Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 7

Mtu Hodari

Mtu Hodari

WATU walipoanza kuongezeka duniani, wengi wao wakafanya mabaya kama Kaini. Lakini mtu mmoja alikuwa tofauti. Ni huyu anayeitwa Henoko. Henoko alikuwa mtu hodari. Watu wote karibu yake walikuwa wakifanya mabaya, lakini Henoko aliendelea kumtumikia Mungu.

Unajua sababu wakati huo watu walifanya mabaya mengi sana? Kumbuka, Nani alifanya Adamu na Hawa wakatae kumtii Mungu kisha wakala tunda ambalo Mungu aliwakataza? Ni malaika mbaya. Biblia inamwita Shetani. Anataka kumfanya kila mtu awe mbaya.

Siku moja Yehova Mungu alimwagiza Henoko awaambie watu jambo fulani ambalo hawakutaka kulisikia. Ni hili: ‘Siku moja Mungu atawaharibu watu wote wabaya.’ Labda watu hao walikasirika sana kwa kusikia hayo. Labda hata walitaka kumwua Henoko. Hivyo ilimpasa Henoko awe hodari sana ili awaambie watu hao jambo ambalo Mungu alikusudia kufanya.

Mungu hakumwacha Henoko akae muda mrefu kati ya watu hao wabaya. Henoko alikaa miaka 365 tu. Kwa nini twasema “miaka 365 tu?” Kwa sababu watu wa siku hizo walikuwa mwenye nguvu nyingi kuliko watu wa sasa. Nao walikaa muda mrefu zaidi. Methusela mwana wa Henoko alikaa miaka 969!

Basi, Henoko alipokufa, watu walizidi kuwa wabaya sana. Biblia yasema kwamba ‘kila jambo walilowaza lilikuwa baya wakati wote,’ na kwamba ‘dunia ikajaa jeuri.’

Unajua sababu moja kwa nini kulikuwako matata mengi sana duniani siku hizo? Shetani alipata njia mpya ya kufanya watu watende mabaya. Tutajifunza hayo katika hadithi inayofuata.