Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, UNAONGOZA MAISHA YAKO?

Changamoto: Kulemewa na Shughuli

Changamoto: Kulemewa na Shughuli

WATOTO wanahitaji uwahudumie haraka. Mwajiri wako pia anakuhitaji. Mwenzi wako pia anahitaji ufanye jambo fulani. Wakati huohuo unahitaji kuwatunza wazazi wako wagonjwa. Halikuwa lengo lako kuwa na maisha hayo yenye shughuli nyingi. Unajiuliza hivi: “Nifanye nini?” “Watu wananihitaji!” Huenda isiwe rahisi kwako kutimiza mahitaji yako na ya wengine. Unawezaje kuongoza mambo?

MFANO KATIKA BIBLIA: MUSA

Akiwa hakimu pekee wa Israeli katika nyakati za Biblia, huenda Musa alihisi kwamba anatimiza wajibu wake. Lakini baba-mkwe wake alimwambia hivi: “Si vema jinsi unavyofanya. Utachoka.” Alimshauri Musa achague wanaume wenye uwezo ili wawe wakihukumu badala yake, na yeye ashughulikie kesi ngumu. Matokeo yangekuwa nini? Baba-mkwe wa Musa alimhakikishia hivi: “Hapo ndipo hakika utakapoweza kulistahimili na, zaidi ya hilo, watu hawa wataenda mahali pao wenyewe kwa amani.”—Kutoka 18:17-23.

MAMBO ANAYOFANYA DELINA

Kama ilivyotajwa katika makala ya kwanza, Delina ana ugonjwa wa neva za misuli unaoitwa dystonia. Anawatunza pia ndugu zake watatu wenye ulemavu. Anasema hivi: “Nimetambua kwamba kutohangaikia ya kesho na kuepuka kuahirisha mambo hupunguza mkazo. Kuwaambia wengine kuhusu hali yangu huwafanya wengi wanisaidie, hasa mume wangu. Pia, ninatumia kipindi fulani kila asubuhi ili kutunza bustani. Hilo limenisaidia nihisi kwamba nimetimiza jambo fulani.”

“Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu.”—Mhubiri 3:1

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Ikiwa unalemewa na shughuli nyingi, jaribu kufanya yafuatayo:

  • Jitahidi kutafuta mtu anayeweza kukusaidia. Kwa mfano, je, unaishi na watoto wanaoweza kukusaidia? Je, una ndugu au marafiki wanaoishi karibu nawe wanaoweza kukusaidia?

  • Zungumza na wengine kuhusu kile unachohitaji. Kwa mfano, zungumza na mwajiri wako ikiwa anataka ufanye kazi kupita kiasi tofauti na makubaliano. Hilo halimaanishi umtishie kwamba utaacha kazi ikiwa hatakusikiliza. Lengo lako ni kumjulisha changamoto unazokabili. Huenda mwajiri wako akakubali kukupunguzia kazi.

  • Panga ratiba ya kazi unazohitaji kutimiza kwa kila juma. Je, kuna kazi unayoweza kuwakabidhi wengine?

  • Si lazima ukubali kila mwaliko unaopewa na wengine. Ikiwa hutaweza kuhudhuria kwa sababu ya kukosa wakati au kuchoka, unaweza kukataa mwaliko huo kwa busara.

Jambo Kuu: Ukijaribu kufanya kila kitu, huenda ukashindwa kutimiza mambo mengine.