Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 17

Mapacha Waliokuwa Tofauti

Mapacha Waliokuwa Tofauti

WAVULANA wawili hapa ni tofauti sana, sivyo? Unajua majina yao? Yule mwindaji ni Esau, na yule anayechunga kondoo ni Yakobo.

Esau na Yakobo walikuwa mapacha wa Isaka na Rebeka. Isaka baba yao, alimpenda sana Esau, kwa sababu alikuwa mwindaji mzuri naye aliiletea jamaa chakula. Lakini Rebeka alimpenda sana Yakobo, kwa sababu alikuwa mtulivu, mwenye amani.

Ibrahimu babu yao alikuwa bado hai. Tunaweza kuwaza namna Yakobo alivyopenda kumsikiliza akisema habari za Yehova. Mwishowe Ibrahimu akafa akiwa mwenye miaka 175, mapacha hao walipokuwa wenye miaka 15.

Esau alipokuwa mwenye miaka 40 alioa wanawake wawili kutoka nchi ya Kanaani. Hilo lilihuzunisha sana Isaka na Rebeka kwa sababu wanawake hao hawakumwabudu Yehova.

Ikawa siku moja Esau akamkasirikia sana Yakobo ndugu yake. Ulifika wakati Isaka alipotaka kumbariki mwanawe mkubwa. Kwa kuwa alikuwa mkubwa kuliko Yakobo, Esau alitazamia kupokea baraka hiyo. Lakini Esau alikuwa amekwisha kumwuzia Yakobo haki hiyo ya kupokea baraka. Pia, wavulana hao wawili walipozaliwa Mungu alikuwa amesema kwamba Yakobo angepokea baraka hiyo. Na ndivyo ilivyokuwa. Isaka alimpa Yakobo mwanawe baraka hiyo.

Baadaye, Esau alipojua hivyo akamkasirikia sana Yakobo. Alikasirika sana hata akasema angemwua Yakobo. Rebeka aliposikia hayo, alisumbuka sana. Basi akamwambia Isaka mume wake hivi: ‘ltakuwa vibaya sana ikiwa Yakobo pia anaoa mwanamke Mkanaani.’

Kisha Isaka akamwita Yakobo mwanawe akamwambia hivi: ‘Usioe mwanamke wa kutoka Kanaani. Nenda kwenye nyumba ya babu yako Betueli katika Harani. Oa mmoja wa binti za Labani mwanawe.’

Yakobo akamsikiliza baba yake, na mara hiyo akaanza safari yake ndefu kwenda kwa watu wake wa ukoo huko Harani.