Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI KUBWA

Yesu Aliishi Kabisa Duniani?

Yesu Aliishi Kabisa Duniani?

ALIKUWA mutu wa kawaida na hakuwa tajiri. Hakuwa hata na nyumba yake. Hata hivyo, mafundisho yake yamechochea maisha ya mamilioni ya watu. Yesu Kristo aliishi kabisa duniani? Watu wenye elimu wa leo na wa zamani wanasema nini?

  • Michael Grant, mwanahistoria na mutu mwenye elimu ya desturi za zamani, alisema hivi: “Ikiwa tunajifunza Agano Jipya kama vile tunajifunza maandishi mengine ya zamani, hatuna sababu ya kukataa kwamba Yesu aliishi kabisa duniani kama vile hatujakuwaka na mashaka juu ya wapagani wengi wenye kuzungumuziwa katika historia.”

  • Rudolf Bultmann, profesa wa masomo ya Agano Jipya, alisema hivi: “Mashaka ya kwamba Yesu aliishi kabisa duniani hayana musingi na haiko lazima kubishana juu ya jambo hilo. Hakuna mutu mwenye kuwa na akili nzuri anaweza kuwa na mashaka kwamba ni Yesu ndiye alianzisha kikundi cha zamani sana [cha Wakristo] cha Palestina.”

  • Will Durant, mwanahistoria, muandikaji, na pia mwanafilozofia, aliandika hivi: “Kama wanaume kidogo na wa kawaida [Waandikaji wa Injili] wangeweza kujitungia, katika kizazi kimoja, mutu mwenye kuwa na sifa za ajabu sana na zenye kuvutia, mwenye mwenendo muzuri sana na mwenye kuonyesha kwa njia ya ajabu namna ya kuishi na watu, huo ungekuwa muujiza wenye kushangaza sana kuliko muujiza wowote wenye kuwa katika Vitabu vya Injili.”

  • Albert Einstein, mwanasayansi Muyahudi mwenye alizaliwa Ujerumani, alisema hivi: “Mimi ni Muyahudi, lakini ninashangazwa sana na ule Munazareti mwenye kuvutia.” Wakati aliulizwa ikiwa anaamini kwamba Yesu aliishi kabisa duniani, alijbu hivi: “Hakuna mashaka! Hakuna mutu mwenye anaweza kusoma Vitabu vya Injili na akose kuona kama Yesu ni mutu wa kweli kabisa. Utu wake unaonekana katika kila neno. Hakuna habari yoyote ya kuwazia yenye inaweza kueleza mambo hivyo.”

    “Hakuna mutu mwenye anaweza kusoma Vitabu vya Injili na akose kuona kama Yesu ni mutu wa kweli kabisa.”—Albert Einstein

HISTORIA INASEMA NINI?

Habari juu ya maisha na utumishi wa Yesu inazungumuziwa sana katika sehemu ya Biblia yenye kuitwa Vitabu vya Injili. Vitabu hivyo vinaitwa kwa majina ya wenye waliviandika: Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. Zaidi ya hilo, maandishi mengine ya zamani yenye haiko ya Kikristo yanamutaja Yesu.

  • TASITO

    (Aliishi karibu na mwaka wa 56 mupaka mwaka wa 120 K.K.Y., ao Kisha Kuzaliwa kwa Yesu) Tasito anajulikana kuwa mumoja kati ya wanahistoria wa zamani wa Roma. Kitabu chake chenye kuitwa Annales kinazungumuzia Utawala wa Roma kuanzia mwaka wa 14 K.K.Y. mupaka mwaka wa 68 K.K.Y. (Yesu alikufa katika mwaka wa 33) Tasito aliandika kwamba wakati moto mukubwa uliharibu muji wa Roma katika mwaka wa 64 K.K.Y., Mutawala Nero ndiye aliwaziwa kuwa alifanya jambo hilo. Lakini Tasito aliandika kwamba Nero aliwashitaki Wakristo kuwa ndio walifanya jambo hilo ili “kumaliza habari hiyo yenye ilienea.” Tena, Tasito alisema hivi: “Kristo, mwenye lile jina [Mukristo] lilitokana na jina lake, alihukumiwa kifo na gavana Pontio Pilato wakati wa utawala wa Tiberio.”—Annales, XV, 44.

  • SUÉTONE

    (Aliishi karibu na mwaka wa 69 mupaka kisha mwaka wa 122 K.K.Y.) Katika kitabu chake Vies des douze Césars, mwanahistoria huyo Muroma anazungumuzia mambo yenye yalitokea wakati wa Watawala 11 wa kwanza wa Roma. Sehemu yenye kuzungumuzia Klaudio inaonyesha muvurugo wenye ulitokea kati ya Wayahudi katika muji wa Roma, pengine kwa sababu ya kutoelewana kuhusu Yesu. (Matendo18:2) Suétone aliandika hivi: “Kwa sababu kila mara Wayahudi walitokeza fujo kuhusu Krestasi [Kristo], yeye [Klaudio] aliwafukuza kutoka Roma.” (Le dieu Claude, XXV, 4) Hata kama alisema uongo kwamba watu walikuwa katika muvurugo kwa sababu ya Yesu, Suétone hakuwa na mashaka kama Yesu aliishi kabisa duniani.

  • PLINI MUDOGO

    (Aliishi karibu na mwaka wa 61 mupaka mwaka wa 113 K.K.Y.) Muandikaji huyo Muroma na pia gavana wa Bithinia (katika Turquie ya leo) alimuandikia Mutawala wa Roma mwenye kuitwa Trajani kuhusu namna ya kutendea Wakristo wa jimbo hilo. Plini alisema kama alijaribu kukaza Wakristo wakatae imani, kwa kuua Mukristo yeyote mwenye alikataa kufanya hivyo. Alisema hivi: “Wale wenye . . . walikuwa wanatoa sala kwa Miungu [ya kipagani] kisha mimi, na wenye waliabudu sanamu yako kupitia divai na ubani . . . na ambao walifikia kumulaani Kristo . . . , niliwaza ni muzuri kuwaacha huru.”—Pliny— Letters, Book X, XCVI.

  • FLAVIUS JOSÈPHE

    (Aliishi karibu na mwaka wa 37 mupaka 100 K.K.Y.) Alikuwa kuhani na mwanahistoria Muyahudi. Alisema kwamba Anasi, kuhani mukubwa Muyahudi mwenye kila mara alikuwa na neno la kusema katika mambo ya siasa, “alikusanya waamuzi wa Sanhedrini [tribinali kubwa ya Wayahudi] na kuleta mbele yao mwanaume mwenye kuitwa Yakobo, ndugu ya ule Yesu mwenye aliitwa Kristo.”—Antiquités judaïques, XX, 200.

  • TALMUD

    Kitabu hicho chenye kuwa na maandishi ya marabi Wayahudi cha tangu mwaka kati ya 201 mupaka 600 K.K.Y., kinaonyesha kwamba hata maadui wa Yesu walisema kama Yesu aliishi duniani. Sehemu moja ya maandishi hayo inasema kwamba kwenye “Siku yenye ilitangulia Pasaka, Yeshu [Yesu] Munazareti alitundikwa;” historia inashuhudia jambo hilo. (Babylonian Talmud, Sanhedrin 43a, Munich Codex; Ona Yohana 19:14-16.) Sehemu ingine inasema hivi: “Tusitokeze mwana ao mwanafunzi mwenye atajizaraulisha mbele ya watu kama vile ule Munazareti,” jina lenye Yesu alipewa.—Babylonian Talmud, Berakoth 17b, maelezo ya chini, Munich Codex; Ona Luka 18:37.

USHUHUDA WA BIBLIA

Vitabu vya Injili vinatusaidia kuelewa muzuri sana maisha na utumishi wa Yesu, kutia ndani mambo madogo-madogo kuhusu watu, mahali, na wakati; mambo hayo yanaonyesha kwamba historia hiyo ni ya kweli. Mufano moja wenye unapatikana katika Luka 3:1, 2, unatusaidia kujua ni wakati gani mwanaume mwenye kuitwa Yohana Mubatizaji, ambaye alimutayarishia Yesu njia, alianza kazi yake.

“Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.” —2 Timotheo 3:16

Luka aliandika hivi: ‘Katika mwaka wa kumi na tano wa kumiliki kwa Kaisari Tiberio, Pontio Pilato alipokuwa gavana wa Yudea, na Herode alipokuwa mutawala wa wilaya ya Galilaya, lakini Filipo ndugu yake alikuwa mutawala wa wilaya wa inchi ya Iturea na Trakoniti, na Lisania alikuwa mutawala wa wilaya ya Abilene, katika siku za mukubwa wa makuhani Anasi na za Kayafa, tangazo la Mungu likamujia Yohana mwana wa Zekaria nyikani.’ Habari hiyo yenye kuwa wazi sana, inatusaidia kuelewa kwamba ‘tangazo la Mungu lilimujia Yohana’ katika mwaka wa 29 K.K.Y.

Wanahistoria wanajua muzuri watu hao saba wenye Luka anataja. Hata hivyo, wakati fulani kuko wachambuzi wenye walikuwa na mashaka kuhusu Pontio Pilato na Lisania. Lakini wachambuzi hao walikuwa haraka kufanya uchambuzi wao. Maandishi ya zamani yenye kuwa na majina ya watawala hao wawili yalivumbuliwa, na yalionyesha kwamba Luka alisema kweli. *

SABABU GANI HABARI HII NI YA MAANA?

Yesu alifundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu, serikali yenye itatawala dunia yote

Kujua kwamba Yesu aliishi duniani ao hapana ni jambo la maana kwa sababu mafundisho yake ni ya maana. Kwa mufano, Yesu alifundisha watu namna ya kuwa na maisha mazuri na yenye furaha. * Tena, aliahidi wakati wenye watu watakuwa na amani na usalama wa kweli, na kuishi kwa umoja chini ya serikali moja yenye kuitwa “Ufalme wa Mungu.”—Luka 4:43.

Maneno “Ufalme wa Mungu” ni yenye kufaa kwa sababu kupitia serikali hiyo Mungu atatawala juu ya dunia yote. (Ufunuo 11:15) Yesu alionyesha wazi jambo hilo wakati alisema hivi katika sala yake ya mufano: “Baba yetu uliye mbinguni, . . . Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani.” (Mathayo 6:9, 10) Ufalme wa Mungu utaletea wanadamu faida gani? Tufikirie ahadi zenye kufuata:

  • Vita na kutoelewana kati ya watu vitaisha.Zaburi 46:8-11.

  • Mambo mabaya, kutia ndani pupa na rushwa (ao, kata-midomo), yataisha milele, pamoja na watu wabaya.Zaburi 37:10, 11.

  • Raia wa Ufalme watakuwa na kazi ya muzuri na yenye kufurahisha.Isaya 65:21, 22.

  • Dunia itarudilia hali yake ya kwanza na itazaa chakula kwa uwingi.Zaburi 72:16; Isaya 11:9.

Watu fulani wanaweza kufikiri kwamba ahadi hizo ni ndoto tu. Lakini hauone kama ni ndoto kutumainia nguvu za wanadamu? Fikiria jambo hili: Hata kama kumekuwa maendeleo sana katika mambo ya elimu, sayansi, na teknolojia, mamilioni ya watu leo hawana usalama kabisa na wako na wasiwasi juu ya wakati wenye kuja. Na kila siku tunaona matendo ya kuoneana katika mambo ya feza, siasa, dini, na tunaona pia pupa na rushwa katika mambo yenye watu wanafanya. Kwa kweli, utawala wa mwanadamu umeshindwa kabisa!—Mhubiri 8:9.

Ndiyo sababu, kujua kwamba Yesu aliishi duniani ao hapana ni jambo lenye tunapaswa kufikiria sana. * Kama vile andiko la 2 Wakorintho 1:19, 20 linaonyesha: “Hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia [ya Kristo].”

^ fu. 23 Maandishi yenye kuwa na jina la tetraki, ao ‘mutawala wa wilaya’ mwenye kuitwa Lisania, yalivumbuliwa. (Luka 3:1) Alitawala Abilene katika kipindi chenye Luka anaonyesha.

^ fu. 25 Mufano muzuri wa mafundisho ya Yesu unapatikana katika Mathayo sura ya 5 mupaka 7; mara nyingi mafundisho hayo yanaitwa Mahubiri ya Mulimani.

^ fu. 32 Ili kupata habari zaidi juu ya Yesu na mafundisho yake, fungua adresi yetu ya www.pr418.com/sw na ufungue kichwa MAFUNDISHO YA BIBLIA > MAJIBU YA MASWALI YA BIBLIA.