Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Maneno Yako Ni Muhimu

Kwa Nini Maneno Yako Ni Muhimu

Maoni ya Biblia

Kwa Nini Maneno Yako Ni Muhimu

Baada ya kuzungumza na mwanamke fulani mzee kwa heshima, na bila kujua kwamba mikrofoni haikuwa imezimwa, waziri mkuu anasema kwamba mwanamke huyo anashikilia sana maoni yake bila kutumia akili, kisha analalamika kwamba wafanyakazi wake walipaswa kumzuia. Maneno hayo ya kumchambua mwanamke huyo yanalishtua taifa zima. Jina lake likiwa limechafuka, waziri huyo mkuu anapoteza kiti chake siku nane tu baadaye katika uchaguzi uliofuata.

HAKUNA mwanadamu anayeweza kuuzuia ulimi wake kikamili. (Yakobo 3:2) Lakini, kisa kilichotajwa hapo juu kinaonyesha kwamba maneno yako ni muhimu. Jina lako, kazi yako, na hata mahusiano yako na watu wengine yanategemea maneno unayosema na jinsi unavyoyasema.

Lakini je, ulijua kwamba maneno yako ni muhimu kwa sababu nyingine? Biblia inaeleza kwamba maneno yako huonyesha jinsi ulivyo kwa ndani, utu wako. Yesu alisema: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mathayo 12:34) Kwa kuwa maneno yako huonyesha jinsi unavyohisi na kufikiri, ni muhimu uchunguze usemi wako kwa undani zaidi. Je, Biblia inaweza kukusaidia kufanya hivyo? Fikiria mambo yafuatayo.

Jinsi ya Kuboresha Usemi Wako

Maneno hutungwa na mawazo ya mtu. Ili kuboresha yale unayosema, unahitaji kuboresha jinsi unavyofikiri. Ona jinsi ambavyo kufuata Neno la Mungu kunaweza kuboresha mawazo yako, na hivyo kuboresha usemi wako.

Jaza moyo wako mambo mazuri. Biblia inataja mambo hayo mazuri inaposema: “Mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”Wafilipi 4:8.

Kutii shauri hilo zuri kutakusaidia kuepuka mawazo mabaya. Kumbuka kwamba mawazo yako yanaathiriwa sana na mambo unayoona na kusoma. Kwa hiyo, ili kuepuka mawazo machafu na yasiyofaa, epuka mambo yasiyofaa. Hilo linamaanisha uepuke burudani chafu na yenye jeuri. (Zaburi 11:5; Waefeso 5:3, 4) Badala yake, kazia fikira mambo yaliyo safi na yanayofaa. Biblia inaweza kukusaidia kufanya hivyo. Kwa mfano, soma Methali 4:20-27; Waefeso 4:20-32; na Yakobo 3:2-12. Ona jinsi kufuata kanuni zinazotajwa katika maandiko hayo kunavyoweza kuboresha usemi wako. *

Fikiri kabla ya kusema. “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya,” inasema Methali 12:18. Ikiwa mara nyingi wewe ‘huchoma,’ au kuumiza hisia za wengine, ni vizuri kujitahidi kufikiri kabla ya kusema. Fuata shauri hili zuri linalopatikana kwenye Methali 15:28: “Moyo wa mwadilifu hutafakari ili kujibu, lakini kinywa cha waovu hububujika mambo mabaya.”

Jaribu kuweka mradi. Mwezi wote ujao, azimia kutosema jambo la kwanza linalokuja akilini mwako, hasa unapochokozwa. Badala yake, fikiria maandiko ambayo yametajwa katika habari hii, na ujitahidi sana kuzungumza kwa hekima, upendo, na utulivu. (Methali 15:1-4, 23) Lakini si hayo tu.

Omba msaada wa Mungu. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisali hivi: “Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yawe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova.” (Zaburi 19:14) Mweleze Yehova Mungu kwamba unataka kutumia ulimi katika njia inayompendeza na ambayo itawafanya watu wafurahie kuwa pamoja nawe. Methali 18:20, 21 inasema: “Fanya maneno yako yawe mema—utafurahi kwamba ulifanya hivyo. Maneno yanaweza kutokeza kifo au uhai!”—Contemporary English Version.

Tumia Neno la Mungu kama kioo. Biblia ni kama kioo ambacho unaweza kutumia kujichunguza kwa uangalifu. (Yakobo 1:23-25) Kwa mfano, unapofikiria kanuni tatu za Biblia zinazofuata, jiulize, ‘Je, maneno na utu wangu unapatana na kanuni hizi?’

“Jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu, lakini neno linaloumiza hufanya hasira ipande.” (Methali 15:1) Je, wewe huzungumza kwa njia ya upole na yenye amani?

“Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu, bali neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.” (Waefeso 4:29) Je, maneno yako yanawajenga wale walio karibu na wewe?

“Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Wakolosai 4:6) Je, wewe hujitahidi, hata katika hali ngumu, kusema kwa neema na kwa njia inayowapendeza wengine?

Ukirekebisha kasoro unazoona kwenye kioo, unaonekana nadhifu mbele ya wengine na unajihisi vizuri. Utapata manufaa kama hayo ukiboresha usemi wako kwa kutumia kioo cha Neno la Mungu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Unaweza kusoma Biblia kwenye Tovuti ya www.watchtower.org.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Maneno yako yanaonyesha nini?—Luka 6:45.

● Unapaswa kuzungumza na wengine kwa njia gani?—Waefeso 4:29; Wakolosai 4:6.

● Unaweza kufanya mambo gani ili kuboresha usemi wako?—Zaburi 19:14; Wafilipi 4:8.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Maneno tunayosema huathiri sifa yetu na mahusiano yetu