Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maoni Ya Biblia

Je, Maisha Yako Yanaongozwa na Nyota?

Je, Maisha Yako Yanaongozwa na Nyota?

Je, ananipenda?

Nisafiri leo?

Nitapata kazi hiyo?

WATU wengi hugeukia unajimu ili kupata majibu ya maswali kama hayo yaliyotajwa hapo juu. * Lakini je, kweli nyota zinaweza kuongoza maisha yako? Je, zinaweza kukusaidia kujua wakati wako ujao, au kujua mambo yanayokuhusu? Biblia inasema nini?

Je, Nyota Zinaweza Kuamua Wakati Wetu Ujao?

Watu fulani wanaamini kwamba hatuwezi kuepuka yatakayotupata wakati ujao. Wanasema kwamba tayari wakati wetu ujao umeamuliwa mapema na nyota zinaweza kutufunulia hilo. Lakini Biblia inasema jambo tofauti na hilo. Inatuambia kwamba Mungu amewapa wanadamu uhuru wa kuchagua, kwa hiyo kwa kiasi fulani wanaweza kudhibiti mambo yatakayowapata. Kwa mfano, aliwaambia hivi Waisraeli: “Nimeweka uzima na kifo mbele yako, baraka na laana; nawe lazima uchague uzima ili uendelee kuwa hai, wewe na uzao wako.”—Kumbukumbu la Torati 30:19.

Kwa maneno hayo, Yehova Mungu alionyesha waziwazi kwamba kwa kiasi kikubwa watu wake wangeweza kuamua mambo yatakayowapata wakati ujao. Ikiwa wangetii amri zake, wangepata baraka. Ikiwa wangekosa kutii, wangejiletea matatizo.

Fikiria hili: Ikiwa wakati ujao wa kila Mwisraeli ungekuwa tayari umeamuliwa mapema na nyota, je, ingepatana na akili kwa Mungu kuwasihi wachague uzima? Je, kweli Mungu angekuwa akitenda kwa haki ikiwa angewaadhibu kwa matendo ambayo hawangeweza kudhibiti?

Biblia inatufundisha jambo hili waziwazi: Maisha yetu yanategemea maamuzi tunayofanya—hayaongozwi na nyota.—Wagalatia 6:7.

Je, Nyota Zinaweza Kuamua Utu Wetu?

Wanajimu wengi wanapuuza wazo la kwamba wakati wetu ujao umeamuliwa mapema. Mmoja wao anadai hivi: “Tunaweza kuamua jinsi wakati wetu ujao utakavyokuwa,” lakini anaongezea hivi: “Kwa upande mwingine, kipindi tulichozaliwa huamua utu wetu.” Watu wengi wana maoni kama hayo. Wanahisi kwamba kwa kuwa nyota, sayari, na nguvu nyingine za asili huathiri dunia yetu, kwa nini basi zisituathiri bila sisi kujua? Biblia inasema nini?

Biblia si kitabu cha kisayansi ambacho hueleza mambo yote kuhusu mwili wa mwanadamu na ulimwengu wote mzima. Hata hivyo, inaeleza kusudi la Yehova la kuumba jua, mwezi, na nyota. Andiko la Mwanzo 1:14, 15 linasema: “Mungu akasema, ‘Mianga na iweko angani, itenge mchana na usiku, ionyeshe nyakati, majira . . . na ing’ae angani na kuiangazia dunia.’”​—Biblia Habari Njema.

Fikiria hili: Ikiwa Mungu angekusudia nyota ziamue utu wetu, je, hangetuambia jambo hilo?

Tutafikia mkataa gani? Kwamba nyota ni sehemu ya kazi za uumbaji za Mungu na haziamui utu wetu.

Mahali Panapofaa Kupata Mwongozo

Ikiwa tunataka kujua kuhusu wakati wetu ujao au kujielewa, tunastahili pongezi. Lakini kuna mahali panapofaa pa kutafuta mwongozo badala ya kutazama nyota.

Biblia inasema kwamba Yehova Mungu ndiye “anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho.” (Isaya 46:10) Ana kusudi ambalo atatimiza. (Isaya 55:10, 11) Tunaweza kujifunza kuhusu kusudi la Mungu kwa kusoma Biblia. Kitabu hicho kitakatifu cha kale pia kinaeleza kwa nini tunateseka na jinsi ambavyo Mungu atakomesha hali zinazowakumba wanadamu. *​—2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1-4.

Biblia ndiyo mwongozo bora zaidi ikiwa mtu angetaka kujua utu wake na kuuboresha. Kwa nini? Kwa sababu tunapoisoma, inatusaidia tujichunguze wenyewe kwa unyoofu. Kwa mfano, Biblia inasema kwamba Yehova Mungu ni “mwenye rehema,” “si mwepesi wa hasira,” na yuko “tayari kusamehe.” (Kutoka 34:6; Zaburi 86:5) Je, sisi tuna sifa hizo? Biblia inaweza kufunua mawazo yetu yasiyofaa na kutusaidia tuone mambo tunayohitaji kurekebisha.

Kwa hiyo, hatuhitaji kutazama nyota ili kujua wakati wetu ujao na kujua utu wetu. Tunaweza kupata mwongozo unaofaa kutoka katika Biblia, ambayo ‘imeongozwa na roho ya Mungu nayo ni yenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.’​—2 Timotheo 3:16, 17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Unajimu ni elimu ya kuchunguza jua, mwezi, sayari, na nyota, mtu akiwa na imani ya kwamba vitu hivyo vinaweza kuathiri maisha yetu na vinaweza kutusaidia kujielewa.

^ fu. 19 Kwa habari zaidi kuhusu kusudi la Mungu, ona sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.