Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilipenda Jeuri

Nilipenda Jeuri

Nilipenda Jeuri

Limesimuliwa na Salvador Garza

NILIPOKUWA mvulana, nilipenda jeuri na nilipigana na yeyote aliyenikasirisha. Bingwa fulani wa ndondi aliona hilo na akanifundisha mchezo wa kupigana ngumi. Punde si punde nilisafiri kotekote Marekani nikiwa mwanandondi wa kulipwa. Baadaye niliajiriwa kazi ya kuwa mlinzi wa jambazi mmoja.

Niliendelea kupenda jeuri hata baada ya kuoa na kupata watoto sita. Wakati huo nilimiliki klabu moja ya usiku. Ingawa watu kadhaa walijaribu kuniua, nilifurahia maisha hayo yenye msisimuko. Pindi moja niliwapiga risasi wanaume wawili tulipokuwa tukipigana na nikawajeruhi vibaya sana. Pia, mimi na rafiki zangu tulipanga njama ya kumteka nyara mwanasiasa mmoja mashuhuri. Lakini polisi waligundua njama hiyo na kunikamata. Polisi walipoenda kuwakamata rafiki zangu, walifyatuliana risasi na rafiki zangu wote wakauawa. Ninafurahi kwamba wakati huo nilikuwa gerezani!

Miaka mingi baadaye, niliachiliwa huru na nikapata kazi. Siku moja, nilipokuwa nikirudi nyumbani kutoka kazini, ghafula niliumwa sana na kichwa. Nilikuwa na wasiwasi mwingi hivi kwamba nilisali nipate msaada. Mke wangu, Dolores, ambaye alikuwa akijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, aliniambia kwamba Mungu ana jina, yaani Yehova. (Zaburi 83:18) Kwa hiyo nilisali nikitumia jina hilo.

Mara tu nilipopata nafuu, Dolores alinitia moyo nihudhurie mikutano ya Mashahidi wa Yehova katika Jumba lao la Ufalme. Niliguswa sana na jinsi Mashahidi walivyonionyesha fadhili na kunijali hivi kwamba nilitokwa na machozi. Jambo hilo lilifanya nianze kujifunza Biblia na mtazamo wangu kuhusu maisha ukaanza kubadilika. Nilifurahia sana mambo niliyokuwa nikifundishwa.

Hata hivyo, ilichukua muda mrefu kujifunza kudhibiti hasira yangu. Kwa mfano, siku moja mimi na rafiki yangu, Antonio, tulipokuwa tukihubiri nyumba kwa nyumba, tulikutana na mwanamume ambaye alitutukana. Nilikasirika sana karibu nimpige. Lakini Antonio akanizuia. Baadaye, kwa subira alinikumbusha jinsi ambavyo Yesu alivumilia dhihaka na matukano. Mtume Petro ambaye alikuwa mwandamani wa karibu wa Yesu, aliandika hivi: “Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa matukano.” (1 Petro 2:23) Maneno hayo yalinigusa sana.

Nikitafakari maendeleo ambayo nimefanya kadiri ambavyo miaka imepita, ninamshukuru Yehova kwa kunipa roho yake takatifu, ambayo hutusaidia kujizuia na kuwa watu wenye kufanya amani. (Wagalatia 5:​22, 23) Familia yangu ina furaha na tunaishi kwa utulivu na amani. Isitoshe, nikiwa mhudumu wa wakati wote, nina pendeleo la kuwasaidia watu kuwa na amani pamoja na Mungu.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kujifunza Biblia kulimsaidia Salvador kupata amani