Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 1

Faida za Sifa ya Kujidhibiti

Faida za Sifa ya Kujidhibiti

NI NINI MAANA YA KUJIDHIBITI?

Kujidhibiti kunatia ndani kuwa na uwezo wa

  • kuzuia tamaa

  • kuzuia hisia

  • kutimiza kazi zisizovutia

  • kuwatanguliza wengine

KWA NINI NI MUHIMU KUWA NA SIFA YA KUJIDHIBITI?

Watoto walio na sifa ya kujidhibiti wanaweza kushinda vishawishi hata ikiwa vinaonekana kuwa vinavutia sana. Kwa upande mwingine, watoto wasiojidhibiti wana mwelekeo wa

  • kuwa wakali

  • kushuka moyo

  • kuvuta sigara au kutumia dawa za kulevya au kunywa pombe kupita kiasi

  • kuwa na mazoea mabaya ya kula

Utafiti mmoja ulifunua kwamba watoto waliozoezwa kujidhibiti, wanapokuwa watu wazima, si rahisi kwao kupata matatizo ya afya na changamoto za kiuchumi, na wana mwelekeo wa kutii sheria. Utafiti huo ulimchochea Profesa Angela Duckworth wa Chuo Kikuu cha Pennsylvania kusema: “Inaonekana hamna kitu kama kujidhibiti ‘kupita kiasi.’”

JINSI YA KUWAFUNDISHA WATOTO KUJIDHIBITI

Jifunze kukataa bila kulegeza msimamo.

KANUNI YA BIBLIA: “Acheni ‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo.”​—Mathayo 5:37.

Mzazi anapokataa jambo, mtoto anaweza kupima msimamo wa mzazi kwa kujifanya amekasirika na kujitupatupa hata mbele ya watu. Mzazi akilegeza msimamo wake, mtoto anatambua kwamba kutumia mbinu hiyo hufanya apate anachotaka hata ikiwa mwanzoni alikataliwa.

Kwa upande mwingine, mzazi akikataa jambo na akashikamana na alichosema, mtoto atajifunza kwamba nyakati fulani hatuwezi kupata kila kitu tunachotaka​—somo muhimu litakalomsaidia maishani. Dakt. David Walsh anasema hivi: “Inashangaza kwamba watu ambao wamejifunza somo hilo ndio wenye shangwe zaidi. Hatuwasaidii watoto wetu kwa vyovyote vile tunapowafanya wafikiri kwamba siku zote watapata kila kitu wanachotaka.” *

Kumkatalia au kumnyima mtoto wako baadhi ya vitu sasa, kutamsaidia awe na uwezo wa kukataa mambo mengine baadaye. Kwa mfano, hata akishawishiwa kutumia dawa za kulevya, kufanya ngono kabla ya ndoa, au kujihusisha na mazoea mengine yasiyofaa, ataweza kukataa.

Msaidie mtoto wako kujua matokeo ya matendo yake, iwe ni mazuri au mabaya.

KANUNI YA BIBLIA: “Lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.”​—Wagalatia 6:7.

Mtoto wako anapaswa kujua kwamba matendo huambatana na matokeo, hivyo asipojidhibiti atapata madhara. Kwa mfano, ikiwa mtoto wako hushindwa kudhibiti hasira yake anapokosewa, wengine watamwepuka. Kwa upande mwingine, ikiwa atasitawisha uwezo wa kuzuia hisia zake au kuwa na subira badala ya kuingilia mambo haraka-haraka, watu watavutiwa naye. Msaidie mtoto wako kuelewa kwamba maisha yatamwendea vizuri akiwa na sifa ya kujidhibiti.

Mfundishe mtoto wako kujua mambo anayopaswa kutanguliza.

KANUNI YA BIBLIA: “Mhakikishe mambo muhimu zaidi.”​—Wafilipi 1:10.

Kujidhibiti si suala tu la kujizuia kufanya mambo mabaya, bali sifa hiyo inatia ndani kujisukuma ili kutimiza mambo yaliyo muhimu hata ikiwa mambo hayo hayatufurahishi. Ni muhimu mtoto wako ajifunze kutambua mambo muhimu na kuyatanguliza. Mzoeze kufanya mambo ya muhimu kwanza kabla ya mambo mengine. Kwa mfano, anapaswa kufanya kazi za shule kabla ya kwenda kucheza.

Weka kielelezo kizuri.

KANUNI YA BIBLIA: “Nimewawekea kielelezo, ili mfanye kama nilivyowafanyia.”​—Yohana 13:15.

Bila shaka mtoto wako ataona jinsi unavyotenda unapokasirishwa au kuudhika. Onyesha kupitia matendo yako kwamba tunapojidhibiti matokeo huwa mazuri. Kwa mfano, mtoto wako akifanya jambo baya, je, wewe hulipuka kwa hasira au huwa unabaki mtulivu?

^ fu. 20 Maelezo hayo yametolewa kwenye kitabu, No: Why Kids​of All Ages​Need to Hear It and Ways Parents Can Say It.