farasi, anaeleza hivi: “Kwa karne nyingi, makabila ya Wabedui yalihakikisha kwamba chembe za urithi za farasi huyo wa Arabia hazichangamani na za farasi wengine. Kwa sababu ya kushikilia sana jambo hilo na utunzaji mzuri wa wafugaji, farasi huyo bora wa Arabia alitokezwa. Wengi kati ya farasi hao ni wa rangi ya kijivu, mchanganyiko wa rangi nyekundu na kahawia, au mchanganyiko wa kijivu, nyekundu, na kahawia; farasi wachache sana kati yao ni weusi.”

Żaneta, ambaye hufuga farasi huyo wa Arabia, anasema hivi: “Wao ni maridadi sana na wanasemwa kuwa farasi wa zamani zaidi na ambao chembe zao za urithi hazijachanganywa na farasi wengine.” Mbali na hasira yao kali, farasi hao wanajulikana pia kwa ujasiri na nguvu zao. Mapafu yenye nguvu ya farasi huyo wa Arabia—yaliyofichwa katika kifua chake kikubwa—humfanya afae sana kwa ajili ya safari za mbali.

Kutoka Arabia Hadi Poland

“Farasi hao wa Arabia walifika Poland jinsi gani?” tulimwuliza Tomasz, ambaye ana farasi wa kiume katika shamba lake wanaotumiwa kutunga mimba. Alitueleza hivi: “Huenda waliletwa na mmoja wa wajumbe wa mfalme alipokuwa akirudi kutoka kwenye moja ya safari zake nyingi kwenye makao ya sultani huko Stambul katika karne ya 16. Hata hivyo, kinachojulikana kabisa ni kwamba programu za uzalishaji nchini Poland zilianza katika karne ya 18.” Izabela Pawelec-Zawadzka, mfugaji stadi wa farasi wa Arabia, anataja kuhusu fungu ambalo Bwana Wacław Rzewuski alitimiza. Kwa kuwa alifahamu vizuri utamaduni wa Asia, yeye ndiye “aliyefanya mipango ili farasi hao waletwe kutoka Arabia,” naye alisafirisha farasi 137 hadi Ulaya ambao hawajachanganywa chembe za urithi.

Kwa sababu ya bidii ya Rzewuski, shamba la kwanza la Farasi wa kiume wa Arabia nchini Poland lilianzishwa huko Janów Podlaski, Poland Mashariki, katika mwaka wa 1817. Tomasz anaeleza hivi: “Ilionekana kwamba mambo yameanza vizuri. Wafugaji stadi waliwatunza farasi hao. Lakini vile vita viwili vya ulimwengu, ambavyo vilipiganwa hasa Ulaya, viliharibu kabisa mashamba ya farasi wa kiume ya Poland. Farasi wengi walikufa, wakatoroka, au wakaibwa.” Hata hivyo, muda fulani baada ya vita vya pili vya ulimwengu, programu ya uzalishaji ilianzishwa tena.

Sasa farasi hao kutoka Arabia wanafugwa katika mashamba 30 hivi nchini Poland. Miaka mia mbili ya kazi hii inahakikisha kwamba farasi bora zaidi wanazaliwa. Kwa sababu hiyo, Poland imekuwa moja kati ya vituo maarufu zaidi vya kuzalisha farasi wa Arabia, na kuwavutia wataalamu na watu wanaopenda farasi kutoka sehemu zote ulimwenguni wahudhurie maonyesho ya kila mwaka yenye fahari na ya kupiga farasi mnada.

Kuwatunza Farasi wa Arabia

Mfugaji wa farasi wa hali ya juu waliotokana na familia isiyochanganywa chembe za urithi anapaswa kuwatunza vizuri sana. Małgorzata, mmiliki mmoja wa shamba la farasi hao, anaeleza hivi: “Ni jambo tata sana kumtunza farasi wa Arabia. Tunahitaji kumlisha farasi huyo chakula kinachofaa kabisa ili kuhakikisha kwamba anaendelea kuwa na afya bora na kudumisha umaridadi wake. Farasi walio na mimba wanahitaji utunzaji wa pekee hata zaidi.” * Ni chakula gani kinachomfaa farasi huyo wa Arabia?

Małgorzata anaendelea kusema hivi: “Asubuhi tunaanza kwa kuwalisha nyasi kavu, ambazo huwapa virutubisho vyote wanavyohitaji kutia ndani vitamini na madini. Aina fulani ya shayiri inayoitwa oats iliyochanganywa na makapi au nyasi huwa na virutubisho vingi; pia shayiri na ngano ni vyakula vinavyowafaa. Lakini farasi hao hupenda hasa chakula cha kijani kibichi—nyasi au alfalfa kutia ndani viazi, karoti, na viazisukari. Katika majira ya baridi kali, mara nyingi wazalishaji hununua mchanganyiko wa vyakula vilivyo na protini nyingi. Pia, farasi wa Arabia wanahitaji kuramba chumvi—chumvi huwa na madini au miti-shamba ambayo huwasaidia watulize hasira yao kali. Hata hivyo, lazima isemwe wazi kwamba hata nyasi kavu au chakula bora zaidi kilichonunuliwa hakiwezi kushinda nyasi za malishoni. Na jambo lingine, farasi wanahitaji kupata maji safi ya kunywa kila wakati—hawawezi kunywa maji machafu.”

Utunzaji wa farasi wa Arabia unatia ndani kushughulikia ngozi na manyoya yake. Hilo linamaanisha wanapaswa kuoshwa kwa uangalifu, kukandwa kwa brashi za pekee, na kupapaswa kwa mikono. Hata hivyo, mengi zaidi yanahusika, kama Tomasz anavyoeleza: “Ni muhimu sana kusafisha kwato zao kila siku, kwa kuwa hilo litazuia wasipatwe na aina mbalimbali za magonjwa, kutia ndani kansa. Lazima pia tuhakikishe tunasafisha macho, mapua, midomo, na masikio ya farasi huyo.” Żaneta anaongezea hivi: “Ili farasi awe na afya na aonekane maridadi anahitaji kukimbia na pia anahitaji mchanga, matope, au nyasi ili agaegae. Anapotokwa na jasho baada ya kukimbia polepole au haraka, kwanza anapaswa kufunikwa kwa blanketi kisha asafishwe baadaye.”

Wataalamu wanakazia umuhimu wa kumjali kila farasi kihususa. Małgorzata anaeleza hivi: “Inaaminika kwamba farasi wa Arabia wana hisi ya sita—wanapenda kuwa pamoja na mwanadamu, kuguswa na kukumbatiwa. Kutendewa kwa njia hiyo ya kibinadamu humfanya farasi huyo amtumaini yule anayemwendesha hivi kwamba anajitoa kabisa kwa mtu huyo. Imesemwa kwamba wao hutoa sauti wanapoona tabasamu, wanapokumbatiwa, au kulishwa kitu fulani wanachopenda—kama vile karoti au kipande cha sukari. Wale wanaopenda farasi hufurahia sana kuwatunza.” Tomasz anaeleza jinsi anavyowapenda: “Nilivutiwa upesi sana na farasi. Ni wanyama maridadi na wenye madaha ya kipekee. Lakini si rahisi kwao kukuamini. Ilinichukua miaka mingi ili waniamini.”

Wakati Ujao wa Farasi Huyo

Tangu zamani, watu wamefurahishwa na umaridadi, kasi, mwendo, nguvu, na werevu wa farasi, hasa farasi wa Arabia, na wamekuwa na uhusiano wa karibu sana nao. Kwa kusikitisha, uhusiano huo umetumiwa vibaya katika vita ambavyo vimefanya farasi wengi wafe. Hata hivyo, chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, watu watatumia farasi kwa makusudi yenye kuheshimika peke yake—ili kumletea sifa Muumba wao, Yehova Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Mfugaji anaweza kuamua wakati ambapo farasi atazaa. Kwa kawaida, anaweza kuzaa kila mwaka, lakini mara kwa mara anashindwa kufanya hivyo. Katika muda wa maisha yake yenye urefu wa miaka 25 hadi 30, farasi anaweza kuzaa watoto 15 au 18 hivi.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Farasi na mtoto wake

[Picha katika ukurasa wa 16]

Utunzaji wa Kila Siku wa Farasi wa Arabia Unatia Ndani

1. Kupiga brashi ngozi na manyoya yake kwa uangalifu

2. Kusafisha kwato zake

3. Kuwatendea kwa upendo

[Picha katika ukurasa wa 17]

Farasi wa kiume wakicheza kwenye theluji