Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mawasiliano ni daraja linalokuunganisha na watoto wako

KWA WAZAZI

5: Mawasiliano

5: Mawasiliano

MAANA YAKE

Unaweza kusema una mawasiliano ya kweli na watoto wako ikiwa mnaelezana kwa uhuru mawazo na hisia zenu.

KWA NINI NI MUHIMU

Mara nyingi si rahisi kwa wazazi kuwasiliana na watoto wao hasa wanapofikia umri wa ujana. Huenda miaka michache iliyopita ilikuwa rahisi kwako kufungua mlango na kuingia kwenye moyo wa mtoto wako. Lakini sasa, ni kana kwamba umesimama nje ukisubiri mlango ufunguliwe. Nyakati nyingine, hata ugonge mara nyingi kadiri gani, haufunguliwi. Ingawa huenda ikaonekana watoto hawataki kuzungumza, ukweli ni kwamba huo ndio wakati ambapo wanahitaji kuwasiliana na wazazi wao zaidi!

MAMBO YA KUFANYA

Uwe tayari kuzungumza na mtoto wako muda wowote anapokuhitaji. Zungumza naye hata ikiwa ni usiku sana.

“Huenda ukatamani kumwambia, ‘Yaani unataka tuongee muda huu? Tulikuwa wote siku nzima!’ Lakini kwa nini ulalamike ikiwa mtoto wako anataka kukufungulia moyo wake? Hilo ndilo jambo ambalo kila mzazi anatamani, sivyo?”—Lisa.

“Ingawa ninapenda kulala mapema, kati ya mazungumzo mazuri zaidi ambayo nimekuwa nayo na vijana wangu yalifanyika usiku sana.”—Herbert.

KANUNI YA BIBLIA: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.”—1 Wakorintho 10:24.

Usijiruhusu kukengeuka. Baba mmoja anakiri hivi: “Nyakati nyingine mimi hujikuta nikifikiria mambo mengine watoto wangu wanapozungumza nami. Na wao hutambua kwamba siwasikilizi!”

Ikiwa umewahi kuwa katika hali hiyo, zima televisheni na uweke pembeni simu au kifaa kingine chochote. Kazia fikira kile ambacho mtoto wako anasema, na uone jambo linalomhangaisha kuwa linahitaji usikivu wa makini hata ikiwa linaonekana kuwa dogo.

“Tunapaswa kuwahakikishia watoto wetu kwamba tunathamini hisia zao. Ikiwa wanahisi hatuwajali, hawatatuambia mambo yanayowahangaisha au watatafuta msaada mahali pengine.”—Maranda.

“Tenda kwa utulivu hata ikiwa maoni ya mtoto wako si sahihi kabisa.”—Anthony.

KANUNI YA BIBLIA: “Kazieni uangalifu jinsi mnavyosikiliza.”—Luka 8:18.

Tumia vizuri fursa zisizo rasmi. Nyakati nyingine watoto huwa huru kufungua mioyo yao kwa wazazi, wanapokuwa hawatazamani nao.

“Sisi huzungumza tunapokuwa kwenye gari. Kuzungumza tukiwa tumetazama upande uleule hufanya tuwe na mazungumzo mazuri zaidi kuliko ikiwa tunatazamana.”—Nicole.

Muda wa chakula hutokeza fursa nyingine ya mazungumzo yasiyo rasmi.

“Wakati wa chakula cha jioni, kila mmoja wetu husimulia jambo baya zaidi na zuri zaidi alilopata siku hiyo. Zoea hili hutuunganisha na kufanya kila mmoja ajue kwamba tuko tayari kutegemezana katika matatizo tunayokabili.”—Robin.

KANUNI YA BIBLIA: “[Uwe] mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema.”—Yakobo 1:19.