Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jina la kibinafsi la Mungu katika herufi za Kiebrania cha kale linapatikana mara nyingi sana kwenye hati za zamani za Biblia

MAONI YA BIBLIA

Jina la Mungu

Jina la Mungu

Mamilioni ya watu humwita Mungu kwa kutumia majina ya cheo kama vile Bwana, Mfalme wa Milele, Allah, au Mungu tu. Hata hivyo, Mungu ana jina lake binafsi. Je, unapaswa kulitumia?

Mungu anaitwa nani?

WATU FULANI HUSEMA NINI?

 

Wengi wanaodai kuwa Wakristo wanaamini jina la Mungu ni Yesu. Wengine wanasema kwamba kwa kuwa kuna Mungu Mweza-Yote mmoja tu, hakuna haja ya kutumia jina lake binafsi. Na kuna wengine wanaosema haifai kutumia jina la Mungu.

BIBLIA INASEMA NINI?

 

Jina la Mungu si Yesu, kwa kuwa Yesu si Mungu Mweza-Yote. Kwa kweli, Yesu aliwafundisha waabudu wenzake wasali kwa Mungu wakisema: “Baba, jina lako na litakaswe.” (Luka 11:2) Yesu mwenyewe alisali kwa Mungu akisema: “Baba, litukuze jina lako.”—Yohana 12:28.

Katika Biblia Mungu alitangaza hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu; nami sitampa mwingine yeyote utukufu wangu mwenyewe.” (Isaya 42:8) “Yehova” ni tafsiri ya Kiswahili ya konsonanti nne za Kiebrania, YHWH, zinazowakilisha jina la Mungu. Jina hilo linapatikana mara 7,000 hivi katika Maandiko ya Kiebrania yanayofahamika pia kama Agano la Kale. * Limetumiwa mara nyingi zaidi kuliko jina lolote la cheo, kama vile, “Mungu,” “Mweza-Yote,” au “Bwana,” na kuliko jina lingine lolote kama Abrahamu, Musa, au Daudi.

Hakuna sehemu yoyote katika Biblia ambapo Yehova anakataza kutumia jina lake kwa heshima. Badala yake, Maandiko yanaonyesha jina la Mungu lilitumiwa kwa uhuru na watumishi wake. Walilihusisha katika majina waliyowapa watoto wao, kama vile Eliya, linalomaanisha “Mungu Wangu Ni Yehova,” na Zekaria, linalomaanisha “Yehova Amekumbuka.” Vilevile hawakusita kutumia jina la Mungu katika mazungumzo yao ya kila siku.—Ruthu 2:4.

Mungu anataka tutumie jina lake. Tunahimizwa hivi: “Mshukuruni Yehova, liitieni jina lake.” (Zaburi 105:1) Kwa kuongezea, Yeye huwakazia uangalifu wale “wanaolifikiria jina lake.”—Malaki 3:16.

“Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” —Zaburi 83:18.

Jina la Mungu linamaanisha nini?

Baadhi ya wasomi wanaamini kwamba katika Kiebrania jina Yehova linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Ufafanuzi huo unaonyesha Mungu anaweza kujisababisha kuwa chochote au kusababisha uumbaji wake uwe chochote kinachohitajika ili kutimiza kusudi lake. Ni Muumba mweza-yote pekee anayestahili jina hilo.

HILO LINA MAANA GANI KWAKO?

 

Kujua jina la Mungu kutabadili maoni yako kumhusu. Itakuwa rahisi kwako kumkaribia. Kwa kweli, huwezi kuwa karibu na mtu ambaye hujui jina lake, sivyo? Kwa kuongezea, wazo tu la kwamba Mungu amekujulisha jina lake, linaonyesha kwamba anataka umkaribie.—Yakobo 4:8.

Unaweza kuwa na uhakika kwamba sikuzote Yehova atatenda kupatana na jina lake, akiwa Mungu ambaye mara zote hutimiza ahadi zake. Ndiyo maana Biblia inasema: “Wale wanaolijua jina lako watakutegemea.” (Zaburi 9:10) Utamtegemea zaidi kadiri unavyojifunza kwamba jina lake Yehova linahusiana moja kwa moja na sifa zake, kama vile upendo mshikamanifu, rehema, huruma, na haki. (Kutoka 34:5-7) Inatia moyo sana kujua kwamba sikuzote Yehova hutimiza ahadi zake, na kamwe hawezi kutenda kinyume na sifa zake.

Kwa kweli, ni pendeleo kujua jina la Mungu Mweza-Yote. Ujuzi huo utakuwezesha kupata baraka sasa na wakati ujao. Mungu anaahidi hivi: “Nitamlinda kwa sababu amelijua jina langu.”—Zaburi 91:14.

“Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokoka.”—Yoeli 2:32.

Jina la Mungu katika lugha mbalimbali

^ fu. 9 Tafsiri nyingi za Biblia zimeondoa jina la Mungu na badala yake kutumia jina la cheo “BWANA” kwa herufi kubwa, ilhali nyingine zimetaja jina la Mungu katika mistari michache tu au katika maelezo ya chini. Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imetumia jina la Mungu mara nyingi katika maandiko yote.