Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kamusi Iliyochukua Miaka 90 Kukamilishwa

Kamusi Iliyochukua Miaka 90 Kukamilishwa

MNAMO 1621 mvumbuzi Mwitaliano aligundua aina ya maandishi yasiyojulikana katika magofu ya jiji la kale la Uajemi la Persepoli. Katika miaka ya 1800, wachimbuaji wa vitu vya kale walipokuwa wakichimbua huko Iraki walipata maandishi kama hayo juu ya mabamba ya udongo na kwenye kuta za makasri. Maandishi hayo ni ya lugha za Mesopotamia zilizozungumzwa na watawala kama vile Sargoni wa Pili, Hammurabi, na Nebukadneza wa Pili. Maandishi hayo yalikuwa na umbo la kikabari, na yakaja kujulikana kama maandishi ya kikabari.

Aina hii ya uandishi ilikuwa muhimu ili kuelewa ustaarabu wa Mesopotamia ya kale. Kwa sababu hiyo, wasomi waliofanya kazi ya kupambanua hati hizo waliona uhitaji wa kuwa na kamusi yenye mambo mengi ya Kiakadi, lugha inayokaribia kufanana na lahaja za Waashuru na Wababiloni.

Kazi hiyo kubwa ilianza kufanywa na Taasisi ya Nchi za Mashariki ya Chuo Kikuu cha Chicago, Marekani mnamo 1921, na ilikamilishwa miaka 90 baadaye katika mwaka wa 2011. Walitokeza kamusi yenye sehemu 26 inayoitwa Assyrian Dictionary, iliyo na kurasa 9,700. Inashughulikia lugha na lahaja zilizotumiwa huko Iran, Iraki, Siria, na Uturuki, kuanzia milenia ya tatu K.W.K. hadi mwaka wa 100 W.K.

Kamusi ya Assyrian Dictionary ina zaidi ya kurasa 9,700!

Kwa nini kamusi hiyo ishughulikie mambo mengi hivyo? Kwa nini ilichukua muda mrefu hivyo kuikamilisha? Na ni nani ambao wangependezwa kuitumia?

Mambo Yanayopatikana Katika Kamusi Hiyo

“Kamusi hiyo si orodha ya maneno tu,” anaeleza Gil Stein, msimamizi wa Taasisi hiyo ya Chicago ya Nchi za Mashariki. Badala yake, “kwa kueleza waziwazi mahali ambapo kila neno lililotoka na jinsi kila neno lilivyotumiwa zamani, buku hilo la pekee ni ensaiklopedia ya utamaduni wa Mesopotamia inayokazia hasa mambo kuhusu historia, jamii, uandishi, sheria, na dini. Hicho ni kifaa muhimu sana cha utafiti kwa ajili ya msomi yeyote ambaye angependa kuchunguza maandishi yanayohusu ustaarabu wa Mesopotamia.”

Wahariri walitambua mapema sana kwamba “ili maana ya neno iweze kueleweka kwa ukamili, lazima wachunguze mara zote ambazo neno hilo lilionekana, na kwamba hawapaswi kukusanya maneno tu, bali wayakusanye maneno pamoja na maandishi yanayozunguka neno hilo ambayo yangesaidia kutambua maana ya neno hilo katika muktadha au matumizi hususa.” Kwa sababu hiyo, kamusi hiyo ikaja kuwa mkusanyo wa manukuu na sehemu za maandishi yaliyotafsiriwa za maandishi yale ya awali ya kikabari yaliyokuwa na maneno yanayofafanuliwa.

Mamilioni ya maandishi ya kikabari yamegunduliwa katika muda wa karne mbili zilizopita, na yanazungumza kuhusu habari nyingi sana tofauti-tofauti. Lugha ya kimataifa katika eneo lote la kale la Mashariki ya Kati ilikuwa lugha ya Waashuru na Wababiloni, au Kiakadi. Hata hivyo, watu katika eneo hilo walitokeza vitabu; wakafanya biashara; wakajifunza hisabati, elimu ya nyota, na kiini-macho; walitunga sheria; walitokeza nyanja za kitaaluma; na wakajihusisha katika dini. Kwa sababu hiyo, maandishi yao kuhusu mambo hayo na mengine yanatupa habari nyingi sana.

Maandishi hayo hayaonyeshi kwamba eneo hilo lilikuwa na ustaarabu usio wa kawaida. “Mambo mengi kati ya yale tunayoona ni mambo ya kawaida​—watu wakiwa na woga na hasira, wakionyesha upendo, wakiomba waonyeshwe upendo,” anasema Matthew Stolper, profesa wa mambo ya Ashuru katika Chuo Kikuu cha Chicago aliyehusika katika kazi hiyo katika muda wa miaka 30. Anaongezea hivi: “Kuna maandishi kutoka kwa wafalme yanayoeleza jinsi walivyokuwa mashuhuri, na maandishi kutoka kwa watu wengine yanayoeleza wazi kwamba wafalme hao hawakuwa mashuhuri kama wanavyodai.” Na maandishi yaliyopatikana huko Nuzi, eneo la Iraki ya leo, yanayoonyesha kesi zilizofanywa miaka 3,500 iliyopita kuhusu mambo kama vile urithi wa mjane fulani, uwanja ulio na mfumo wa kunyunyizia maji, na punda aliyeazimwa.

Je, Kazi Hiyo Ilikamilishwa?

Wachunguzi wa historia ya Ashuru kutoka sehemu zote duniani walihusika katika kazi hiyo. Wafanyakazi wa taasisi hiyo walitumia makumi ya miaka wakihifadhi kadi 2,000,000 hivi zinazoonyesha matumizi ya maneno. Buku la kwanza lilichapishwa katika mwaka wa 1956. Tangu wakati huo, mabuku mengine 25 yametolewa kadiri yalivyokuwa tayari. Mabuku yote yanauzwa kwa dola 2,000 (za Marekani) lakini habari yote inaweza kupatikana kwenye Intaneti, bila malipo.

Miaka 90 ilihitajika ili kukamilisha kamusi hiyo. Hata hivyo, wale waliofanya kazi hiyo kubwa walitambua upungufu wake. Makala moja iliyozungumzia kazi hiyo ilisema hivi: “Bado hawajui maana ya maneno fulani, na kwa sababu ugunduzi mwingine unafanywa kila wakati, bado . . . kazi hiyo inaendelea.”