Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 TUNAYOJIFUNZA KUTOKANA NA HISTORIA

Konstantino

Konstantino

Konstantino alikuwa maliki wa kwanza wa Roma kudai kuwa Mkristo. Kwa kufanya hivyo, alikuwa na uvutano mkubwa kwenye historia ya ulimwengu. Aliikubali dini hiyo ambayo hapo awali waumini wake waliteswa na alisaidia kuanzisha dini zinazodai kuwa za Kikristo. Hivyo, Ukristo huo ukawa “chombo chenye nguvu zaidi kisiasa na kijamii” kilichobadili historia, kulingana na ensaiklopidia moja (The Encyclopædia Britannica).

KWA nini utake kujua kuhusu maliki wa zamani wa Roma? Ikiwa unapendezwa na Ukristo, basi unapaswa kujua kwamba harakati za kisiasa na za kidini za Konstantino zimeathiri imani na desturi za makanisa mengi leo. Hebu tuone jambo hilo.

MAKANISA—YATAMBULIWA KISHERIA KISHA YATUMIWA VIBAYA

Katika mwaka wa 313 W.K., Konstantino alitawala majimbo ya Magharibi ya Milki ya Roma, na Licinius na Maximinus wakatawala Majimbo ya Mashariki. Konstantino na Licinius waliwapa watu wote uhuru wa kuabudu kutia ndani Wakristo. Konstantino aliulinda Ukristo, kwa kuwa aliamini dini hiyo ingewaunganisha watu katika milki yake. *

Konstantino alishangaa kuona migogoro mingi iliyogawanya Ukristo. Akiwa na nia ya kuleta makubaliano, alianzisha na baadaye kulazimisha watu wafuate mafundisho aliyodai kuwa ya kweli. Ili kumfurahisha, makasisi walilegeza msimamo wao na kwa kufanya hivyo, hawakutozwa kodi na pia walipewa misaada mingi ya kifedha. Mwanahistoria Charles Freeman aliandika: “Kufuata mafundisho ya Kikristo yaliyoonwa kuwa ya kweli kulifungua njia ya kuingia mbinguni na pia njia ya kupata mali nyingi duniani.” Makasisi wakawa watu mashuhuri katika mambo ya ulimwengu. Mwanahistoria  A.H.M. Jones alisema: “Kanisa lilikuwa limepata mlinzi na pia bwana mkubwa.”

“Kanisa lilikuwa limepata mlinzi na pia bwana mkubwa.”—Mwanahistoria A.H.M. Jones

JE, ULIKUWA UKRISTO WA KWELI?

Mapatano kati ya Konstantino na maaskofu yalitokeza dini yenye mafundisho ya Kikristo na ya kipagani. Isingeweza kuwa vingine, kwa kuwa lengo lake halikuwa kutafuta dini ya kweli bali alitaka kuunganisha imani mbalimbali. Kwa kweli, alikuwa mtawala wa milki ya kipagani. Mwanahistoria mmoja alisema kuwa, ili kufurahisha dini zote, Konstantino aliamua “kutounga mkono waziwazi upande wowote katika shughuli zake za kibinafsi na za serikali kwa ujumla.”

Ingawa alidai kuutetea Ukristo, Konstantino alishikilia imani za kipagani. Kwa mfano, alikuwa mnajimu na mwaguzi—mazoea ya kichawi ambayo Biblia hukataza. (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Tao la Konstantino huko Rome lina mchoro wake akitoa dhabihu kwa miungu ya kipagani. Aliendelea kumtukuza mungu huyo kwa kuweka picha yake kwenye sarafu na kuendeleza ibada ya mungu-jua. Na baadaye hata aliruhusu wakaaji wa mji mdogo wa Umbria, huko Italia wajenge hekalu kwa ajili yake na familia yake, na akaweka makuhani wahudumu katika hekalu hilo.

Konstantino alibatizwa na kuwa “Mkristo” siku chache kabla ya kifo chake mwaka wa 337 W.K. Wasomi wengi huamini kuwa aliahirisha kubatizwa ili aendelee kuungwa mkono kisiasa na Wakristo na wapagani katika milki yake. Kwa kweli, maisha yake na kuchelewa kwake kubatizwa kunafanya watu wengi watilie shaka imani yake ya Kikristo. Hata hivyo, jambo moja ni hakika: Kanisa ambalo Konstantino aliweka rasmi lilikuja kuwa shirika lenye nguvu kisiasa na kidini, ambalo lilimwacha Kristo na kufuata mambo ya ulimwengu. Lakini, Yesu alisema hivi kuhusu wafuasi wake: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14) Kanisa hilo—ambalo sasa lilikuwa linafuata mambo ya ulimwengu—lilitokeza madhehebu mengine mengi.

Tunajifunza nini kutokana na mambo hayo yote? Hatupaswi kukubali tu mafundisho ya kanisa lolote bali tunahitaji kuyachunguza kwa kutumia Biblia.—1 Yohana 4:1.

^ fu. 6 Watu wengi wanatilia shaka ikiwa kwa kweli Konstantino aligeuka na kuwa Mkristo, kwa sababu, kulingana na kitabu fulani, aliendelea “kukubali ibada za kipagani, hadi mwishoni mwa utawala wake.”