Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Mawasiliano?—Sehemu ya 1

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Mawasiliano?—Sehemu ya 1

Vijana Huuliza

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Mawasiliano?​—Sehemu ya 1

“Nina marafiki wanaoishi katika nchi nyingine, na njia bora ya kuwasiliana nao ni kutumia vituo vya mawasiliano. Ninafurahia kuzungumza nao hata ingawa wanaishi mbali sana.”—Sue, 17. *

“Ninafikiri kutumia vituo vya mawasiliano ni kupoteza wakati, ni njia ambayo wavivu hutumia kuwasiliana. Kuwasiliana uso kwa uso ndiyo njia pekee ya kudumisha urafiki.”—Gregory, 19.

MAONI yako yanakaribiana na maoni gani yaliyoonyeshwa hapo juu? Vyovyote vile, jambo moja ni hakika: Vituo vya mawasiliano vinatumiwa na watu wengi sana. * Fikiria hili: Ilichukua miaka 38 kwa watu milioni 50 kuanza kutumia redio, miaka 13 kwa idadi hiyohiyo ya watu kuanza kutumia televisheni, na miaka 4 kwa idadi hiyohiyo kuanza kutumia Intaneti. Lakini, hivi karibuni, katika muda wa miezi 12 tu, kituo cha mawasiliano kinachoitwa Facebook kimepata watumiaji milioni 200!

Tia alama kuonyesha kama ni kweli au si kweli chini ya sentensi ifuatayo:

Idadi kubwa ya watu wanaotumia vituo vya mawasiliano wana umri wa kati ya miaka 13 hadi 19. ․․․․․ Kweli ․․․․․ Si kweli

Jibu: Si kweli. Karibu asilimia 66 ya watu wanaotumia kituo maarufu zaidi cha mawasiliano wana umri wa miaka 25 au zaidi. Katika mwaka wa 2009 idadi kubwa zaidi ya watu walioanza kutumia kituo hicho walikuwa na umri wa zaidi ya miaka 55!

Hata hivyo, mamilioni ya vijana hutumia vituo vya mawasiliano, na kwa baadhi yao hiyo imekuwa ndiyo njia wanayopendelea zaidi kuwasiliana. “Nilifunga akaunti yangu,” anasema msichana mmoja anayeitwa Jessica, “lakini nikaifungua tena kwa sababu hakuna mtu aliyekuwa akiwasiliana nami kupitia simu. Ni kana kwamba watu wanakusahau iwapo hutumii kituo cha mawasiliano!”

Kwa nini watu wengi wanavutiwa na vituo vya mawasiliano? Jibu ni rahisi: Wanadamu wana tamaa ya kiasili ya kuwasiliana na wanadamu wenzao. Na hilo ndilo kusudi kuu la kituo cha mawasiliano. Fikiria sababu zinazoweza kuwachochea wengi wajiandikishe katika vituo hivyo.

1. Ni rahisi.

“Inaweza kuwa vigumu kuwasiliana na marafiki, lakini wote wanapokuwa katika tovuti moja, ni rahisi sana.”—Leah, 20.

“Ninapopachika habari fulani kwenye akaunti yangu ni kana kwamba nimewasiliana na kila mmoja wa rafiki zangu wakati uleule.”—Kristine, 20.

2. Kushinikizwa na marafiki.

“Kila wakati ninaombwa na watu niwe katika orodha yao ya marafiki, lakini sijafungua akaunti, kwa hiyo, ninashindwa kufanya hivyo.”—Natalie, 22.

“Ninapowaambia watu kwamba nimeamua kutofungua akaunti, wananipa jicho kana kwamba wanauliza, ‘Wewe una shida gani?’”—Eve, 18.

3. Kushinikizwa na vyombo vya habari.

“Kuna wazo linaloendelezwa katika vyombo vya habari kwamba usipokuwa katika mtandao wa watu wanaotumia vifaa vya mawasiliano, hutakuwa na marafiki. Na usipokuwa na marafiki ni kana kwamba huna maisha. Kwa hiyo, ikiwa hutumii vituo vya mawasiliano, wewe ni bure.”—Katrina, 18.

4. Shule.

“Walimu wangu wanatumia vituo vya mawasiliano. Wengine hutuma ujumbe kutueleza wakati ambapo tutakuwa na mtihani. Au kwa mfano, katika somo la hesabu, iwapo sijaelewa jambo, ninaweza kutuma ujumbe kwenye Ukuta wa akaunti ya mwalimu wangu na atanisaidia kufanya hesabu hiyo kwenye Intaneti.”—Marina, 17.

5. Kazi.

“Watu wanaotafuta kazi hutumia kituo cha mawasiliano ili kuzungumza na wengine. Nyakati nyingine kufanya hivyo huwasaidia wapate kazi.”—Amy, 20.

“Mimi hutumia kituo cha mawasiliano kufanya kazi yangu. Kinawawezesha wateja kuona kazi ninazoshughulikia za michoro ya kompyuta.”—David, 21.

Je, wewe unapaswa kufungua akaunti katika kituo cha mawasiliano? Ikiwa unaishi nyumbani, wazazi wako ndio wanaopaswa kuamua jambo hilo. * (Methali 6:20) Ikiwa wazazi wako hawataki ujiandikishe, unapaswa kutii.—Waefeso 6:1.

Kwa upande ule mwingine, wazazi fulani huwaruhusu watoto wao waliokomaa watumie kituo cha mawasiliano—nao husimamia jinsi wanavyokitumia. Ikiwa wazazi wako wanafanya hivyo, je, wanaingilia faragha yako? La hasha! Kituo cha mawasiliano ni kifaa muhimu na hatari vilevile, na wazazi wako wana haki ya kuchunguza jinsi unavyokitumia. Ukweli wa mambo ni kwamba kituo cha mawasiliano—kama tu matumizi mengine yoyote ya Intaneti—kina hatari zake. Ikiwa wazazi wako wanakuruhusu ufungue akaunti katika kituo cha mawasiliano, unaweza kuepuka hatari hizo jinsi gani?

Uwe Mwangalifu

Kwa njia fulani, kutumia Intaneti kunaweza kulinganishwa na kuendesha gari. Bila shaka umejionea kwamba si watu wote walio na leseni ambao huendesha gari kwa uangalifu. Kwa kweli, watu wengi wamepatwa na aksidenti mbaya kwa sababu ya kutokuwa waangalifu au kupuuza mambo.

Ni hali moja na watu wanaotumia Intaneti. Wengine huitumia kwa busara; wengine ovyoovyo. Ikiwa wazazi wako wamekuruhusu uwe na akaunti katika kituo cha mawasiliano, wanatumaini kwamba utaitumia kwa njia nzuri. Kwa hiyo, wewe ni dereva wa aina gani? Je, umeonyesha kwamba ‘unalinda hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri’?—Methali 3:21.

Katika habari hii tutazungumzia mambo mawili kuhusu vituo vya mawasiliano ambayo yanastahili kufikiriwa kwa uzito—faragha yako na wakati wako. Habari ya “Vijana Huuliza” katika toleo linalofuata la Amkeni! itazungumzia sifa yako na marafiki wako.

FARAGHA YAKO

Huenda usifikirie kwamba unahitaji kulinda faragha yako unapotumia kituo cha mawasiliano. Kwa kweli, kusudi kuu la kufungua akaunti ni kuwafikia watu. Hata hivyo, usipokuwa mwangalifu utapatwa na madhara.

Kwa mfano, tuseme kwamba una pesa nyingi. Je, utawaonyesha watu wote unapotembea na marafiki wako barabarani? Kufanya hivyo kungekuwa upumbavu—ni kana kwamba ungekuwa unamwomba mtu fulani aje aziibe! Ukiwa na hekima, utaficha pesa zako mahali ambapo hazionekani.

Linganisha habari zako za kibinafsi na pesa. Ukiwa na hilo akilini, angalia orodha iliyo hapa chini na utie alama kwenye mambo ambayo hungetaka yajulikane na mtu usiyemjua.

․․․․․ mahali ninapoishi

․․․․․ anwani yangu ya barua-pepe

․․․․․ shule ninayosomea

․․․․․ wakati ambapo niko nyumbani

․․․․․ wakati ambapo hakuna mtu nyumbani

․․․․․ picha zangu

․․․․․ maoni yangu

․․․․․ mapendezi yangu

Hata ikiwa wewe ndiye mtu mwenye urafiki zaidi ulimwenguni, bila shaka utakubali kwamba kuna mambo fulani katika orodha iliyo hapo juu ambayo hayapaswi kufunuliwa kwa watu wote. Lakini vijana wengi—na hata watu wazima—wamewaambia watu wasiowafahamu kabisa habari kama hizo! Unaweza kuepuka hatari kama hiyo jinsi gani?

Wazazi wako wakikuruhusu utumie kituo cha mawasiliano, unahitaji kufahamu kabisa mbinu ambazo kituo hicho hutumia kuweka siri—na uzitumie. Usidhani eti kituo hicho kitalinda faragha yako kwa niaba yako. Ukweli ni kwamba kituo hicho kimepanga mambo kwa njia ya kwamba watu wengi zaidi wanaweza kuona na kutoa maelezo kwenye ukurasa wako kuliko unavyofikiri. Hiyo ni sababu moja iliyomfanya msichana anayeitwa Allison afiche habari zake kwa njia ambayo ni marafiki wake tu wa karibu wangeweza kuona anachofanya kwenye kituo hicho. “Baadhi ya marafiki wangu walikuwa na marafiki ambao sikuwajua,” anasema, “nami sikutaka watu hao nisiowajua wasome mambo kunihusu.”

Hata ikiwa unawasiliana na marafiki wako wa karibu tu, bado unahitaji kuwa mwangalifu. “Unaweza kunaswa na tamaa ya kupokea maelezo kutoka kwa marafiki wako,” anasema Corrine mwenye umri wa miaka 21, “na hivyo uanze kuonyesha habari nyingi zaidi za kibinafsi kuliko unavyopaswa kufanya.”

Sikuzote unapaswa kukumbuka kwamba Intaneti haina siri kabisa. Kwa nini? “Tovuti kubwa huweka nakala za habari zake,” anasema Gwenn Schurgin O’Keeffe katika kitabu chake CyberSafe, na anaongezea hivi: “Kwa kweli, mambo tunayopachika kwenye Intaneti hayapotei. Lazima tukumbuke kwamba habari zote ni za kudumu kwa kuwa kuna nakala mahali fulani; kufikiria kwa njia tofauti ni upumbavu.”

WAKATI WAKO

Si faragha yako tu bali pia wakati wako unaweza kulinganishwa na pesa nyingi. Kwa sababu hiyo, unahitaji kupanga jinsi utakavyotumia wakati wako. (Mhubiri 3:1) Na hilo ni moja kati ya mambo magumu zaidi kuhusiana na matumizi ya Intaneti, kutia ndani matumizi ya vituo vya mawasiliano. *

“Mara nyingi sana nimejiambia, ‘Nitaitumia kwa dakika moja tu.’ Lakini saa moja baadaye, bado ninajikuta nikitumia kituo hicho.”—Amanda, 18.

“Nilikuwa mraibu. Kila mara niliporudi nyumbani kutoka shuleni, ningetumia saa nyingi kuchunguza kile ambacho watu walikuwa wakisema kuhusu mambo niliyopachika na kuchunguza walichopachika vilevile.”—Cara, 16.

“Ningeweza kutumia tovuti hiyo kwenye simu yangu, kwa hiyo ningeifungua nilipokuwa nikielekea shuleni, nilipokuwa shuleni, na nilipokuwa nikitoka shuleni. Kisha nilipofika nyumbani, niliitumia kwenye kompyuta. Nilijua kwamba mimi ni mraibu, lakini sikutaka kuacha!”—Rianne, 17.

Ikiwa wazazi wako wamekuruhusu utumie kituo cha mawasiliano, fikiria utakitumia kwa wakati mwingi kadiri gani kila siku. Kisha ujichunguze. Kwa mwezi mmoja, chunguza unatumia muda mwingi kadiri gani kwenye kituo cha mawasiliano na uone ikiwa unafuata mipaka uliyojiwekea. Kumbuka kwamba wakati wako ni kama pesa zako. Kwa hiyo, usiache kituo cha mawasiliano “kikufilisi.” Isitoshe, kuna mambo muhimu zaidi maishani!—Waefeso 5:15, 16; Wafilipi 1:10.

Vijana fulani wamechukua hatua za kuhakikisha kwamba wanadhibiti wakati wao. Kwa mfano, fikiria mambo yafuatayo:

“Nilifunga akaunti yangu, na nikapata wakati mwingi zaidi. Nilijihisi nikiwa huru zaidi! Hivi karibuni, nilifungua tena akaunti yangu, lakini ninajidhibiti kabisa. Nyakati nyingine siitumii kwa siku nyingi. Mara kwa mara mimi hata husahau kuihusu. Ikiwa akaunti hiyo itaniletea matatizo tena, nitaifunga tu.”—Allison, 19.

“Mara kwa mara nimechukua ‘likizo ya kutotumia vituo vya mawasiliano,’ na nikafunga akaunti yangu kwa miezi kadhaa kisha nikaifungua tena. Ninafanya hivyo kila mara ninapotambua kwamba nimekuwa nikiitumia kwa muda mwingi sana. Sasa sijihisi nikiwa nimenaswa nayo sana kama hapo awali. Mimi huitumia kwa kusudi fulani, kisha ninaachana nayo.”—Anne, 22.

Jambo Muhimu

Kuna jambo lingine kuhusu vituo vya mawasiliano ambalo unapaswa kufikiria. Ili kukusaidia uelewe jambo hilo, tia alama ya ✔ kando ya jibu unaloona ni sahihi.

Kituo cha mawasiliano hasa ni . . .

(A) ․․․․․ biashara.

(B) ․․․․․ klabu cha kujumuika.

(C) ․․․․․ aina ya burudani.

Jibu sahihi ni nini? Amini usiamini ni A. Kwanza kabisa, kituo cha mawasiliano ni biashara. Kusudi lake kuu ni kupata faida, hasa kupitia matangazo ya kibiashara. Na kwa watangazaji wa kibiashara, thamani ya kituo cha mawasiliano huongezeka kadiri watu wengi zaidi wanavyojiandikisha na kadiri vitu ambavyo watu hao wanapachika vinavyosambazwa. Kwa kweli, kadiri wewe au mtu yeyote anavyotumia wakati mwingi zaidi katika kituo cha mawasiliano, ndivyo matangazo mengi zaidi yatakavyotazamwa.

Kutambua jambo hilo kunakusaidia kutambua kwamba kituo cha mawasiliano hakipotezi chochote—na watangazaji wa kibiashara wanafaidika sana—unapowasambazia watu wengi sana habari au unapotumia muda mwingi sana kwenye Intaneti. Kwa vyovyote basi, ikiwa unatumia kituo cha mawasiliano, linda faragha yako na uwe mwangalifu kuhusu muda unaotumia katika kituo hicho.

KATIKA HABARI INAYOFUATA YA “VIJANA HUULIZA” . . .

Vituo vya mawasiliano vinaweza kuathiri sifa yako na marafiki wako. Soma uone.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 5 Kituo cha mawasiliano ni Tovuti inayowawezesha watu waliojiandikisha waweze kuwasiliana na kikundi cha marafiki waliochagua.

^ fu. 24 Amkeni! haipendekezi wala haishutumu tovuti yoyote ya mawasiliano. Wakristo wanapaswa kuhakikisha kwamba matumizi yao ya Intaneti hayavunji kanuni zozote za Biblia.—1 Timotheo 1:5, 19.

^ fu. 47 Kwa habari zaidi, ona “Vijana Huuliza . . . Je, Mimi Ni Mraibu wa Vifaa vya Elektroniki?” katika Amkeni! la Januari 2011. Chunguza hasa sanduku kwenye ukurasa wa 26, “Nilikuwa Mraibu wa Vituo vya Mawasiliano.”

[Blabu katika ukurasa wa 25]

Ilichukua miaka 38 kwa watu milioni 50 kuanza kutumia redio

[Blabu katika ukurasa wa 25]

Katika mwaka 1 tu hivi karibuni, kituo cha mawasiliano kinachoitwa Facebook kilipata zaidi ya watumiaji milioni 200!

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Zungumza pamoja na wazazi wako kuhusu jinsi ya kutunza siri unapotumia Intaneti. Ni mambo gani unayopaswa kuweka yakiwa siri na kwa nini? Ni habari gani inayoweza kuwa hatari ukiipachika katika sehemu yoyote ya Intaneti? Pia, waombe wazazi wako mashauri ya jinsi unavyoweza kuwa na usawaziko wa kuwasiliana na watu kupitia Intaneti na uso kwa uso. Wanapendekeza ufanye mabadiliko gani?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Huenda mambo unayofanya kwenye kituo cha mawasiliano yasiwe siri kama unavyofikiri

[Picha katika ukurasa wa 27]

Wakati ni kama pesa. Ukiutumia wote mahali pamoja, hutakuwa na wa kutosha unapouhitaji