Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Machozi Yako ya Ajabu

Machozi Yako ya Ajabu

KILIO huambatana nasi kuanzia siku tunayozaliwa. Mtaalamu mmoja anaeleza kwamba kwa watoto wachanga, uhai wao hutegemea kilio kwa kuwa wao hulia ili kupata mahitaji ya kimwili na ya kihisia. Lakini, kwa nini tunaendelea kulia hata tunapokuwa watu wazima?

Tunatokwa na machozi ya hisia kwa sababu mbalimbali. Tunaweza kulia kwa sababu ya huzuni, kuchanganyikiwa, na mateso ya kimwili au ya kiakili. Lakini pia msisimko, kitulizo, na mafanikio hutufanya tutoe machozi ya hisia, hayo huitwa machozi ya furaha. Machozi pia huambukiza. María anasema: “Nikiona mtu akilia, hata kama sijui sababu, mimi pia hutokwa na machozi.” Labda hata hadithi za kutungwa kwenye sinema au vitabu zimekufanya ulie.

Vyovyote vile, kulia ni lugha kubwa isiyo na maneno. Kitabu kimoja kuhusu kulia (Adult Crying) kinaeleza: “Kulia ni moja kati ya njia chache za kusema mengi katika muda mfupi.” Machozi hutuchochea kutenda. Kwa mfano, wengi wetu hatuwezi kupuuza tunapoona mtu akitokwa na machozi ya huzuni kwani yanatuambia kwamba mtu huyo anateseka. Hivyo, tunaweza kuitikia kwa kumfariji au kumsaidia mtu anayelia.

Wataalamu fulani wanaamini kulia ni njia nzuri ya kutoa yaliyo moyoni na tukizoea kuepuka kulia tunaweza kudhuru afya zetu. Wengine wanabisha, wakidai kwamba faida za kimwili au za kiakili za kulia bado hazijathibitishwa kisayansi. Hata hivyo, utafiti unaonyesha kwamba asilimia 85 ya wanawake na asilimia 73 ya wanaume huhisi vizuri baada ya kulia. Noemí anasema: “Kuna wakati najua nahitaji kulia, ili niweze kutulia na kuona mambo kwa njia nzuri zaidi.”

Utafiti unaonyesha kwamba asilimia 85 ya wanawake na asilimia 73 ya wanaume huhisi vizuri baada ya kulia

Lakini hisia hii ya kupata nafuu haisababishwi tu na machozi tunayotoa. Jinsi watu wanavyoitikia wanapotuona tukilia pia huchangia hali hiyo. Kwa mfano, machozi yetu yanapowachochea wengine kutufariji  na kutusaidia, tunapata nafuu. Lakini wakitupuuza, basi tunaweza kuhisi aibu au hata kuhisi hatupendwi.

Kwa kweli, bado kilio ni fumbo. Tunachojua kwa uhakika ni kwamba kulia ni moja ya njia za ajabu ambazo Mungu ametupa ili tuonyeshe hisia zetu.