Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nichague nani kuwa mfano wa kuiga?

Nichague nani kuwa mfano wa kuiga?

Vijana Huuliza

Nichague nani kuwa mfano wa kuiga?

Katika makala hii, utajifunza

KWA NINI unahitaji mifano mizuri ya kuiga?

Utawapata WAPI?

Utaiga mfano wao JINSI GANI?

KWA NINI UNAWAHITAJI?

UKWELI WA MAMBO: Ni kawaida kujitahidi kuwa kama watu unaopendezwa nao. Hilo linaweza kuwa jambo zuri​—au baya​—ikitegemea unapendezwa na nani hasa.

Unachohitaji: Watu wa kuiga walio na mfano mzuri.​—Wafilipi 3:17.

Tatizo: Watu wengi huwahusudu hasa watu mashuhuri, kama vile wanamuziki, mabingwa wa michezo, au waigizaji mashuhuri wa sinema​—hata kama wana sifa mbaya.

Jambo la kufikiria: Biblia inasema kwamba tabia zetu ni kama vazi. (Wakolosai 3:​9, 10) Ikiwa ungeenda kununua nguo, je, ungemruhusu muuzaji aliyevalia ovyoovyo akuchagulie nguo? Kwa nini basi umruhusu mtu mashuhuri mwenye sifa mbaya akuamulie jinsi utakavyojiendesha? Badala ya kufanya hivyo au kuufuata tu umati, kujichagulia watu ambao ni mifano mizuri kutakusaidia (1) uchague sifa unazotaka kukuza na (2) uwaige watu wenye sifa hizo nzuri.

UTAWAPATA WAPI

Tia alama ya kweli au si kweli.

1. Mfano wa kuigwa anapaswa kuwa mtu ambaye umewahi kukutana naye.

Kweli Si kweli

2. Mfano wa kuigwa anapaswa kuwa mkamilifu.

Kweli Si kweli

3. Unaweza kuwa na mifano mingi ya kuiga.

Kweli Si kweli

Majibu

1. Si kweli. Unaweza kuchagua watu walioishi zamani za kale wawe mifano ya kuiga. Mifano bora zaidi inaweza kupatikana katika Biblia. Kwa mfano, ukisoma sura ya 11 ya kitabu cha Biblia cha Waebrania, utaona kwamba Mtume Paulo anataja wanaume na wanawake 17 ambao walikuwa mifano mizuri katika imani. Jambo la maana hata zaidi ni kwamba, katika sura inayofuata, Paulo aliwasihi Wakristo ‘wamtazame kwa makini’ Yesu na wamwige. (Waebrania 12:2) Yesu ndiye mfano wetu bora zaidi wa kuiga.​—Yohana 13:15. *

2. Si kweli. Mbali na Yesu, Adamu hakuwa kuwa na wazao wowote wakamilifu. (Waroma 3:23) Hata nabii jasiri Eliya “alikuwa binadamu kama sisi.” (Yakobo 5:​17, Biblia Habari Njema) Ndivyo walivyokuwa pia wengine kama vile Miriamu, Daudi, Yona, Martha, na Petro. Biblia inafunua waziwazi makosa ambayo wanaume na wanawake hao walifanya. Hata hivyo, waliweka vielelezo vizuri katika mambo mengi maishani, na kwa hiyo wanaweza kuwa mifano mizuri ya kuigwa.

3. Kweli. Unaweza kuwa na mifano mingi ya kuiga kadiri unavyotaka. Mmoja anaweza kuwa mfano bora wa kuwa na bidii, mwingine kwa sababu ya kuwa mwenye subira. Huenda mwingine akawa kielelezo kizuri kwa sababu anadumisha mtazamo mzuri hata anapokabili matatizo. (1 Wakorintho 12:28; Waefeso 4:​11, 12) Tafuta sifa nzuri katika watu wengine, na utaona zile ambazo zinafaa kuigwa.​—Wafilipi 2:3.

UTAIGA MFANO WAO JINSI GANI?

1. Wachunguze wale uliochagua wawe mifano ya kuiga. Mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo wa karne ya kwanza: “Mutazame wao wanaotembea kwa kufuata mufano tuliowapa ninyi.”​— Wafilipi 3:​17, Zaire Swahili Bible.

2. Wafahamu. Ikiwezekana, tumia wakati pamoja na wale uliowachagua wawe mifano ya kuigwa. Biblia inasema hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.”​— Methali 13:20.

3. Onyesha sifa nzuri za wale uliochagua wawe mifano ya kuigwa. Waebrania 13:7 linasema: “Mnapotafakari jinsi mwisho wa mwenendo wao unavyokuwa, igeni imani yao.”

Je, uko tayari kuanza? Jaza sehemu ifuatayo.

Hatua za Kuchukua

Chagua sifa unayotaka kukuza. (Je, ungependa kuwa mwenye urafiki zaidi? mkarimu? mwenye bidii? mstahimilivu? mwenye kutegemeka? mwenye kutumainika?)

․․․․․

Chagua mtu anayeonyesha sifa ambayo ungependa kukuza. *

․․․․․

Unapochagua mtu fulani awe mfano wa kuigwa, lengo lako si kufanana naye. Bado wewe una sifa zako nzuri za kipekee. Hata hivyo, kuwa na mifano mizuri ya kuiga kutakusaidia kukuza sifa nzuri zaidi unapoendelea kuwa mtu mzima. Si hilo tu, lakini ukifuata mfano wao mzuri, wewe pia utakuwa mfano mzuri wa kuigwa na wengine.

Unaweza kupata makala zaidi za “Vijana Huuliza” katika Tovuti ya www.watchtower.org/ype

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Bila shaka, hata watu wanaoishi sasa wanaweza kuwa mifano mizuri ya kuigwa. Anaweza kuwa mzazi, ndugu au dada yetu, mshiriki wa kutaniko la Kikristo aliyekomaa, iwe unamjua au umesoma kumhusu.

^ fu. 32 Pia, unaweza kuanza na hatua hii ya mwisho ukipenda. Kwanza, chagua mtu unayependezwa naye. Halafu, jiulize hivi, ‘Ni sifa gani hususa inayomfanya mtu huyo avutie?’ Kisha, jitahidi kuiga sifa uliyochagua, kwa njia ambayo mtu huyo anaionyesha.

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Kwa nini umruhusu mtu mashuhuri mwenye sifa mbaya akuamulie jinsi utakavyojiendesha?

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 22, 23]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

Layla​—Rafiki yangu Sandra huwa na mtazamo unaofaa. Pia, anaifahamu Biblia yake vizuri. Kwa sababu hiyo, yeye anajua jinsi ambavyo anaweza kusuluhisha matatizo yake kwa njia rahisi sana. Ninaweza kumweleza tatizo lolote nililo nalo, liwe kubwa au dogo.

Terrence​—Rafiki zangu Kyle na David hawapuuzi kamwe hisia za wengine. Kila mara, wao huwa tayari kuwasaidia watu wenye matatizo, na wanaacha mahangaiko yao pembeni kwanza. Mimi huwaona kuwa mifano mizuri sana.

Emmaline​—Mimi humwona mama yangu kuwa mfano mzuri wa kuiga. Anaifahamu Biblia vizuri sana, na kila mara yeye hutafuta fursa ya kuwaeleza watu wengine kuhusu imani yake. Anaamini kabisa kwamba kuhubiri ni pendeleo, wala si kazi yenye kuchosha. Ninamheshimu kwa sababu hiyo!

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

SOMA ZAIDI KUHUSU HABARI HII!

Je, unatatizika kupata mifano mizuri ya kuiga? Soma Waebrania sura ya 11 na uchague mmoja wa wanaume au wanawake wanaotajwa hapo. Anza mradi wa kujifunza kumhusu mtu huyo ukiwa na lengo la kuiga sifa zake zinazokuvutia.

Unaweza kupata mifano mingi ya kuigwa iliyo katika Biblia kwenye Buku la 1 na la 2 la kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yanayofanya Kazi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Ona “Fahirisi ya Mifano ya Kuigwa” kwenye upande wa ndani wa jalada la nyuma la vitabu hivyo.

[Sanduku katika ukurasa wa 23]

MBONA USIWAULIZE WAZAZI WAKO?

Zungumza na wazazi wako kuhusu mifano mizuri ambayo wao waliiga wakati walipokuwa na umri kama wako na wanayoiga sasa. Wazazi wako wamefaidika jinsi gani kwa kuwa na mifano ya kuiga maishani?