Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mimi Sijafa”

“Mimi Sijafa”

“Mimi Sijafa”

“Msisimame kwenye kaburi langu na kulia,

mimi simo humo.

Mimi sijafa.”

● Unajua shairi hilo? Umewahi kusikia watu wakilikariri? Katika miaka michache iliyopita, shairi hilo limewafariji watu wengi ulimwenguni pote. Haijulikani kwa uhakika ni nani aliyetunga shairi hilo ingawa washairi tofauti-tofauti wametajwa kuwa ndio watungaji. Wengine wamedai kuwa shairi hilo ni sala ya mazishi ya Wanavajo. Katika Kiingereza, shairi hilo linajulikana, si kwa mstari wake wa kumalizia uliotajwa kwenye kichwa, bali kwa mstari wake wa ufunguzi: “Msisimame kwenye kaburi langu na kulia.”

Miaka michache iliyopita, shairi hilo lilikuwa wimbo maarufu sana nchini Japani, lakini pia liliwafanya watu wengi wachanganyikiwe. Wajapani huenda kwenye makaburi ya watu wa ukoo mara kwa mara ili kufanya desturi fulani kwa kuwa wanaamini bado watu hao wako hai. Kwa kuwa wimbo huo unafundisha jambo tofauti kabisa na imani yao, wengi wameuliza, “Wafu wako wapi?”

Tangu zamani Wabudha wa Japani wamefanya maziko, makesha, na ibada za ukumbusho. Lakini Wabudha wengi hawana jibu la swali hili, Wafu wako wapi? Na pia hawawezi kujibu maswali mengine, kama vile: Je, watu wa dini nyingine au taifa lingine wanapokufa wanaenda mahali palepale? Kwa nini wafu hawawezi kuongea?

Wengi wanahisi kwamba maswali kama hayo hayawezi kujibiwa na ni kupoteza tu wakati kujaribu kutafuta majibu yake. Huenda bado ukajiuliza, ‘Ni nini hutupata tunapokufa?’ Tunaweza kupata wapi majibu ya maswali hayo? Biblia inasema kwamba Mungu aliumba wanadamu wawili wa kwanza wakiwa wakamilifu na akawapa bustani nzuri iwe makao yao. Walikuwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso duniani iwapo wangemtii Mungu. Lakini hawakufanya hivyo.

Kwa hiyo, Mungu akachukua hatua. Aliwafukuza wenzi hao wawili kutoka kwenye makao yao yaliyokuwa Paradiso na akaacha kutegemeza uhai wao. Alieleza matokeo mabaya ya kutokutii kwao aliposema: “Kwa maana wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” Mwanadamu aliumbwa kutoka mavumbini, na mwishowe—anapokufa—yeye hurudi mavumbini.—Mwanzo 2:7; 3:19.

Mwanamume mmoja huko Kofu, Japani, anayetunza kaburi kubwa alisema: “Vyombo vya kuwekea majivu ya maiti huwa vimejaa jivu na mifupa ninapoviingiza kaburini. Baada ya miaka mitano hivi huwa vimepungua na kufikia nusu. Baada ya miaka kumi, vyombo vingi huwa vitupu kabisa.” Miili yetu imefanyizwa kwa madini ya udongo, na kadiri wakati unavyopita, madini hayo hurudi kuwa mavumbi tena. Kwa hiyo, ni nini kinachobaki?

Ingawa fahamu hupotea mtu anapokufa, Muumba wetu, ambaye anajua hata shore mmoja anapokufa, anatukumbuka kwa upendo. (Mathayo 10:29-31) Kama alivyoahidi, atatufufua, ndiyo, ataturudisha kuwa hai tena. Atatuita kutoka katika usingizi wa kifo.—Ayubu 14:13-15; Yohana 11:21-23, 38-44.

Ikiwa ungependa kujua mengi kuhusiana na habari hii, waandikie wachapishaji wa gazeti hili, ambao watafurahi kukueleza zaidi, au tembelea Tovuti yetu ya www.watchtower.org.