Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Utafanya Maamuzi Yenye Hekima?

Je, Utafanya Maamuzi Yenye Hekima?

Je, Utafanya Maamuzi Yenye Hekima?

“Muziki ambao wazazi wangu wanasikiliza unachosha sana,” analalamika Jordan, mwenye umri wa miaka 17. *

“Muziki ambao mwanangu husikiliza umejaa maneno yenye hasira na mambo yenye kushtua,” anasema Denise, mama yake.

KWA nini wazazi huzozana na vijana wao kuhusu muziki? Jambo moja ni kwamba mapendezi ya mtu yanaweza kubadilika kadiri anavyokua. Sababu nyingine ni kwamba muziki hubadilika. Hivyo, muziki ambao ni maarufu leo, huenda kesho ukawa umepitwa na wakati.

Vyovyote vile, muziki hutuathiri kwa njia fulani. Je, umewahi kutambua jinsi ambavyo muziki huathiri hisia zako? Mfalme Sauli wa Israeli la kale aliposumbuliwa na hisia, muziki taratibu ulimtuliza. (1 Samweli 16:23) Kwa njia fulani, muziki unaweza kufananishwa na watu tunaoshirikiana nao. Muziki fulani hutufanya tuwe na hisia nzuri, kama vile furaha na upendo. Lakini mwingine hutuchochea tuwe na hasira na hata chuki.—Methali 13:20.

Kwa kuwa muziki una uvutano wenye nguvu jinsi hiyo, wazazi na watoto wanapaswa kuwa wenye hekima wanapochagua muziki watakaosikiliza. Ikiwa wewe ni mzazi, je, unapendezwa kikweli kujua vijana wako anasikiliza muziki wa aina gani na kwa muda gani? Je, unaweka viwango vya kufuatwa?

Hilo halimaanishi tu kupiga marufuku albamu fulani au muziki wa aina fulani. Bali unapaswa kuwasaidia vijana wako kuchagua muziki wa aina nyingine. Kitabu On Becoming Teenwise kinasema hivi: “Huwezi tu kumnyang’anya mtu kitu fulani anachopenda na kuthamini sana na kuacha pengo. Lazima awe na kitu kingine cha badala, kitu kipya kitakachochukua nafasi ya kile kilichoondolewa, la sivyo atarudia tabia zake za hapo awali.”

Jambo lingine la kutiliwa maanani ni hili: Watoto wako hutumia muda mwingi kiasi gani kusikiliza muziki? Je, wanatumia muda ambao wanapaswa kutumia kufanya mambo mengine ya maana zaidi, kama vile kazi ya shule, mambo ya kiroho, au majukumu mengine ya nyumbani? Kama vile tu Biblia inavyosema, “kuna wakati uliowekwa wa kila kitu.”—Mhubiri 3:1.

Huenda tatizo lingine likawa kujitenga. Ni kweli kwamba sisi sote tunahitaji kuwa na wakati wa faragha na hivyo tunapaswa kutenga wakati ili tuwe na pindi za kutafakari kwa undani mambo muhimu maishani. (Zaburi 1:2, 3) Hata hivyo, mtu anapotumia wakati mwingi akiwa amejitenga na wengine, huenda awe na mwelekeo wa kujifikiria sana na kuwa na ubinafsi. (Methali 18:1) Felipe, ambaye sasa ana umri wa miaka 20, anasema kwamba wakati aliotumia kusikiliza muziki ulikuwa ‘wakati muhimu wa kuwa peke yake.’ “Lakini,” anasema, “mama yangu alikuwa na wasiwasi kwamba ninajitenga na watu.”

Ni nini kitakachowasaidia vijana kama vile Felipe na wazazi wao waepuke kuzozana kuhusu muziki? Ni kwa njia gani sisi sote tunaweza kuchagua muziki kwa hekima? Wengi wamepata msaada kwa kutumia kanuni za Biblia. Hebu chunguza maswali matatu yafuatayo pamoja na watoto wako.

Muziki huu unapitisha ujumbe gani? “Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa visitajwe hata kidogo katikati yenu.” (Waefeso 5:3) Nyimbo nyingi huwa na maneno safi. Lakini nyingine, kwa njia iliyo wazi au iliyofichika, hukubaliana au hata kuchochea mwenendo unaovunja kanuni za maadili, kama zile zinazopatikana katika Biblia. Kwa kweli, miziki ya aina fulani inajulikana kwa upotovu wa maadili, chuki, na jeuri. Mwandikaji, Karen Sternheimer, anasema kwamba “nyakati nyingine maneno yanayotumika katika muziki wa rapu huwa yenye kushtua sana, yenye ukatili, yenye matusi, na yamejaa chuki dhidi ya wanawake.” Mara nyingi maneno ya muziki wa heavy-metal hutia ndani jeuri na uchawi. Hata miziki mingi yenye midundo ya kisasa inaweza kuwachochea wasikilizaji wawe na mwenendo usiofaa. Kwa hiyo, unapochagua muziki utakaosikiliza, unapaswa kutumia ‘nguvu zako za kufikiri’ ili ufanye uamuzi wa hekima. (Waroma 12:1) Usichague muziki kwa sababu ni maarufu tu au kwa kuwa una mdundo mtamu.

Muziki unaathiri hisia zangu jinsi gani? “Linda moyo wako . . . kwa maana ndiko zinakotoka chemchemi za uzima.” (Methali 4:23) Muziki unaochagua unaonyesha wewe ni mtu wa aina gani. Unaweza kuathiri akili na moyo wako. Jordan aliyenukuliwa hapo awali anasema hivi: “Baada ya kusikiliza aina fulani ya muziki nilihisi nikiwa mwenye hasira na jeuri.” Jiulize hivi: ‘Muziki ninaosikiliza unaathiri jinsi gani mawazo na hisia zangu? Je, baada ya kuusikiliza, mimi huwa nimeburudishwa au ninajihisi nikiwa na wasiwasi na nimekasirika? Je, unachochea mawazo machafu?’ (Wakolosai 3:5) Ikiwa muziki fulani unakufanya uwe na hisia zisizofaa au mawazo machafu, ni jambo la hekima kuuharibu. (Mathayo 5:28, 29) Hannah, mwenye umri wa miaka 17, anasema, “Nimeona madhara yanayotokea mtu anaposikiliza muziki mbaya, nami sitaki kuusikiliza hata kidogo.”

Je, muziki utaathiri viwango vyangu? “Chukieni yaliyo mabaya, pendeni yaliyo mema,” linasema Amosi 5:15. Siku hizi ni vigumu kufuata shauri hilo, kwa sababu kama vile tu unabii wa Biblia unavyosema, watu ni “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, . . . wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” (2 Timotheo 3:1-4) Kwa sababu hiyo, mstari wa 5 unasema: “Nawe geukia mbali kutoka kwa hao.”

Unaweza jinsi gani kugeukia mbali kutoka kwa watu kama hao? Ni wazi kwamba unahitaji kufanya mengi zaidi ya kuwaepuka. Ni lazima pia uepuke muziki na vitu vingine vinavyohusiana na njia zao zisizo za kimungu. (Waefeso 4:25, 29, 31) Lakini je, kufanya hivyo kunamaanisha usisikilize muziki wowote? La hasha!

Panua Mapendezi Yako

Katika familia nyingi, wazazi na watoto hufurahia kusikiliza na kubadilishana rekodi za muziki. Lena anasema hivi: “Binti yangu mwenye umri wa miaka 13 aliniomba nisikilize muziki anaopenda sana, na sasa mimi ninafurahia kusikiliza muziki wake.” Heather, mwenye umri wa miaka 16, hufurahia kusikiliza muziki ambao wazazi wake husikiliza, nao hubadilishana CD kwa ukawaida.

Ulimwenguni pote, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wa umri wote na wa tamaduni zote hufurahia aina tofauti za muziki, kutia ndani muziki wenye kujenga kiroho unaopatikana katika kitabu cha nyimbo kinachoitwa Mwimbieni Yehova. * Hata hivyo, huenda muziki huo ukawa na mtindo tofauti na ule ambao watu wamezoea katika tamaduni nyingi.

Iwe wewe ni mzazi au kijana, unapotaka kununua albamu ya muziki au kupakua muziki kutoka kwenye Intaneti, jiulize maswali yafuatayo: ‘Ni nani aliyenipa uwezo wa kufurahia muziki? Je, si Muumba wangu, Yehova Mungu? Ninaweza kumwonyesha jinsi gani kwamba ninathamini zawadi zake? Je, si kwa kuthamini sana viwango vyake kuhusu mema na mabaya au kutofautisha kati ya jambo lenye hekima na lisilo na hekima?’ Kufikiria maswali kama hayo kutakusaidia kufanya maamuzi yenye hekima unapochagua muziki, na hivyo kukuletea shangwe moyoni, na kuufanya moyo wa Muumba wako ushangilie.—Methali 27:11.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 17 Unaweza kupakua kutoka kwa Tovuti ya www.pr418.com.

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Miziki ya aina fulani inajulikana kwa upotovu wa maadili

[Blabu katika ukurasa wa 8]

Kuna aina nyingi ya muziki ambao unaweza kufurahia

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Sababu Iliyonichochea Kufanya Mabadiliko

“Sikumbuki mengi kuhusu miaka yangu ya ujana kwa kuwa nilikuwa nikitumia sana kileo, dawa za kulevya, na nilikuwa mjeuri,” anasema Ashley, mwenye umri wa miaka 24, “na muziki wa rapu na heavy metal ndio ulionichochea kufanya mambo hayo. Muziki uliojaa matusi, chuki, na pia midundo yake mizito ilinifanya nijihisi nikiwa shujaa. Muziki huo ulinifanya nishirikiane na marafiki waliokuwa wakitumia dawa za kulevya. Wasanii wa muziki wa rapu na heavy-metal ndio tuliowavulia kofia na kuwaona kuwa vielelezo vyetu.

“Hata hivyo, muda mfupi baadaye, maisha yangu yaliharibika zaidi. Nilipokuwa na umri wa miaka 17, nilikuwa karibu kufa kwa kutumia dawa za kulevya kupita kiasi. Niliporudiwa na fahamu, nilimwomba Mungu anisaidie. Nilikumbuka kwamba wakati fulani kijana mmoja aliniambia kuwa jina la Mungu ni Yehova, na hivyo nikatambua kuwa Mashahidi wa Yehova huwafundisha watu kumhusu. Kwa hiyo, nilitafuta namba ya simu ya Mashahidi wa Yehova kwenye kitabu cha simu, nikawapigia, na nikaanza kujifunza Biblia pamoja nao.

“Niliacha mazoea mabaya na nikatupa muziki wangu. Lakini, nilipotupa CD hizo kwenye pipa, nilisimama hapo nikizitazama kwa muda. Nilitambua kuwa haikuwa rahisi kufanya uamuzi huo. Hivyo, nilijikumbusha kwamba muziki huo, pamoja na mwenendo wangu, ulikuwa ukiniharibia maisha. Basi niligeuka na kwenda.

“Ingawa miaka kadhaa imepita, bado mimi huvutiwa na muziki wa rapu na heavy metal. Hivyo, mimi huuepuka kana kwamba ninaepuka dawa za kulevya. Leo, mimi hufurahia kusikiliza muziki wa aina nyingine, ikiwa ni pamoja na nyimbo taratibu, muziki taratibu wa roki, pamoja na baadhi ya muziki wa kale. Lakini jambo muhimu ni kwamba sasa ninaweza kuchagua muziki unaofaa.”

[Sanduku katika ukurasa wa 9]

Mapendekezo ya Kuwasaidia Wazazi

Je, una wasiwasi kuhusu muziki ambao kijana wako anasikiliza? Unaweza kumsaidia jinsi gani bila kuanzisha ubishi? Hebu chunguza mapendekezo yafuatayo:

Pata habari Kabla ya kuzungumza, ni vizuri kupata habari kamili. Kwanza sikiliza muziki, elewa maneno yake, na uchunguze jalada la rekodi hiyo. Jiulize hivi, ‘Nina sababu nzuri ya kuwa na wasiwasi, au ni kwamba ninafuatilia mambo madogo-madogo tu?’ Biblia inasema hivi: “Watu wenye akili wanafikiri kabla ya kusema; hivyo yale wanayosema yanakuwa yenye kushawishi zaidi.”—Methali 16:23, Today’s English Version.

Uwe na utambuzi Muziki unaweza kukusaidia kujua yale ambayo mtoto wako anafanya, anayofikiria, na jinsi anavyohisi. Mwulize kwa upole kuhusu hisia zake. Mwulize: “Kwa nini muziki huu unakuvutia? Je, unaonyesha kwa njia fulani jinsi unavyohisi?” Kisha sikiliza kwa makini anapojibu. Methali 20:5 inasema: “Fikira za mtu zimefichika kama kilindi cha maji; lakini mtu mwenye busara ajua kuzichota humo.”—Biblia Habari Njema.

Uwe mwenye kujenga Lengo lako si kumfanya kijana atupe CD fulani tu. Bali ungependa kuzoeza ‘nguvu zake za ufahamu . . . kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia’ ili aweze kujifanyia maamuzi ya hekima. (Waebrania 5:14) Kwa hiyo, mfundishe mtoto wako sasa ili aweze kujitegemea hata katika maisha yake ya baadaye: Mfundishe jinsi ya kufanya utafiti na kufikiri akitumia kanuni za Biblia. Kwa njia hiyo, utamsaidia akuze nguvu zake za ufahamu na hekima ya kimungu, mambo ambayo ni yenye thamani sana kuliko dhahabu yote ulimwenguni!—Methali 2:10-14; 3:13, 14.

Uwe imara, mwenye huruma, na fadhili “Jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu.” (Wakolosai 3:12) Unapozungumza na kijana wako, usiwe mbishi wala usishikilie sana maoni yako. Kumbuka kwamba wakati mmoja hata wewe ulikuwa kijana.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Dumisha viwango vya juu unapochagua muziki