Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Teknolojia Inaathirije Uwezo Wako wa Kujifunza?

Teknolojia Inaathirije Uwezo Wako wa Kujifunza?

Kila siku watu hujifunza mambo mapya​—iwe ni shuleni, kazini au kwa sababu nyingine. Teknolojia inaweza kutusaidia. Leo, ni rahisi kupata taarifa bila hata kuondoka nyumbani wala kuinuka kwenye kiti chako.

Hata hivyo, watu wengi wanaotumia teknolojia kupita kiasi wametambua kwamba . . .

  • si rahisi kukaza fikira wanaposoma.

  • si rahisi kufanya jambo moja bila kukengeushwa.

  • wanachoka upesi wanapokuwa peke yao.

UNACHOPASWA KUJUA

KUSOMA

Baadhi ya watu wanaotumia vifaa vyao vya kielektroni kupita kiasi hawawezi kusoma kwa makini kitabu au makala fulani na kuimaliza yote, badala yake wanapitia juujuu ili kupata mambo makuu.

Unaweza kupitia kitabu au makala kijuu-juu ikiwa unahitaji kupata jibu la swali fulani haraka. Lakini, kufanya hivyo kutapunguza uwezo wako wa kujifunza mambo kwa kina.

JAMBO LA KUFIKIRIA: Je, unaweza kusoma vifungu virefu vya maneno bila kuchoka? Kusoma kwa makini kunaweza kukusaidiaje kujifunza mambo kwa kina?​—METHALI 18:15.

KUKAZA FIKIRA

Baadhi ya watu wanahisi kwamba teknolojia inawapa uwezo wa kufanya mambo mawili kwa wakati mmoja​—kwa mfano, wanaweza kutuma ujumbe huku wakiwa wanasoma. Lakini wanakengeushwa na mwishowe wanashindwa kufanya jambo lolote vizuri, hasa ikiwa mambo yote mawili yanahitaji kufanywa kwa umakini.

Unahitaji kujidhibiti ili ukazie fikira jambo unalofanya, lakini kuna faida kubwa ya kufanya hivyo. Msichana anayeitwa Grace anasema hivi: “Utafanya makosa machache na hutakuwa na mkazo mwingi. Nimejifunza kwamba ni bora kufanya kazi moja kwa makini kuliko kukengeushwa kwa kufanya kazi nyingi kwa wakati mmoja.”

JAMBO LA KUFIKIRIA: Je, kufanya mambo mengi kwa wakati mmoja kunakuzuia usikazie fikira jambo unalojifunza au hata kulisahau kabisa?​—METHALI 17:24.

UNAPOKUWA PEKE YAKO

Baadhi ya watu hawapendi kuwa peke yao, hivyo wanatumia teknolojia zaidi ili wasiwe wapweke. Mwanamke anayeitwa Olivia anakiri hivi: “Ninachoka ninapokaa kwa dakika 15 tu bila kuangalia simu, kifaa cha kielektroni (tablet), au kuangalia TV.”

Hata hivyo, kipindi cha kuwa peke yako ni muhimu sana ili ufikirie mambo kwa kina​—hilo ni muhimu kwa watoto na watu wazima hasa wanapotaka kujifunza jambo fulani.

JAMBO LA KUFIKIRIA: Je, unaweza kutumia vizuri wakati wa kuwa peke yako ili ujifunze jambo fulani?​—1 TIMOTHEO 4:15.

UNACHOWEZA KUFANYA

CHUNGUZA JINSI UNAVYOTUMIA TEKNOLOJIA

Ni kwa njia gani unaweza kutumia teknolojia kuboresha uwezo wako wa kujifunza? Teknolojia inaweza kukuzuiaje usikaze fikira na kujifunza kikamili?

KANUNI YA BIBLIA: “Ilinde hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.”​—METHALI 3:21.