Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Kuwasiliana na Pepo

Kuwasiliana na Pepo

Je, ni makosa kujaribu kuwasiliana na wafu?

“Msiwaendee wenye kuwasiliana na pepo . . . ili kutiwa unajisi nao.” —Mambo ya Walawi 19:31.

WATU HUSEMA NINI?

Kwa kawaida watu wangependa kuhakikishiwa kwamba mpendwa wao aliyekufa hateseki. Huenda wakasema: “Ngoja tujaribu kuwasiliana naye kupitia kwa mchawi. Labda atatuambia mambo fulani ili kututuliza.”

BIBLIA INASEMA NINI?

Biblia inataja wazi maoni ya Mungu kuhusu zoea la kuwasiliana na wafu—ambalo lilikuwa limeenea hapo kale. Kwa mfano, Sheria ambayo Yehova Mungu aliwapa Waisraeli ilisema hivi:“Asipatikanendaniyakoyeyote. . .anayetafuta shauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo au . . . anayeuliza habari kutoka kwa wafu. Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 18: 10-12) Pia, Biblia inasema kwamba wale wanaowasiliana na pepo kwa njia yoyote ile “hawataurithi ufalme wa Mungu.”Wagalatia 5:19-21.

 Je, wafu wanaweza kuwadhuru au kuwasaidia walio hai?

“Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.”Mhubiri 9:5.

WATU HUSEMA NINI?

Watu wengi huamini kwamba wafu huendelea kuishi kwa njia nyingine. Hivyo, huenda wakajaribu kuwasiliana na wafu ili kupata habari fulani au kuwatuliza ili wasiwasumbue walio hai.

BIBLIA INASEMA NINI?

“Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe. . . . Upendo wao na chuki yao na wivu wao [waliokuwa nao wakiwa hai] tayari zimepotea.” (Mhubiri 9:5, 6) Kwa kweli, Biblia inafundisha kwamba mtu akifa haendelei— kuishi! Hawezi kufikiri, kutenda, wala kumwabudu Mungu. Andiko la Zaburi 115:17 linasema: “Wafu wenyewe hawamsifu [Mungu], wala wowote wanaoingia mahali penye kimya.”

Je, si ni kweli kwamba nyakati nyingine wachawi hutoa habari sahihi?

“Je, maombi yatolewe kwa watu waliokufa kwa ajili ya watu walio hai?”Isaya 8:19.

WATU HUSEMA NINI?

Watu fulani husema kwamba watu wanaowasiliana na pepo wanaweza kutoa habari zinazojulikana tu na wafu, watu wa familia, au rafiki zao.

BIBLIA INASEMA NINI?

Sura ya 28 ya kitabu cha 1 Samweli inasimulia kuhusu mfalme Sauli ambaye alivunja amri ya Mungu kwa kutafuta habari kutoka kwa mchawi. Alienda kwa mwanamke mchawi, ambaye ilionekana kana kwamba anazungumza na Samweli, mtumishi wa Mungu aliyekuwa amekufa! Lakini je, kweli alizungumza na Samweli? La! Alikuwa akizungumza na kiumbe aliyejifanya kuwa Samweli aliyekufa.

Kiumbe huyo alikuwa roho mwovu aliyetumiwa na “baba ya uwongo”—Shetani. (Yohana 8:44) Kwa nini roho waovu, au mashetani, wanataka watu waamini kwamba wafu wako hai? Lengo lao ni kumharibia Mungu sifa na kufanya watu wasiamini Neno lake, Biblia.2 Timotheo 3:16.

Je, hilo linamaanisha kwamba wafu hawana tumaini lolote? La hasha! Biblia inaahidi kwamba kutakuwa na ufufuo wa wale walio “usingizini” katika kaburi. * (Yohana 11:11-13; Matendo 24:15) Kwa sasa, tuna hakika kwamba wapendwa wetu waliokufa hawateseki hata kidogo.

^ fu. 16 Sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? ina kichwa “Tumaini Hakika kwa Wapendwa Wako Ambao Wamekufa.”