Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanye Nini ili Niwavutie Watu Mara ya Kwanza?

Nifanye Nini ili Niwavutie Watu Mara ya Kwanza?

Vijana Huuliza

Nifanye Nini ili Niwavutie Watu Mara ya Kwanza?

“Mahojiano haya ya kazi yanaendelea vizuri sana! Nina uhakika kwamba “mwajiri” huyu wangu tayari amegundua kwamba nimetulia, kwani tangu niingie ofisini mwake nimekuwa nikimwita kwa jina lake la kwanza. Ninajua kwamba ataniajiri!”

“Kweli huyu ni yule kijana aliyetuma zile habari zenye kupendeza sana kumhusu? Siwezi kumwajiri! Sasa ikiwa anajiendesha hivi hata kabla hajapata kazi, namna gani baada ya kumwajiri?”

Tazama picha hii, halafu usome habari iliyo hapo juu. Unaweza kutambua makosa matatu ambayo kijana huyu anafanya anapotafuta kazi kwa mara ya kwanza?

1 ․․․․․

2 ․․․․․

3 ․․․․․

● Majibu yameonyeshwa hapa chini

1. Kijana huyo amevalia mavazi ambayo hayafai kwa mahojiano ya kazi. 2. Usemi wake haufai (kumwita mwajiri wake kwa jina la kwanza), unaonyesha ni kana kwamba wamezoeana sana. 3. Ishara zake za mwili zinaonyesha kwamba hana heshima.

WAZIA kwamba ni mara yako ya kwanza kula chakula fulani. Itakuchukua muda gani kuamua ikiwa kinakupendeza au la? Huenda ukahitaji tu kukionja na hivyo kuamua ikiwa utakila tena wakati mwingine—au hata ikiwa utamaliza kile unachokula.

Hali inayofanana na hiyo hutukia unapokutana na mtu kwa mara ya kwanza. Mara moja, unakuwa na maoni fulani kumhusu. Jambo unalopaswa kukumbuka ni kwamba wakati uleule, yeye pia anafanyiza maoni fulani kukuhusu.

Je, unatafuta kazi, rafiki, au mwenzi wa ndoa? Utafanikiwa ikiwa mara ya kwanza utatenda kwa njia yenye kuvutia. Tutazungumzia mambo matatu ambayo huenda ukahitaji kufanyia kazi ili uboreshe ustadi wako wa kushirikiana na watu na hivyo kuwavutia zaidi.

1. Sura Yako

Huenda usipendezwe na wazo hili, lakini ukweli wa mambo ni kwamba maoni ya watu kukuelekea kwa mara ya kwanza huenda yakategemea sura yako. Mara nyingi wazo la kuwavutia watu mara ya kwanza hupuuzwa. Msichana mmoja anayeitwa Clarissa * anasema, “Inaonekana kwamba siku hizi unapoenda kwenye mkahawa, hujui ikiwa watu watakuja wakiwa wamevalia mavazi rasmi au nguo za kulala!”

Kwa kweli unapaswa kuvalia mavazi yanayofaana na hali. Kwa mfano, hutavalia mavazi ya kuogelea unapoenda kutafuta kazi! Lakini namna gani ikiwa hujui ni mavazi gani yanayofaa? Siri ni kuwa na usawaziko. Ikiwa huna uhakika kuhusu mavazi unayopaswa kuvalia, afadhali uvalie kwa kiasi.

KUMBUKA! Mavazi na kujipamba kwako kunafunua utu wako, kama vile picha ya eksirei inavyoonyesha jinsi ulivyo kwa ndani.

“Ninapowaona watu kwenye tafrija wakiwa wamevalia mavazi ya ajabu, mimi huepuka kushirikiana nao. Ninachojua tu ni jinsi wanavyoonekana, na mavazi yao yanawafanya waonekane kuwa na utu usiovutia.”Diane.

Biblia inatuhimiza tuwe na “mavazi yenye mpangilio mzuri” ambayo yanaonyesha kwamba tuna “kiasi na utimamu wa akili.”—1 Timotheo 2:9.

Jiulize hivi: ‘Je, mavazi yangu yana mpangilio mzuri, au ni shaghala-baghala? Ikiwa ninatafuta kazi, rafiki, au mwenzi wa ndoa, je, mavazi yangu yanaonyesha kwamba sina “utimamu wa akili?”

Dokezo: Pata ushauri kutoka kwa mtu unayemheshimu kwa sababu yeye huvalia vizuri.

2. Usemi Wako

Usemi wako utaonyesha ikiwa wewe ni mtu mnyenyekevu au mwenye kiburi, ikiwa unafikika kwa urahisi au hujali hata kidogo. Kumbuka hayo hasa ikiwa ungependa kumvutia mtu wa jinsia tofauti unayekutana naye kwa mara ya kwanza. Msichana anayeitwa Valerie anasema, “Mimi huudhika sana ninapozungumza na mvulana lakini yeye anaongea sana kujihusu.” Anaongezea hivi, “Vijana wengine hukosa usawaziko na wanataka kujua kila kitu kukuhusu mara moja. Hilo humfanya msichana ajihisi akiwa amelemewa na kutaka kuacha mazungumzo hayo na kutoroka.”

KUMBUKA! Maneno yako yanaweza kuwasaidia watu kujua jinsi ulivyo kwa kweli—hivyo unapaswa kutumia maneno yako kwa njia itakayovutia zaidi!

“Ninapokutana na kijana, mimi huvutiwa ninapomwona akijiendesha kwa njia ya kawaida. Pindi hiyo ya kwanza ni muhimu sana. Ikiwa mvulana atalazimika kutafuta maneno ambayo yatanifurahisha tu, basi ni afadhali asiseme chochote.”Selena.

Biblia inasema hivi: “Utasema jambo lisilofaa ukizungumza sana—basi uwe na busara na ujihadhari unasema nini.”—Methali 10:19, Contemporary English Version.

Jiulize hivi: ‘Ninaweza kuonyesha usawaziko jinsi gani ili nisiongee kupita kiasi au kunyamaza kupita kiasi? Je, usemi wangu utawaumiza au kukwaza wengine?’

Dokezo: Chunguza kwa makini watu ambao wanaonekana kuwa na kipawa cha kuzungumza. Wao hutumia mbinu gani kuendeleza mazungumzo? Je, unaweza kuwaiga?

3. Matendo Yako

Kuna msemo unaosema, muungwana ni kitendo. Kwa mfano, ikiwa wewe ni mwenye tabia nzuri, matendo yako yataonyesha kwamba unawaheshimu wengine. Hilo ni jambo lingine unalopaswa kukumbuka unapotafuta mwenzi wa ndoa. Msichana mmoja anayeitwa Carrie anasema hivi: “Kufanyia watu mambo madogo-madogo, kama vile kuwafungulia mlango, huonyesha kwamba unawaheshimu. Si lazima ufanye mambo makubwa na yasiyo ya kawaida.”

KUMBUKA! Matendo yako ni kama ubao mkubwa wa matangazo unaoonyesha waziwazi sifa zako za ndani. (Methali 20:11) Matendo yako “yanasema” nini kukuhusu?

“Kwa maoni yangu, ni muhimu sana kuwa msikilizaji mzuri. Pia, utaonyesha kwamba una tabia nzuri kwa kumsikiliza mtu anapozungumza bila kumkatiza, isipokuwa iwe lazima kufanya hivyo.”Natalia.

Biblia inasema hivi: “Watendeeni wengine kama ambavyo mngetaka wawatendee ninyi.”—Luka 6:31, Neno—Biblia Takatifu.

Jiulize hivi: ‘Je, mimi ni mwenye tabia nzuri? Ninapendezwa kikweli na wengine? Ninategemeka? Mimi hufika kwa wakati?’

Dokezo: Mnapopanga kukutana na mtu, panga ufike angalau dakika kumi kabla ya wakati ili uwe na muda wa ziada kushughulikia mambo yasiyotazamiwa. Usiruhusu maoni ya kwanza ya watu kukuhusu yawe ni kwamba wewe ni mtu wa kuchelewa!

Tahadhari: Ili uvutie mara ya kwanza haimaanishi eti ufiche jinsi ulivyo, kwani kufanya hivyo ni udanganyifu. (Zaburi 26:4) Badala yake, amua ungependa watu wakutambue kwa sifa gani halafu ujaribu sana kuzikuza kutoka moyoni na kuzifanya zionekane kupitia matendo yako. (Wakolosai 3:9, 10) Unapofanya hivyo, kumbuka kwamba ni wewe tu unayeweza kujijengea jina. Ukikazia fikira sura yako, usemi wako, na matendo yako, utafaulu kuvutia zaidi mara ya kwanza na watu watakujua kwa sifa zako nzuri!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Ni vizuri kuchagua marafiki wako kwa hekima. Ninaweza kuona jinsi marafiki huathiri mtazamo wangu, kwa hiyo mimi hujaribu kutafuta wale ambao watanisaidia.”

“Kuanzisha urafiki na watu hakutegemei ikiwa una sura yenye kuvutia au pesa—mambo ambayo huwezi kudhibiti—bali kunategemea sifa zako. Hilo ni jambo unaloweza kudhibiti!”

[Picha]

Sier

Ashley

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

NJIA ZA KUWAVUTIA WATU . . .

● Tabasamu lenye kuvutia

● Salamu imara (lakini usimbane mtu mkono sana)

● Dumisha usafi

● Mtazame machoni kwa heshima

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]

USIPITE KIASI!

Zungumza LAKINI usitawale mazungumzo

Uliza maswali LAKINI usimchimbe mtu

Onyesha urafiki LAKINI usicheze-cheze kimapenzi

Jiamini LAKINI usijigambe

[Sanduku katika ukurasa wa 28]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Mlipokuwa na umri wangu, mlifanya nini ili kuwavutia watu mara ya kwanza?

․․․․․