Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA

Namna ya Kutumia Wakati Wako kwa Hekima

Namna ya Kutumia Wakati Wako kwa Hekima

“Ikiwa tu ningekuwa na wakati zaidi!” Umekwisha kusema hivyo mara ngapi? Kwa njia fulani, wanadamu wote wana wakati uleule, kwa sababu watu wenye uwezo na matajiri hawana wakati mwingi kupita watu wa hali ya chini na maskini. Tena, hakuna mutu anayeweza kujiwekea akiba ya wakati, iwe tajiri wala maskini. Wakati ukipita, haurudie tena. Kwa hiyo, ni jambo la hekima tutumie wakati wetu vizuri. Namna gani? Fikiria njia ine ambazo zimesaidia watu wengi watumie wakati wao kwa hekima.

Njia ya 1: Upange Wakati Wako

Upange mambo ya kutia pa nafasi ya kwanza. Biblia inatushauri hivi: ‘Muhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Wafilipi 1:10) Andika kwenye karatasi mambo yote unayotaka kufanya yaliyo ya maana ao ya haraka ao yote mbili, ukifikiria katika akili yako kwamba mambo yote ya maana si lazima yawe ya haraka. Kwa mufano, pengine kuenda kuuza nguo za mupya hakuwezi kuwa jambo la haraka kabisa. Na jambo ambalo linaonekana kuwa la haraka, kwa mufano, kufuata mwanzo wa programu ya televisheni unayofurahia sana, hakuwezi kuwa jambo la maana sana. *

Ufikiri mbele ya wakati. Andiko la Mhubiri 10:10 linasema hivi: ‘Ikiwa kifaa cha chuma kimepoteza makali na mutu asikinoe, ndipo atatumia nguvu zake mwenyewe.’ Andiko hilo linaongeza hivi: ‘[Lakini] kutumia hekima kwa mafanikio kunaleta faida.’ Andiko hilo linatupatia somo gani? Ni lazima tupange mambo mbele ya wakati ili kutumia wakati wetu vizuri zaidi. Upange kufanya mambo mengine baadaye ao uondoe kazi zisizo za lazima ambazo zinakupotezea tu wakati na nguvu. Ikiwa unapata wakati kwa sababu kazi iliisha mbele, unaweza kufanya jambo ambalo ulipanga kufanya baadaye. Kwa kufikiri mbele ya wakati utakuwa na matokeo mazuri zaidi, kama mufanyakazi mwenye hekima anayenoa kifaa chake.

Upunguze mambo fulani katika maisha yako. Jifunze kukataa mambo yasiyo ya maana ao yanayokupotezea tu wakati. Kuwa na mipango mingi na mambo mengi ya kufanya kunaweza kukuongezea mahangaiko yasiyo ya lazima na kukufanya ukose furaha.

Njia ya 2: Uepuke Mambo Yanayoiba Wakati

Tabia ya kuchelewesha mambo na kusitasita kuchukua uamuzi. “Anayeuangalia upepo hatapanda mbegu; naye anayetazama mawingu hatavuna.” (Mhubiri 11:4) Andiko hilo linatupatia somo gani? Tabia ya kuchelewesha mambo inatuiba wakati na inafanya tusipate matokeo mazuri. Mulimaji anayechunga hali ziwe nzuri zaidi hawezi kupanda mbegu wala kuvuna hata siku moja. Vilevile, tunaweza kuacha mambo yasiyotazamiwa yanayotokea katika maisha yatufanye kuwa watu wenye kusitasita kuchukua uamuzi. Ao tunaweza kufikiri kwamba ni lazima tungojee mupaka tupate habari zote za maana mbele ya kuchukua uamuzi fulani. Bila shaka, inaomba kufanya utafiti na kufikiri ili kuchukua maamuzi ya maana. Andiko la Methali 14:15 linasema hivi: ‘Mutu mwerevu anazifikiria hatua zake.’ Lakini ukweli ni kwamba maamuzi mengi yanachukuliwa bila kujali mambo fulani yasiyotazamiwa.​—Mhubiri 11:6.

Kupenda kufanya mambo bila kukosea hata kidogo. Andiko la Yakobo 3:17 linasema hivi: “Hekima inayotoka juu [ao kwa Mungu] kwanza kabisa ni . . . yenye usawaziko.” Kwa kweli, si vibaya kuwa na nia ya kufanya mambo vizuri! Hata hivyo, wakati fulani, tunaweza kutaka kufanya mambo bila kukosea hata kidogo na hilo linaweza kutuvunja moyo ao hata kutufanya tushindwe. Kwa mufano, mutu anayejifunza luga nyingine, anapaswa kutazamia kwamba atafanya makosa, akijua kwamba atajifunza kutokana na makosa hayo. Lakini, mutu anayetaka kufanya mambo bila kukosea hata kidogo, anaweza kuogopa kutamka neno fulani vibaya na hilo linaweza kumuzuia asifanye maendeleo. Ni vizuri tuwe na usawaziko katika mambo tunayotazamia kufanya! Andiko la Methali 11:2 linasema hivi: “Wenye kiasi [ao usawaziko] wana hekima.” Zaidi ya hayo, watu wanyenyekevu na wenye usawaziko hawajione kuwa bora sana na wanaweza kujicheka mara nyingi wanapofanya makosa.

“Kwa kweli hatuuze vitu kwa feza. Tunaviuza kupitia wakati.”—What to Do Between Birth and Death

Njia ya 3: Uwe na Maoni Yenye Usawaziko na Yanayofaa

Uwe na usawaziko kuhusu kazi na mambo ya kujifurahisha. ‘Konzi moja ya pumuziko ni afazali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.’ (Mhubiri 4:6) Mara nyingi watu wanaojifanya kuwa watumwa wa kazi hawapate matokeo ya “konzi mbili [ao mikono miwili yenye kujaa] za kazi ngumu” wanayofanya. Wanajikuta hawana tena wakati na nguvu. Kwa upande mwengine, mutu muvivu anachagua “konzi mbili” za pumuziko na anapoteza wakati wake wa maana. Biblia inatushauri tutumike kwa bidii na tufurahie matokeo ya kazi yetu. Furaha hiyo ni “zawadi ya Mungu.”​—Mhubiri 5:19.

Ulale vya kutosha. Muandikaji mumoja wa Biblia alisema hivi: “Katika amani nitajilaza na kulala usingizi.” (Zaburi 4:8) Watu wazima wanahitaji kulala kwa muda wa saa 8 kila usiku ili wawe na hali nzuri ya mwili, ya moyo, na ya akili. Kuhusu jambo hilo, mutu anayelala vya kutosha anatumia wakati wake vizuri; kwa sababu usingizi unasaidia mutu kukaza akili juu ya mambo fulani, kukumbuka mambo, na hivyo mutu anakuwa na uwezo wa kujifunza. Lakini, kukosa kulala vya kutosha kunapunguza uwezo wa kujifunza na kunachangia kutokeza aksidenti, makosa, na kukasirika haraka.

Ujiwekee miradi unayoweza kutimiza. “Ni heri kuona kwa macho kuliko kutangatanga kwa tamaa.” (Mhubiri 6:9; La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo) Andiko hilo linatupatia somo gani? Mutu mwenye hekima haache tamaa ziongoze maisha yake, zaidi sana tamaa zisizofaa ao ambazo hawezi kutimiza. Kwa hiyo, hashawishiwe na matangazo ya ujanja ao ya kupata mukopo haraka. Lakini, anajifunza kutosheka na mambo anayoweza kutimiza, ni kusema, yale ‘anayoona kwa macho.’

Njia ya 4: Uongozwe na Kanuni za Mungu

Ufikirie kanuni zinazokuongoza. Kanuni zinazokuongoza zinakuwezesha kujua mambo mazuri, ya maana, na yanayostahili. Ikiwa maisha yako yana kusudi, kanuni zinazokuongoza zitakusaidia ufuatilie kusudi hilo. Kwa hiyo, kanuni nzuri zinakusaidia kutia mambo ya maana katika maisha pa nafasi ya kwanza na kutumia wakati wako vizuri kila saa na kila siku. Unaweza kupata wapi kanuni kama hizo? Watu wengi wanazitafuta katika Biblia, sababu wanajua kwamba Biblia ina hekima ya hali ya juu.​—Methali 2:6, 7.

Ufanye upendo uwe kanuni yako ya kwanza. Andiko la Wakolosai 3:14 linasema kwamba upendo “ni kifungo kikamilifu cha muungano.” Bila upendo, hatuwezi kuwa na furaha kabisa na kuwa na amani ya moyoni, zaidi sana katika familia. Watu wanaozarau hilo, labda kwa kutanguliza utajiri na kazi yao, hawawezi kuwa na furaha. Ndiyo sababu Biblia inafanya upendo kuwa kanuni ya maana, neno hilo linapatikana mara nyingi sana katika Biblia.​—1 Wakorintho 13:1-3; 1 Yohana 4:8.

Upange wakati wa kutimiza uhitaji wako wa kumujua Mungu. Mwanaume mumoja anayeitwa Geoff alikuwa na bibi muzuri, watoto wawili wenye furaha, marafiki wazuri, na kazi yenye mushahara muzuri sana, ni kusema, alikuwa munganga wa kushugulikia hali zinazoomba kutenda haraka. Lakini, kazi yake ilimufanya aone mara nyingi watu wakiteseka na kufa. Alijiuliza hivi: “Je, maisha yalipangwa kuwa hivi?” Kisha, siku moja akasoma vichapo fulani vinavyotegemea Biblia vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova na akapata majibu yenye kufurahisha.

Geoff alimuelezea bibi yake na watoto wake mambo aliyokuwa anajifunza, nao pia wakapendezwa na mambo hayo. Familia yake ilianza kujifunza Biblia, na funzo lao la Biblia lilifanya maisha yao yawe mazuri zaidi na liliwasaidia kutumia wakati wao kwa hekima zaidi. Kupitia funzo lao la Biblia walipata tumaini nzuri la uzima wa milele katika dunia isiyokuwa na mambo yasiyofaa kitu na mateso.​—Ufunuo 21:3, 4.

Habari hiyo ya Geoff inatukumbusha maneno haya ya Yesu Kristo: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Je, wewe pia una nia ya kupanga wakati kidogo ili kutimiza uhitaji wako wa kumujua Mungu? Kwa kweli, hakuna jambo lingine linaweza kukupatia hekima ya kufanya mambo ya maana, si siku moja tu, lakini katika maisha yako yote.

^ Soma habari, “Mbinu 20 za Kutafuta Wakati Zaidi,” katika gazeti Amuka! la Mwezi wa 4, 2010.