Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni ya Wazazi

Maoni ya Wazazi

Maoni ya Wazazi

Ikiwa wewe ni mzazi wa mtoto ambaye hajaanza kwenda shule, huenda ukawa na kibarua kigumu. Kwa mfano, utakabiliana jinsi gani na milipuko ya hasira ya mtoto? Unaweza kutumia njia gani kumfundisha mtoto wako ajue jema na baya na umrekebishe kwa njia yenye usawaziko? Ona jinsi wazazi fulani walivyokabiliana na changamoto hizo.

MILIPUKO YA HASIRA

“Katika miaka miwili ya kwanza, mtoto hutarajia apewe anachotaka. Mtoto wetu alikuwa na tatizo hilo. Kama asingepewa alichotaka, angerusha vitu. Kwa kuwa alikuwa mtoto wetu wa kwanza, hatukujua jinsi ya kushughulika na milipuko ya hasira. Hata wazazi wenzetu walipotuambia kwamba jambo hilo ni la kawaida kwa watoto walio na umri huo, hatukufarijika kwa njia yoyote.” —Susan, Kenya.

“Alipokuwa na umri wa miaka miwili, binti yetu angelala kwenye sakafu, apige kelele, alie, na kurusharusha miguu yake hewani . . . Jambo hilo lilikuwa linaudhi kama nini! Ilikuwa kazi ya bure kujaribu kuongea naye wakati kama huo. Kwa hiyo, mimi na mume wangu tungempeleka chumbani mwake na kumwambia kwa upole kwamba atakapoacha kulia, anaweza kutoka, kisha tuzungumze kuhusu jambo hilo. Alipotulia, mmoja wetu angeingia chumbani mwake na kumsaidia atambue kwamba tabia yake si nzuri. Mbinu hiyo ilifanikiwa. Hata wakati mmoja tulimsikia akimwomba Yehova msamaha. Kadiri wakati ulivyopita, milipuko yake ilipungua na hatimaye ikaisha kabisa.”—Yolanda, Hispania.

“Watoto wachanga hujaribu sana kupima ikiwa wanaweza kufanya mambo fulani bila kuadhibiwa. Mtoto huchanganyikiwa anapoachwa tu afanye jambo alilokatazwa. Tuligundua kwamba tulipokuwa imara, bila kubadili sheria, watoto wetu walijifunza hatua kwa hatua kwamba kupiga kelele hakungewasaidia kupata wanachotaka.”—Neil, Uingereza.

NIDHAMU

“Mtoto anapokuwa chini ya umri wa miaka mitano, ni vigumu sana kujua ikiwa anakusikiliza. Ni jambo la maana sana kurudia-rudia mambo unayomwambia. Yarudie mara nyingi kadiri unavyoweza, ukitumia ishara na sauti thabiti.”—Serge, Ufaransa.

“Hata ingawa tuliwalea katika mazingira yaleyale, kila mmoja wa watoto wetu wanne alikuwa tofauti kabisa. Binti mmoja angelia mara tu alipotambua ametuudhi; mwingine angejaribu kutupima aone ikiwa tungemwacha afanye mambo fulani bila kumwadhibu. Nyakati nyingine, ingetosha tu kumtazama mtoto kwa ukali au kumkemea, ilhali nyakati nyingine ingebidi kutoa adhabu hususa.”—Nathan, Kanada.

“Ni muhimu sana kwamba usilegeze msimamo wako. Lakini wakati huohuo, mzazi hapaswi kushikilia sana maoni yake au kuwa mkali. Nyakati nyingine, mtoto anapoonyesha kwa kweli anasikitikia kosa alilofanya, tunahisi kwamba ni vyema kuwa na usawaziko na kupunguza adhabu tutakayompa.”—Matthieu, Ufaransa.

“Mimi hujitahidi sana nisiweke sheria nyingi mno, lakini zile chache ambazo tayari zipo hazibadiliki. Mwanangu mwenye umri wa miaka mitatu anajua matokeo ya kutotii, na hilo humsaidia ajiendeshe kwa njia inayofaa. Ninapokuwa nimechoka, ni rahisi sana kupuuza makosa anayofanya. Lakini ili asione kwamba sheria zinaweza kubadilika, mimi hujilazimisha kuchukua hatua. Kuhakikisha kwamba sheria hazibadiliki-badiliki ni muhimu sana!”—Natalie, Kanada.

KUTOBADILI SHERIA

“Watoto wadogo wana kumbukumbu nzuri sana, kwa hiyo wanakumbuka vizuri sana mzazi anapobadili sheria.”—Milton, Bolivia.

“Wakati mwingine, mwana wangu anauliza jambo moja akitumia njia tofauti ili aone kama tutatoa jibu lilelile. Nikisema jambo moja na mama yake aseme jambo tofauti, anatambua haraka tofauti hiyo na kujaribu kupata anachotaka.”—Ángel, Hispania.

“Nikiwa na furaha mimi hupuuza tabia mbaya ya mwana wangu, lakini nikiwa nimekasirika mimi humwadhibu kwa hasira. Niligundua kwamba jambo hilo lilifanya azidi kuwa na tabia mbaya.”—Gyeong-ok, Korea.

“Ni muhimu watoto wadogo waelewe kwamba ikiwa tabia fulani ni mbaya leo, daima itabaki kuwa hivyo.”—Antonio, Brazili.

“Wazazi wakibadili-badili sheria, mtoto atajiambia kwamba Baba na Mama hawana msimamo, na kwamba wao hufanya maamuzi kwa kutegemea hisia zao. Lakini wazazi wakiwa na msimamo, watoto watajua jambo baya haliwezi kugeuka kuwa zuri. Hiyo ni njia moja ambayo wazazi wanaweza kuwalinda na kuwaonyesha watoto wao upendo.”—Gilmar, Brazili.

“Watoto wanaweza kutumia vibaya nafasi ambazo mzazi hawezi kuepuka kufanya jambo aliloombwa na mtoto wake—kama vile kunapokuwa na watu wengine. Kama jibu langu ni hapana, mimi husema hivyo tangu mwanzo, nami humwambia mwana wangu wazi kwamba sitamsikiliza hata akiendelea kunibembeleza.”—Chang-seok, Korea.

“Lazima wazazi wakubaliane. Ikiwa mimi na mke wangu hatukubaliani kuhusu jambo fulani, tunalizungumzia faraghani. Watoto wanaweza kujua ikiwa maoni ya wazazi yanatofautiana, na watatumia vibaya nafasi hiyo.”—Jesús, Hispania.

“Mtoto akijua kwamba wazazi wana umoja na hawawezi kubadili msimamo hata wanapobembelezwa, anajihisi akiwa salama. Anajua anachotarajia kutoka kwa wazazi, iwapo atatii au la.”—Damaris, Ujerumani.

“Mimi na mke wangu huamini kwamba tunapomwahidi binti yetu kwamba tutampa kitu fulani kizuri hatupaswi kubadili ahadi yetu. Hivyo anajifunza kutumainia ahadi zetu.” —Hendrick, Ujerumani.

“Iwapo kila wakati mwajiri wangu angebadili mambo anayotazamia nifanye kazini, ningeudhika. Ndivyo ilivyo pia kwa watoto. Wanajihisi salama wanapojua sheria na wanapojua kwamba sheria hizo hazitabadilika. Wanapaswa pia kuelewa vizuri adhabu ya kuvunja sheria hizo, na kwamba adhabu yenyewe haibadiliki.”—Glenn, Kanada.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

“Acheni Ndiyo yenu imaanishe Ndiyo, na Siyo yenu, Siyo.”—Yakobo 5:12

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

MASIMULIZI YA FAMILIA

Mimba Ambayo Haikutarajiwa​—Jinsi Tulivyobadili Maisha Yetu

Limesimuliwa na Tom na Yoonhee Han

Tom: Tulikuwa tumeoana kwa miezi sita tu wakati ambapo mke wangu, Yoonhee, aligundua kwamba yeye ni mja-mzito. Kwa nje, nilijifanya kuwa mtulivu ili nimhakikishie Yoonhee kwamba anaweza kunitegemea ili apate faraja na utegemezo. Lakini kwa kweli nilikuwa na hofu moyoni!

Yoonhee: Nililemewa na hisia—na nilijawa na woga! Nililia tena na tena; sikujihisi nikiwa tayari kuwa mama.

Tom: Hata mimi sikujihisi nikiwa tayari kuwa baba! Lakini baada ya kuongea na wazazi wengine, tulitambua kwamba watu wengi hupata mimba bila kutarajia. Tulifaidika pia kusikia kuhusu shangwe ambazo wazazi wengine hupata. Pole kwa pole, wasiwasi wangu ulibadilika na nikaanza kutazamia kuwa na mtoto.

Yoonhee: Amanda alipozaliwa, tulianza kukabili changamoto za aina nyingine. Alilia bila kukoma, nami sikuweza kulala kwa majuma kadhaa. Nilikosa hamu ya kula, na nilijihisi mchovu kupita kiasi. Mwanzoni, nilijaribu kujitenga na watu. Lakini nikatambua kwamba kujitenga kwa kukaa nyumbani hakutanisaidia. Kwa hiyo, nikaanza kuchangamana na akina mama wengine. Kufanya hivyo kulinisaidia kubadilishana mawazo nao, na nikatambua kwamba si mimi peke yangu niliyekuwa na matatizo hayo.

Tom: Nilijitahidi kudumisha ratiba nzuri katika familia. Kwa mfano, tukiwa Mashahidi wa Yehova, mimi na Yoohnee tuliazimia kuwa wa kawaida katika kazi ya kuhubiri na mikutanoni. Pia, mtu hupata gharama nyingine kwa sababu ya kuwa na mtoto mchanga, na nyingine huja bila kutarajiwa. Tulijitahidi kuishi kulingana na mapato yetu ili tusijiingize katika madeni, ambayo yangetuletea mfadhaiko zaidi.

Yoonhee: Mwanzoni, nilifikiri kwamba hatuwezi kwenda kuhubiri, kwa kuwa watoto wanaweza kuwa wasumbufu sana. Lakini ukweli ni kwamba watu wengi hupenda sana watoto wachanga. Kutambua jambo hilo kulinisaidia kuendelea kuhubiri na kuwa na maoni yanayofaa kumhusu mtoto wangu.

Tom: Biblia inasema kwamba watoto “ni urithi kutoka kwa Yehova” na “ni thawabu.” (Zaburi 127:3) Maneno hayo yananionyesha kwamba mtoto ni zawadi yenye thamani sana. Kama ilivyo na urithi mwingine wowote ule, unaweza kuamua utautumia kwa njia gani: Ama uuhifadhi vizuri ama uupoteze. Ninajifunza kwamba kila hatua katika ukuzi wa mtoto ni ya pekee, na ninahitaji kujionea kila hatua katika maisha ya binti yangu kwa sababu inapopita, haiwezi kurudiwa.

Yoonhee: Nyakati nyingine, mambo tusiyoyatarajia hutukia katika maisha yetu, na kupata mtoto bila kutazamia si jambo baya. Sasa Amanda ana umri wa miaka sita, na sioni kama ninaweza kuishi bila yeye.

[Picha]

Tom na Yoonhee wakiwa na binti yao, Amanda