Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Jinsi ya Kutumia Wakati Wako Vizuri

Jinsi ya Kutumia Wakati Wako Vizuri

“Laiti ningalikuwa na muda zaidi!” Huenda umesema maneno hayo mara nyingi sana. Kwa njia fulani, wakati huwafanya wanadamu wote wawe sawa, kwa sababu matajiri na maskini wana kipimo kilekile cha wakati. Isitoshe, hakuna mtu yeyote anayeweza kuhifadhi wakati, awe maskini au tajiri. Wakati ukishapita, hauwezi kurudishwa tena. Kwa hiyo, jambo la hekima ni kutumia vizuri wakati tulio nao. Tunawezaje kufanya hivyo? Fikiria mbinu nne ambazo zimewasaidia watu wengi kutumia wakati wao vizuri.

Mbinu ya 1: Panga Mambo kwa Utaratibu

Tanguliza mambo muhimu. Biblia inashauri hivi: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Wafilipi 1:10) Andika orodha ya mambo muhimu au mambo ambayo ungependa kufanya haraka, ukitilia maanani kwamba huenda jambo muhimu lisiwe la haraka na jambo linaloonekana kuwa la haraka lisiwe muhimu. Kwa mfano, ingawa kununua chakula cha jioni ni jambo muhimu huenda lisiwe jambo la haraka, na ingawa kufika kwa wakati ili kutazama kipindi cha televisheni unachopenda likaonekana kuwa jambo la haraka, huenda lisiwe jambo muhimu. *

Panga mambo mapema. Andiko la Mhubiri 10:10 linasema: “Ikiwa kifaa cha chuma kimepoteza makali na mtu asikinoe, ndipo atatumia nguvu zake mwenyewe.” Kisha linaendelea kusema: “Kutumia hekima kwa mafanikio huleta faida.” Tunajifunza nini? Unaweza kunoa shoka lako kwa njia ya mfano kwa kupanga mambo mapema ili utumie wakati wako vizuri. Ahirisha au epuka mambo yasiyo muhimu ambayo yatakupotezea tu wakati na nguvu. Ikiwa una wakati wa ziada kwa sababu ulimaliza kazi yako mapema, fanya kazi uliyopangia kufanya baadaye. Kwa kupanga mambo mapema, utatimiza mengi, kama mfanyakazi mwenye hekima ambaye hunoa shoka lake.

Rahisisha maisha yako. Jifunze kukataa kufanya mambo ambayo si muhimu au mambo ambayo yatachukua wakati wako. Ukipanga kufanya mambo mengi kupita kiasi, utapatwa na mkazo na kukosa shangwe.

 Mbinu ya 2: Epuka Mambo Yanayopoteza Wakati

Kuahirisha na kusita-sita kufanya maamuzi. “Anayeuangalia upepo hatapanda mbegu; naye anayetazama mawingu hatavuna.” (Mhubiri 11:4) Tunajifunza nini? Ukiahirisha mambo utapoteza wakati na hutatimiza mengi. Mkulima anayengoja mpaka hali ziwe nzuri hatapanda mbegu wala kuvuna. Vivyo hivyo, huenda tusifanye maamuzi kwa sababu tuna wasiwasi kuhusu mambo yanayoweza kutokea maishani. Au huenda tukasubiri hadi tuwe na habari kamili ndipo tufanye uamuzi. Kwa kweli, mtu anahitaji kufanya utafiti na kufikiria sana kabla ya kufanya maamuzi muhimu. Methali 14:15 inasema: “Mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” Ukweli wa mambo ni kwamba hatuwezi kujua matokeo ya kila uamuzi tunaofanya.—Mhubiri 11:6.

Ukamilifu. ‘Hekima inayotoka juu au kutoka kwa Mungu ni yenye usawaziko,’ linasema andiko la Yakobo 3:17. Bila shaka ni vizuri kujiwekea viwango vya juu. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda tukajiwekea viwango vya juu sana na kushindwa kuvifikia na hivyo kukata tamaa. Kwa mfano, mtu ambaye anajifunza lugha mpya anapaswa kujua kwamba atafanya makosa, na atajifunza kutokana na makosa hayo. Hata hivyo, mtu anayetaka kufanya kila kitu kwa ukamilifu ataogopa kukosea na hilo linaweza kumzuia kujifunza lugha hiyo. Ni vizuri kuwa na kiasi kuhusiana na mambo tunayotaka kutimiza! “Wenye kiasi wana hekima,” inasema Methali 11:2. Isitoshe, watu wenye kiasi na unyenyekevu hawachukui kila jambo kwa uzito na wanaweza kucheka wanapokosea.

“Hulipii vitu kwa pesa. Unavilipia kwa wakati unaotumia..”—Kitabu What to Do Between Birth and Death

 Mbinu ya 3: Uwe Mwenye Usawaziko na Uone Mambo Kihalisi

Uwe na usawaziko katika kazi na burudani. “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.” (Mhubiri 4:6) Mara nyingi watu ambao hufanya kazi kupita kiasi hawafurahii matunda ya “konzi mbili za kazi [yao] ngumu.” Hawana wakati wala nguvu za kufurahia matunda ya kazi yao. Kwa upande mwingine, wavivu hutaka tu “konzi mbili” za pumziko na hutumia vibaya wakati wao. Biblia inatutia moyo tuwe na mtazamo huu uliosawazika: Fanya kazi kwa bidii na ufurahie matunda yake. Kushangilia kwa njia hiyo ni “zawadi ya Mungu.”—Mhubiri 5:19.

Lala vya kutosha. Mwandikaji mmoja wa Biblia alisema hivi: “Katika amani nitajilaza na kulala usingizi.” (Zaburi 4:8) Watu wazima wanahitaji kulala kwa saa nane hivi kila siku ili wapate nguvu za kimwili, kihisia, na waboreshe uwezo wao wa kufikiri. Kutenga wakati wa kulala vya kutosha kuna faida kwa sababu kunasaidia mtu awe makini na pia aweze kukumbuka mambo na hivyo kujifunza haraka. Kinyume na hilo, kukosa kulala vya kutosha kunamzuia mtu kujifunza na kunaweza kusababisha aksidenti, makosa, na kukasirika-kasirika.

Weka miradi unayoweza kufikia. “Heri kuona kwa macho kuliko kutangatanga kwa tamaa.” (Mhubiri 6:9, Union Version.) Tunajifunza nini? Mtu mwenye hekima haongozwi na tamaa maishani, hasa tamaa ambazo haziwezi kutoshelezwa. Kwa hiyo, hashawishiwi na matangazo ya biashara au njia rahisi za kupata mkopo. Badala yake, anajifunza kutosheka na mambo anayoweza kupata, yaani, kile ‘anachoona kwa macho.’

 Mbinu ya 4: Ongozwa na Maadili Mazuri

Fikiria maadili yako. Maadili yako hukusaidia kuamua jambo lililo sawa, muhimu, na linalofaa. Ikiwa maisha yako yangekuwa mshale, basi mshale huo ungelengwa na maadili yako. Kwa hiyo, maadili mazuri hukusaidia kujua mambo ya kutanguliza maishani na kutumia wakati wako vizuri kila saa na kila siku. Unaweza kupata wapi maadili hayo? Watu wengi huchunguza Biblia, kwa kuwa wanatambua kwamba ina hekima ya hali ya juu.—Methali 2:6, 7.

Fanya upendo uwe sifa yako kuu. Andiko la Wakolosai 3:14 linasema kwamba upendo “ni kifungo kikamilifu cha muungano.” Hatuwezi kuwa na furaha ya kweli na kuhisi tunapendwa ikiwa hakuna upendo, hasa katika familia. Watu ambao hupuuza jambo hilo, huenda kwa kutanguliza mali au kazi, hawana furaha. Hiyo ndiyo sababu Biblia inakazia sifa ya upendo kwa kuitaja mara nyingi sana.—1 Wakorintho 13:1-3; 1 Yohana 4:8.

Tenga wakati wa kujifunza kumhusu Mungu. Mwanamume mmoja anayeitwa Geoff alikuwa na mke aliyempenda, watoto wawili wachangamfu, marafiki wazuri, na kazi yenye kuridhisha akiwa mhudumu wa matibabu ya dharura. Hata hivyo, mara kwa mara alijionea watu wakiteseka na kufa. Alijiuliza, “Je, hivi ndivyo maisha yanavyopaswa kuwa?” Kisha siku moja alisoma vitabu fulani vinavyozungumzia Biblia ambavyo huchapishwa na Mashahidi wa Yehova na akapata majibu yenye kuridhisha.

Geoff alimwambia mke na watoto wake mambo aliyokuwa akijifunza, nao wakapendezwa. Familia hiyo ilianza kujifunza Biblia na hilo liliboresha maisha yao na kuwasaidia kutumia wakati wao vizuri. Pia, kwa kujifunza Biblia walipata tumaini zuri la kufurahia milele maisha yenye kusudi katika ulimwengu usio na mateso.—Ufunuo 21:3, 4.

Kisa cha Geoff kinatukumbusha maneno ya Yesu Kristo, aliyesema: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Je, uko tayari kutenga wakati wa kutosheleza uhitaji wako wa kiroho? Kwa kweli, ukifanya hivyo utapata hekima itakayokusaidia kutumia vizuri wakati wako na pia maisha yako.

^ fu. 5 Ona makala “Mbinu 20 za Kutafuta Wakati Zaidi,” katika gazeti Amkeni! la Aprili 2010.