Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 5

Maisha ya Taabu Yanaanza

Maisha ya Taabu Yanaanza

NJE ya bustani ya Edeni, Adamu na Hawa walipata taabu nyingi. Iliwapasa kufanya kazi kwa bidii wajipatie chakula. Mahali pa miti mizuri ya matunda, waliona miiba mingi inamea kuwazunguka. Ndivyo ilivyokuwa Adamu na Hawa walipokataa kumtii Mungu, wasiwe tena rafiki zake.

Zaidi ya hayo, Adamu na Hawa walianza kufa. Kumbuka, Mungu aliwaonya hivyo, ikiwa wangekula tunda la mti fulani. Walianza kufa siku ile ile waliyokula. Walikuwa wapumbavu sana kukataa kumsikiliza Mungu!

Watoto wote wa Adamu na Hawa walizaliwa Mungu akisha kuwafukuza wazazi wao katika bustani ya Edeni. Kwa hiyo, watoto pia wangezeeka na kufa.

Kama Adamu na Hawa wangemtii Yehova, wao na watoto wangekaa kwa furaha. Wote wangeweza kukaa duniani milele kwa furaha. Hakuna ambaye angezeeka, awe mgonjwa na kufa.

Mungu anataka watu wakae milele kwa furaha, Naye anaahidi kwamba siku moja watakaa hivyo. Dunia nzima itakuwa nzuri, hata watu wote watakuwa wenye afya. Kila mtu duniani atakuwa rafiki mzuri wa kila mtu mwingine na Mungu.

Lakini Hawa hakuwa tena rafiki ya Mungu. Haikuwa rahisi kwake kuzaa watoto wake. Alipata maumivu. Kukataa kumtii Yehova kulimetea huzuni nyingi, sivyo?

Adamu na Hawa wakazaa wana na binti wengi. Mwana wao wa kwanza alipozaliwa, walimwita jina Kaini. Walimwita mwana wao wa pili Habili. Walipatwa na nini? Unajua?