Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kubalehe—Kujitayarisha Kuwa Mtu Mzima

Kubalehe—Kujitayarisha Kuwa Mtu Mzima

Kubalehe​—Kujitayarisha Kuwa Mtu Mzima

HEBU wazia kwamba umesafiri kutoka kwenye eneo lenye joto hadi kwenye eneo lenye baridi kali. Baada tu ya kushuka ndege, unatambua kwamba hilo ni eneo lenye theluji nyingi. Je, unaweza kuzoea hali hizo? Ndiyo, lakini itakubidi ufanye mabadiliko fulani.

Unapatwa na hali kama hiyo watoto wako wanapobalehe. Huenda ikaonekana kwamba watoto wako wanabadilika mara moja. Yule mvulana ambaye aliambatana nawe kokote ulikoenda, sasa anataka kuchangamana tu na vijana wenzake. Yule msichana ambaye alitamani sana kukueleza jinsi siku yake ilivyokuwa, sasa anakujibu kwa maneno machache tu.

“Habari ya shule?” unamwuliza.

“Nzuri,” anajibu.

Halafu kimya.

“Unafikiria nini?” unamwuliza.

“Hakuna,” anajibu.

Halafu kimya tena.

Kwani ni nini kimetukia? Muda mfupi uliopita, “inaonekana ni kana kwamba ulikuwa na ruhusa ya kujua mambo ya siri katika maisha ya watoto wako,” kinasema kitabu Breaking the Code. Kinaendelea kusema kwamba ni kana kwamba hakuambii mambo mengi na huenda hata akawaambia wengine mambo ambayo hawezi kukuambia. Huenda ukahisi ni kana kwamba unamtazama kijana wako akikua na huwezi kumsaidia.

Je, hilo linamaanisha kwamba haiwezekani kuwa na uhusiano wa karibu na watoto wako wanapobalehe? La hasha! Unaweza kuwa karibu na watoto wako wanapobalehe. Hata hivyo, kwanza, unahitaji kuelewa ni nini hasa kinachoendelea katika kipindi hicho cha ukuzi chenye kusisimua na vilevile kilicho na matatizo.

Wanaacha Kuwa Watoto na Kuwa Watu Wazima

Wakati fulani uliopita, watafiti walifikiri kwamba ubongo wa mtoto huwa umekomaa kabisa kufikia wakati anapokuwa na umri wa miaka mitano. Sasa wanaamini kwamba ingawa ukubwa wa ubongo hubadilika kidogo sana baada ya umri huo, hilo ni tofauti kabisa kuhusu kazi unaofanya. Vijana wanapoanza kubalehe, homoni zilizo ndani ya miili yao huanza kubadili jinsi wanavyofikiri. Kwa mfano, watoto wadogo hawachanganui mambo, wanayaona jinsi yalivyo tu, lakini vijana wanaobalehe huchanganua mambo kwa undani zaidi. (1 Wakorintho 13:11) Wao huanza kuwa na msimamo wao na hawaoni haya kujieleza.

Paolo, anayeishi nchini Italia aliona kwamba kijana wake alikuwa akipitia mabadiliko hayo. “Ninapomtazama mwanangu,” anasema, “ninahisi kana kwamba yeye ni mwanamume mdogo na si mvulana tena. Si kwa sababu ya mabadiliko ya mwili wake. Kile kinachonishangaza zaidi ni jinsi anavyofikiri. Haogopi kueleza maoni yake na kuyatetea!”

Je, umeona mabadiliko hayo katika kijana wako anayebalehe? Huenda alipokuwa mtoto, alifuata tu maagizo aliyopewa. Alihitaji tu kuambiwa, “Kwa sababu nimesema hivyo.” Sasa, kwa kuwa anabalehe, anataka kujua sababu za kufanya mambo, na hata wakati mwingine angependa kujua kwa nini kuna sheria fulani nyumbani. Huenda nyakati nyingine ikaonekana kwamba anaasi kwa sababu ya jinsi anavyotoa maoni yake.

Hata hivyo, usikate kauli kwamba kijana wako anataka kukiuka sheria ulizoweka. Huenda akawa anajitahidi kuishi kulingana na viwango ulivyomwekea, anajaribu tu kuona jinsi vitakavyofaa katika maisha yake. Hebu wazia unahamia nyumba nyingine pamoja na vitu vyako. Je, itakuwa rahisi kupata nafasi ya kuweka kila kitu katika nyumba yako mpya? Huenda isiwe rahisi. Hata hivyo, ukweli ni kwamba hutatupa kitu chochote unachoona kuwa ni cha thamani.

Kijana wako yuko katika hali kama hiyo anapojitayarishia wakati ambapo “atamwacha baba yake na mama yake.” (Mwanzo 2:24) Ni kweli, huenda wakati huo uko mbali sana; kijana wako bado si mtu mzima. Lakini sasa ni kana kwamba anapakia mizigo yake ili ahame. Akiwa tineja, anajichunguzia viwango ambavyo amelelewa navyo, na anaamua ni viwango gani atahama navyo atakapokuwa mtu mzima. *

Huenda ukaogopa unapofikiri kwamba mtoto wako anafanya maamuzi kama hayo. Lakini unaweza kuwa na hakika kwamba atakapokuwa mtu mzima, atafuata tu viwango ambavyo yeye anaona kuwa ni vyenye thamani. Kwa hiyo, sasa—wakati ambapo kijana wako bado yuko nyumbani—ndio wakati anapaswa kuchunguza kwa undani viwango atakavyofuata maishani.—Matendo 17:11.

Kwa kweli, kijana wako atafaidika sana kwa kufanya hivyo. Ikiwa sasa atakubali viwango vyako bila kujichunguzia, huenda baadaye akakubali viwango vya wengine bila kufikiri. (Kutoka 23:2) Biblia inaeleza kwamba kijana kama huyo hushawishika kwa urahisi kwa sababu “amepungukiwa moyoni”—maneno yanayomaanisha kwamba anakosa utambuzi, pamoja na sifa nyingine muhimu. (Methali 7:7) Kijana ambaye hana uhakika wa mambo anayoamini anaweza ‘kurushwa huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho kupitia udanganyifu wa watu.’—Waefeso 4:14.

Unaweza kufanya nini ili kijana wako asipatwe na hali kama hiyo? Hakikisha kwamba ana mambo haya matatu muhimu:

1 NGUVU ZA UFAHAMU

Mtume Paulo aliandika kwamba ‘nguvu za ufahamu za watu wakomavu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Waebrania 5:14) Huenda ukasema, ‘Lakini nilimfundisha mtoto wangu yaliyo sawa na yaliyo makosa miaka mingi iliyopita.’ Ni kweli, na bila shaka elimu hiyo ilimfaidi wakati huo na kumtayarisha kwa ajili ya kipindi kilichofuata cha ukuzi maishani mwake. (2 Timotheo 3:14) Hata hivyo, Paulo alisema kwamba nguvu za ufahamu zinahitaji kuzoezwa. Ingawa watoto wadogo wanaweza kupata ujuzi kuhusu yaliyo sawa na yaliyo makosa, matineja wanahitaji kuwa “watu wazima katika nguvu za uelewaji.” (1 Wakorintho 14:20; Methali 1:4; 2:11) Hungependa kijana wako atii tu bila kufikiri, bali atumie uwezo wake wa kufikiri. (Waroma 12:1, 2) Unaweza kumsaidia afanye hivyo jinsi gani?

Njia moja ya kufanya hivyo ni kumruhusu ajieleze. Usimkatize anapozungumza, na usimwonyeshe kwamba umekasirika kupita kiasi, hivi kwamba aache kuzungumza—hata anaposema jambo la kushtua. Biblia inasema hivi: ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19; Methali 18:13) Zaidi ya hilo, Yesu alisema hivi: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mathayo 12:34) Ikiwa utamsikiliza, utaweza kujua mambo ambayo kwa kweli yanamhangaisha kijana wako.

Unapoongea, jaribu kumwuliza maswali badala ya kumwambia mambo moja kwa moja. Nyakati nyingine Yesu aliuliza, “Mnaonaje?” ili kuwasaidia watu wajieleze waziwazi na kwa unyoofu, si wanafunzi wake tu, bali hata wale waliokuwa wakaidi. (Mathayo 21:23, 28) Unaweza kufanya hivyo unaposhughulika na kijana wako anayebalehe, hata anapotoa maoni yanayotofautiana na yako. Kwa mfano:

Kijana wako anaposema: “Sidhani ninaamini kwamba kuna Mungu.”

Badala ya kumjibu: “Si tulikufundisha kwamba kuna Mungu—lazima uamini kwamba Mungu yuko!”

Unaweza kusema: “Kwa nini unasema hivyo?”

Kwa nini unapaswa kumtia moyo kijana wako ajieleze? Kwa sababu hata ingawa unasikia anachosema, unahitaji kujua yale anayofikiri. (Methali 20:5) Huenda akawa na tatizo na viwango vya Mungu si eti haamini kuna Mungu.

Kwa mfano, huenda kijana ambaye anashawishiwa kuvunja sheria za Mungu za maadili akaamua kutoamini kwamba kuna Mungu ili iwe rahisi kuzivunja. (Zaburi 14:1) Huenda akajiambia, ‘Ikiwa hakuna Mungu, basi si lazima niishi kulingana na viwango vya Biblia.’

Ikiwa kijana wako ana maoni kama hayo, msaidie afikirie swali hili, Je, kweli ninaamini kwamba viwango vya Mungu vina faida kwangu? (Isaya 48:17, 18) Ikiwa anaamini kwamba vinaweza kumfaidi, basi mtie moyo atambue kwamba anapaswa kufanya kila awezalo kudumisha hali yake nzuri.—Wagalatia 5:1.

Kijana wako anaposema: “Hii ni dini yako, si lazima iwe dini yangu.”

Badala ya kumjibu: “Hii ni dini yetu, wewe ni mtoto wetu, na ni lazima uamini yale tunayokufundisha.

Unaweza kusema: “Hayo kwa kweli ni maneno makali. Ikiwa hukubaliani na imani yangu, lazima uwe na imani nyingine tofauti. Kwa hiyo, unaamini nini? Unafikiri ni viwango gani bora vya kufuata maishani?”

Kwa nini unapaswa kumtia moyo kijana wako ajieleze? Kwa sababu unapotumia maswali kwa njia hiyo ili kuufikia moyo wake, utamsaidia achunguze maoni yake mwenyewe. Huenda akashangaa anapotambua kwamba imani yake ni sawa na yenu ila tu anahangaishwa na jambo lingine tofauti kabisa.

Kwa mfano, huenda kijana wako hajui jinsi ya kuwaeleza wengine mambo anayoamini. (Wakolosai 4:6; 1 Petro 3:15) Au huenda amevutiwa kimapenzi na mtu wa jinsia tofauti ambaye hana imani kama yake. Tafuta kiini cha tatizo, na umsaidie kijana wako kufanya hivyo pia. Kadiri anavyotumia nguvu zake za ufahamu, ndivyo atakavyojitayarisha vizuri zaidi kuwa mtu mzima.

2 MWONGOZO WA MTU MZIMA

Katika tamaduni fulani leo, hakuna “mahangaiko na mkazo” mwingi ambao wanasaikolojia fulani wanadai ungetarajiwa wakati wa ujana. Watafiti wamegundua kwamba katika maeneo kama hayo watoto wanakomaa wakiwa na umri mdogo. Wao hushirikiana na kufanya kazi na watu wazima, na hata kupewa majukumu ya watu wazima. Maneno kama vile “utamaduni wa vijana,” “vijana wasio na adabu,” na hata “kubalehe” hayatumiki katika maeneo hayo.

Tofauti na hilo, hebu wazia kuhusu vijana katika maeneo fulani ambao husoma katika shule zilizosongamana ambako wanashirikiana tu na vijana wenzao. Wanaporudi nyumbani, hawapati mtu. Baba na Mama wako kazini. Watu wa ukoo wanaishi mbali. Watu wanaoshirikiana nao kwa ukaribu mara nyingi ni vijana wenzao tu. * Je, unaona hatari iliyopo? Tatizo si kuwa tu ataanza kushirikiana na vijana watundu. Watafiti wanasema kwamba hata vijana wenye mwenendo mzuri hushawishiwa na kuingia kwenye mwenendo mbaya wasiposhirikiana na watu wazima.

Jamii moja ambayo haikuwatenga vijana kutoka kwa watu wazima ni ile ya Israeli la kale. * Kwa mfano, Biblia inaeleza kumhusu Uzia, aliyewekwa kuwa mfalme wa Yuda alipokuwa bado tineja. Ni nini kilichomsaidia Uzia kuutimiza mgawo huo mzito? Ni wazi kwamba ilikuwa kwa sababu ya uvutano wa mtu mzima aliyeitwa Zekaria, ambaye Biblia inasema ‘alikuwa akiwafundisha watu kumwogopa Mungu wa kweli.’—2 Mambo ya Nyakati 26:5.

Je, kijana wako ana mshauri mmoja au kadhaa walio na umri mkubwa na walio na viwango kama vyako? Usione wivu ikiwa kijana wako ana marafiki kama hao. Wanaweza kumsaidia kijana wako afanye lililo sawa. Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.”—Methali 13:20.

3 KUTEGEMEKA

Katika nchi fulani, sheria zinawazuia vijana wasifanye kazi ya kuajiriwa kwa zaidi ya saa fulani kila juma au wasifanye kazi za aina fulani. Vizuizi hivyo viliwekwa ili kuwalinda watoto kutokana na kazi hatari—viliwekwa wakati wa ule mvuvumko wa kiviwanda wa karne ya 18 na 19.

Ingawa sheria hizo zinawalinda vijana kutokana na hatari na kutumiwa vibaya, wataalamu fulani wanasema kwamba zinawazuia wasiwajibike. Kwa sababu hiyo, kinasema kitabu Escaping the Endless Adolescence, vijana wengi wamesitawisha “mtazamo wa kudai vitu kwa nguvu, eti wanastahili kila kitu wanachopata bila hata kufanya kazi yoyote.” Waandishi wa kitabu hicho wanasema kwamba inaonekana mtazamo huo “unatokana na ulimwengu unaopendelea hasa kuwatumbuiza vijana badala ya kutazamia wafanye jambo lolote.”

Tofauti na hilo, Biblia inaeleza kuhusu vijana ambao walichukua madaraka mazito walipokuwa wangali wachanga. Fikiria kisa cha Timotheo, ambaye huenda alikuwa tineja tu alipokutana na mtume Paulo—mtu mzima ambaye alikuwa na uvutano mkubwa juu yake. Wakati mmoja, Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Uichochee kama moto zawadi ya Mungu iliyo ndani yako.” (2 Timotheo 1:6) Huenda muda fulani kabla au baada ya kutimia miaka 20, Timotheo aliondoka nyumbani na kusafiri pamoja na mtume Paulo, akisaidia kuanzisha makutaniko na kuimarisha akina ndugu. Baada ya kufanya kazi pamoja na Timotheo kwa miaka kumi hivi, Paulo aliwaambia hivi Wakristo huko Filipi: “Sina mtu mwingine yeyote aliye na mwelekeo kama wake atakayejali kwa unyoofu mambo yenu.”—Wafilipi 2:20.

Mara nyingi, vijana wana hamu ya kuchukua madaraka, hasa wanapotambua kwamba watafanya kazi ya maana na inayowasaidia watu. Kufanya hivyo hakuwasaidii tu wawe watu wazima wenye kutegemeka katika maisha ya baadaye bali pia kunawasaidia kusitawisha sifa nzuri hata sasa.

Kuzoea Hali Mpya

Kama ilivyotajwa mwanzoni mwa habari hii, ikiwa wewe ni mzazi wa kijana anayebalehe, huenda ukahisi kwamba unakabili hali tofauti na ile uliyokabili miaka michache tu iliyopita. Uwe na hakika kwamba unaweza kubadilikana na hali hiyo, kama vile tu ulivyofanya katika hatua nyingine zote za ukuzi wake.

Ona miaka ya utineja ya mtoto wako kuwa nafasi ya (1) kumsaidia kukuza nguvu zake za ufahamu, (2) kumsaidia apate mwongozo wa mtu mzima, na (3) kumsaidia awe mwenye kutegemeka. Kwa kufanya hivyo, utakuwa ukimtayarisha kijana wako anayebalehe kwa ajili ya maisha ya utu uzima.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kitabu kimoja kinasema kwamba umri wa kubalehe ni “kipindi cha kujitayarisha kuwaaga wazazi.” Kwa habari zaidi, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 2009 (1/5/2009), ukurasa wa 10-12, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 38 Burudani ambazo zimekusudiwa hasa kwa ajili ya vijana huendeleza wazo la kwamba wanapaswa kushirikiana na vijana wenzao tu, kwa kuwa wana utamaduni ambao watu wazima hawawezi kuuelewa.

^ fu. 39 Maneno “kubalehe” na “tineja” hayapatikani katika Biblia. Ni wazi kwamba vijana waliokuwa miongoni mwa watu wa Mungu katika nyakati za kabla ya Ukristo na katika enzi za Ukristo walikomaa wakiwa na umri mdogo kuliko ilivyo katika jamii nyingi leo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 20]

“SIWEZI KUWAZIA KUWA NA WAZAZI BORA KULIKO HAWA”

Kwa maneno na matendo, wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova huwafundisha watoto wao kuishi kupatana na kanuni za Biblia. (Waefeso 6:4) Hata hivyo, hawawalazimishi kufanya hivyo. Wazazi ambao ni Mashahidi wanatambua kwamba kila mtoto, anapofikia umri wa kujiamulia, lazima aamue viwango atakavyofuata maishani.

Aislyn, mwenye umri wa miaka 18, ameamua kufuata viwango alivyofundishwa tangu utotoni. Anasema hivi: “Kwa maoni yangu, dini yangu si kitu cha kufuatwa siku moja tu kwa juma. Ni njia yangu ya maisha. Inahusisha kila kitu ninachofanya na kila uamuzi ninaofanya—iwe ni marafiki wangu, masomo nitakayochagua, na vitabu nitakavyosoma.”

Aislyn anathamini sana jinsi ambavyo wazazi wake Wakristo wamemlea. Anasema hivi: “Siwezi kuwazia kuwa na wazazi bora kuliko hawa, na ninafurahi kwamba wamenifundisha kuwa na tamaa ya kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova na kudumu nikiwa hivyo. Wazazi wangu wataendelea kuwa na uvutano mkubwa katika maisha yangu yote.”

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mruhusu kijana wako azungumze

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mshauri aliye na umri mkubwa anaweza kuwa na uvutano mzuri kwa mtoto wako

[Picha katika ukurasa wa 19]

Kazi yenye kuridhisha inawasaidia vijana kuwa watu wazima wenye kutegemeka