Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kudhibiti Hasira

Kudhibiti Hasira

Kudhibiti Hasira

ZAIDI ya miaka 2,000 iliyopita, Aristotle mwanafalsafa Mgiriki, alitumia neno “catharsis” kufafanua jinsi ya kutoa mkazo wa kihisia ambao mtu hupata anapotazama mchezo wa kuigiza wenye kuhuzunisha. Wazo lake lilikuwa kwamba baada ya mkazo kutoka, mtu hujihisi akiwa ametulia akili.

Mapema katika karne iliyopita, Sigmund Freud, mtaalamu wa mfumo wa neva kutoka Austria aliendeleza wazo hilo. Alidai kwamba ikiwa watu wangefungia hisia zisizofaa, baadaye zingejitokeza kama matatizo ya akili kama vile msisimko wa hisia mbalimbali. Kwa hiyo, Freud alidai kwamba unapaswa kuonyesha hasira badala ya kuizuia.

Katika miaka ya karibuni zaidi, watafiti waliochunguza dai hilo katika miaka ya 1970 na 1980, hawakupata chochote cha kuunga mkono nadharia hiyo. Matokeo ya utafiti wao yalimfanya mwanasaikolojia, Carol Tavris aandike hivi: “Tunapaswa kuacha kabisa kuunga mkono nadharia ya kwamba kuonyesha hasira kuna manufaa. Hakuna utafiti wowote ambao umewahi kuunga mkono wazo la kwamba kutenda kwa jeuri huondoa uhasama.”

Mwanasaikolojia mwingine, Gary Hankins, alisema: “Utafiti unaonyesha kwamba mara nyingi ‘kulipuka’ kwa hasira hukufanya ujihisi ukiwa na hasira zaidi, badala ya kuipunguza.” Ni kweli kwamba wataalamu wa akili hawajawahi kukubaliana na nadharia ya kwamba mtu anapaswa kuonyesha hasira. Hata hivyo, watu wengi wamenufaika kutokana na chanzo kingine cha hekima, yaani, Biblia.

“Acha Hasira”

Wazo la kudhibiti hasira linaonyeshwa vizuri na mtunga-zaburi za Biblia, Daudi, aliyesema hivi: “Acha hasira na uache ghadhabu; usijionyeshe umewaka hasira ili tu kufanya uovu.” (Zaburi 37:8) Ili uepuke kusema au kufanya jambo ambalo huenda ukajutia baadaye, ni vizuri kwanza uepuke ‘kuwaka hasira.’ Ingawa ni vigumu kufanya hivyo, unaweza kufaulu! Acheni tuzungumzie njia tatu ambazo unaweza kutumia ili kudhibiti hasira.

Punguza Kiwango cha Hasira

Ili upunguze hasira, tulia. Epuka kusema jambo la kwanza linalokuja akilini. Unapojihisi unapandwa na hasira na huenda ukashindwa kudhibiti hisia zako, fuata shauri hili la Biblia: “Mwanzo wa ugomvi ni kama mtu anayefungulia maji; kwa hiyo kabla mabishano hayajalipuka, jiondokee.”—Methali 17:14.

Shauri hilo lilimsaidia mwanamume anayeitwa Jack kudhibiti hasira yake yenye jeuri. Baba ya Jack alikuwa mlevi na mwenye hasira. Alipokuwa akikua, Jack alianza pia kuwa mjeuri. Anasema hivi: “Nilipokasirika, nilihisi ni kana kwamba ninawaka moto. Ningewafokea watu kwa hasira na kuwapiga ngumi.”

Hata hivyo, mambo yalianza kubadilika Jack alipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alikuja kuelewa kwamba kwa msaada wa Mungu, anaweza kubadilika na kujifunza kudhibiti hasira yake. Na alibadilika! Jack anaeleza yaliyotokea wakati mfanyakazi mwenzake alipomtusi kwa hasira: “Nilijihisi nikipandwa na hasira kali. Nilitaka kumshika na kumtupa chini.”

Ni nini kilichomsaidia Jack kuwa mtulivu? Anaeleza: “Nakumbuka nikisali hivi, ‘Tafadhali Yehova, nisaidie niwe mtulivu!’ Kisha, kwa mara ya kwanza maishani, nilijihisi nikiwa na amani na nikaweza kuondoka.” Jack aliendelea kujifunza Biblia. Alitumia wakati mwingi kusali na kutafakari maandiko kama Methali 26:20, linalosema: “Pasipo na kuni moto huzimika, na pasipo na mchongezi ugomvi hutulia.” Baadaye, Jack alifaulu kudhibiti hasira yake.

Jifunze Kutulia

“Moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.” (Methali 14:30) Kufuata ukweli huo wa msingi wa Biblia kunaweza kuboresha afya yako ya kihisia, kimwili, na kiroho. Anza kwa kujifunza mbinu rahisi za kutulia ambazo zitakusaidia kupunguza hasira. Mbinu zifuatazo zimekuwa na matokeo katika kukabiliana na hasira inayotokana na mkazo:

● Kupumua polepole ni njia bora tena ya haraka ya kupunguza hasira yako.

● Unapopumua polepole, jiambie neno au maneno yatakayokutuliza kama vile, “tulia” au “achana na jambo hilo” au “si jambo kubwa.”

● Jishughulishe na jambo unalopenda kufanya, kama vile kusoma, kusikiliza muziki, kutunza bustani, au utendaji mwingine unaokufanya utulie.

● Fanya mazoezi kwa ukawaida na ule vyakula vyenye lishe.

Badili Mtazamo Wako

Huenda usiweze kuepuka kabisa watu au mambo yanayokuchochea ukasirike, lakini unaweza kujifunza kudhibiti jinsi unavyotenda. Hilo linatia ndani kubadili jinsi unavyofikiri.

Watu wenye matarajio makubwa hushindwa kudhibiti hasira. Kwa nini? Kwa sababu mtu asipofikia au jambo fulani lisipofanywa kulingana na viwango vyake vya juu, anatamauka na kukasirika. Ili kushinda mtazamo huo wa kutazamia ukamilifu, ni vizuri kukumbuka kwamba “hakuna mwanadamu mwadilifu, hakuna hata mmoja . . . Watu wote wamepotoka.” (Waroma 3:10, 12) Kwa hiyo, tutatamauka ikiwa tutatarajia sisi wenyewe au wengine wawe wakamilifu.

Ni jambo la hekima kutotarajia mengi mno kutoka kwa watu wengine au kwetu wenyewe. Biblia inasema: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yakobo 3:2) Naam, “hakuna mwanadamu aliye mwadilifu duniani ambaye huendelea kufanya mema na asifanye dhambi.” (Mhubiri 7:20) Kwa hiyo tukidai kwamba sisi ni wakamilifu, maisha yetu yatajaa mambo yenye kutamausha na hasira.

Kwa kuwa sisi ni wanadamu wenye dhambi, tunakasirika mara kwa mara. Lakini sisi wenyewe ndio tutakaoamua jinsi tutakavyotenda tunapokasirika. Mtume Paulo aliwaonya hivi Wakristo wenzake: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka.” (Waefeso 4:26) Naam, tukidhibiti hasira yetu, tunaweza kuonyesha hisia zetu katika njia inayofaa ambayo itawanufaisha wengine.

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 89]

JIFUNZE KUTULIA

Jizoeze kupumua polepole

Jishughulishe na jambo unalopenda kufanya

Fanya mazoezi kwa ukawaida