Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 13

Ibrahimu​—Rafiki ya Mungu

Ibrahimu​—Rafiki ya Mungu

MAHALI pamoja ambapo watu walikaa baada ya Gharika ni Uru. Pakawa mji wa maana wenye nyumba nzuri. Lakini watu wa huko waliabudu miungu ya uongo. Ndivyo walivyofanya hata katika Babeli. Watu wa Uru na Babeli hawakuwa kama Nuhu na Shemu mwanawe, waliozidi kumtumikia Yehova.

Mwishowe, ilipopita miaka 350 tangu gharika, Nuhu mwaminifu akafa. Ilipopita miaka miwili mtu unayemwona katika picha hii alizaliwa. Alikuwa mtu wa pekee sana kwa Mungu. Jina lake ni Ibrahimu. Alikaa pamoja na jamaa yake katika mji huo wa Uru.

Siku moja Yehova alimwambia Ibrahimu (Abrahamu): ‘Ondoka Uru, wewe na ukoo wako, uende kwenye nchi ambayo nitakuonyesha.’ Je! Ibrahimu alimtii Mungu na kuacha starehe zote za Uru? Ndiyo. Ibrahimu alijulikana kuwa rafiki ya Mungu kwa sababu alimtii Mungu sikuzote.

Wengine wa jamaa ya Ibrahimu walimfuata alipoondoka Uru. Tera baba yake alimfuata. Hata Lutu mpwa wake. Na pia Sara mke wa Ibrahimu. Halafu wote wakafika Harani, na huko Tera akafa. Walikuwa mbali sana na Uru.

Muda kidogo Ibrahimu na jamaa yake wakaondoka Harani kuja Kanaani. Yehova akasema: “Hii ndiyo nchi nitakayowapa watoto wako.’ Ibrahimu alikaa Kanaani katika hema.

Mungu alianza kumsaidia Ibrahimu hata akawa na kondoo na wanyama wengine wengi na mamia ya watumishi. Lakini yeye pamoja na Sara hawakuwa na watoto wowote.

Ibrahimu alipokuwa mwenye miaka 99, Yehova alimwahidi hivi: ‘Utakuwa baba ya mataifa mengi.’ Lakini watoto wangezaliwa namna gani, maana Ibrahimu na Sara ni wazee mno?