Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Kijana Wako Anapojiumiza

Kijana Wako Anapojiumiza

KIKWAZO

Unagundua kuwa kijana wako amekuwa akijiumiza kimakusudi. Unajiuliza ‘Kwani kuna shida gani? Je, binti yangu anajaribu kujiua?’

Yaelekea hataki kujiua. Hata hivyo, ikiwa binti yako hujiumiza, * anahitaji msaada. Unaweza kumsaidiaje? Kwanza fikiria ni nini kinachomfanya ajiumize. *

KWA NINI JAMBO HILI HUTUKIA

Je, kujiumiza ni mtindo tu unaofuatwa na wengi? Ni kweli kwamba vijana fulani huanza kujiumiza kwa sababu wamesikia kwamba wengine hufanya hivyo. Hata ingawa huenda hilo likawa kweli, huu si mtindo wa kawaida tu. Kwa nini zoea hilo si jambo la kawaida? Msichana anayejiumiza hufanya hivyo kwa siri naye huaibikia sana tabia yake. Celia * mwenye umri wa miaka 20 anasema hivi: “Sikutaka mtu yeyote ajue nilichokuwa nikifanya, nilificha makovu yangu.”

Je, kujiumiza ni njia tu ya kufanya wengine wakuhurumie? Huenda vijana fulani wakajiumiza ili kuvuta fikira za wengine. Hata hivyo, zoea tunalozungumzia katika makala hii linahusu vijana ambao huficha mazoea yao na hawatumii majeraha au mikwaruzo yao kuwafanya wengine wawakazie fikira. Ingawa hivyo, kijana aliyekuwa akijiumiza hapo zamani anasema alitamani mtu fulani aone majeraha yake ili tatizo lake lijulikane na apate msaada haraka.

Basi, kwa nini watu hujiumiza? Si rahisi kueleza kinachowafanya watu wajiumize, lakini sababu kuu ni kwamba kijana anahisi maumivu ya kihisia ambayo hawezi kuyaeleza. Katika kitabu chake Cutting (Kujikata), mtaalamu wa afya ya akili Steven Levenkron anamfafanua anayejiumiza kuwa “mtu ambaye amegundua kwamba maumivu ya kimwili yanaweza kuponya maumivu ya kihisia.”

Mtu anayejiumiza huhisi maumivu ya kihisia ambayo hawezi kuyaeleza

Vipi ikiwa unajilaumu? Badala ya kufikiria kwamba wewe si mzazi mzuri na ndiyo sababu kijana wako anajiumiza, kazia fikira jinsi unavyoweza kuwa mzazi mzuri kwa kumsaidia aache zoea hilo.

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Mtie moyo binti yako azungumze nawe kuhusu kinachomsumbua. Madokezo yafuatayo yanaweza kusaidia.

Mfariji. Binti yako anapokuambia kwamba yeye hujiumiza, usishtuke kupita kiasi. Badala yake, ongea naye kwa utulivu na kwa njia yenye kufariji.—Kanuni ya Biblia: 1 Wathesalonike 5:14.

Usimuulize maswali kana kwamba unamhukumu. Kwa mfano, unaweza kusema: “Najua mara nyingi hujihisi vizuri. Ni mambo gani yanayokufadhaisha zaidi?” au “Ninaweza kufanya nini ili kukusaidia unapokuwa na wasiwasi au unaposhuka moyo?” au “Ni jambo gani muhimu sana ninaloweza kufanya ili kuboresha uhusiano wetu?” Sikiliza majibu yake bila kumkatiza.Kanuni ya Biblia: Yakobo 1:19.

Msaidie kijana wako atambue sifa zake nzuri. Kwa kuwa watu wanaojiumiza mara nyingi wanakazia fikira udhaifu wao, labda unaweza kumtia moyo binti yako atambue sifa zake nzuri. Unaweza kumpendekezea aorodheshe angalau mambo matatu anayopenda kujihusu. Msichana anayeitwa Briana anasema, “Kuorodhesha sifa zangu nzuri kulinisaidia kutambua kuwa nina sifa nzuri.” *

Mtie moyo kijana wako asali kwa Yehova Mungu. Biblia inasema: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’ (1 Petro 5:7) Lorena, mwenye umri wa miaka 17 anasema hivi: “Nilijitahidi kumweleza Yehova Mungu hisia zangu, hasa niliposhawishiwa kujiumiza. Jambo hilo lilinisaidia kujitahidi hata zaidi kuacha zoea hilo.”Kanuni ya Biblia: 1 Wathesalonike 5:17.

^ fu. 5 Kujiumiza ni tendo la kujidhuru kimakusudi, iwe ni kwa kujikata, kujikwaruza, kujipiga, au kwa njia nyingine.

^ fu. 5 Ingawa makala hii inamrejelea mtu anayejiumiza kuwa wa kike, kanuni zilizozungumziwa zinawahusu watu wote.

^ fu. 7 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 15 Mara nyingi, kujiumiza ni dalili za kushuka moyo au ugonjwa mwingine. Katika visa kama hivyo huenda ingefaa kumwona daktari. Amkeni! halipendekezi tiba yoyote hususa. Hata hivyo, Wakristo wanapaswa kuhakikisha kwamba matibabu yoyote wanayochagua hayapingani na kanuni za Biblia.