Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nidhamu humwongoza mtoto kama ambavyo usukani huisaidia boti ipite mahali panapotakiwa

KWA WAZAZI

6: Nidhamu

6: Nidhamu

MAANA YAKE

Neno nidhamu linamaanisha kuongoza au kufundisha. Nyakati fulani, hiyo inatia ndani kurekebisha tabia ya mtoto ambayo si nzuri. Hata hivyo, mara nyingi nidhamu huhusisha kumzoeza mtoto kuwa na maadili ambayo yatamsaidia kutenda kwa hekima bila kuhitaji kurekebishwa baadaye.

KWA NINI NI MUHIMU

Katika miaka ya hivi karibuni, wazazi wengi wameacha kuwatia nidhamu watoto wao, wakihofia kwamba kuwatia nidhamu kutafanya wasijiamini. Hata hivyo, wazazi wenye busara huweka sheria ambazo si zenye kubana sana na kuwazoeza watoto wao kuzifuata.

“Watoto wanahitaji kuwekewa mipaka itakayowasaidia kuwa na sifa zinazohitajika watakapokuwa watu wazima. Bila nidhamu, watoto watakuwa kama meli ambayo haina usukani—itapoteza mwelekeo au hata kuzama.”—Pamela.

MAMBO YA KUFANYA

Uwe na msimamo. Mtoto asipofuata sheria ulizoweka, mwadhibu. Kwa upande mwingine, mpongeze kutoka moyoni anapotii.

“Mimi huwapongeza watoto wangu kwa kuwa watiifu katika ulimwengu huu ambao sifa hiyo ni adimu sana. Kuwapongeza hufanya iwe rahisi kwao kukubali kurekebishwa inapohitajika.”—Christine.

KANUNI YA BIBLIA: “Lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.”—Wagalatia 6:7.

Uwe na usawaziko. Unapomrekebisha mtoto wako, fikiria umri, uwezo wake, na uzito wa kosa alilofanya. Adhabu inayotolewa huwa na matokeo mazuri ikiwa inahusiana na kosa lililofanywa. Kwa mfano, adhabu ya kutumia vibaya simu inaweza kuwa kumwekea mtoto mipaka katika matumizi ya simu kwa kipindi fulani. Wakati huohuo, epuka kufanya makosa madogo yaonekane kuwa makubwa mno.

“Mimi hujitahidi kutambua ikiwa mtoto amefanya kosa kwa makusudi au bila kukusudia. Kuna tofauti kati ya tabia mbaya inayohitaji kurekebishwa na kisa ambacho mtoto anahitaji kuonyeshwa tu amekosea.”—Wendell.

KANUNI YA BIBLIA: “Msiwachokoze watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”—Wakolosai 3:21; maelezo ya chini.

Onyesha upendo. Watoto huitikia na kukubali nidhamu kwa urahisi zaidi wanapojua kwamba mzazi anawarekebisha kwa sababu anawapenda.

“Mwana wetu alipofanya makosa, tulimhakikishia kwamba tulipendezwa na maamuzi yote mazuri aliyofanya awali. Tulimweleza kwamba kosa alilofanya halitaharibu sifa nzuri alizokuwa nazo iwapo tu atajirekebisha na kwamba tulikuwa tayari kumsaidia.”—Daniel.

KANUNI YA BIBLIA: “Upendo ni wenye subira na fadhili.”—1 Wakorintho 13:4.