Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 23

Ndoto za Farao

Ndoto za Farao

MIAKA miwili inapita, Yusufu angali gerezani. Mnyweshaji hamkumbuki. Ndipo usiku mmoja Farao anaota ndoto mbili za pekee sana, naye hajui maana yazo. Unamwona akilala pale? Kesho yake Farao anawaita wenye akili na kuwaambia mambo ambayo ameota. Lakini hawawezi kumwambia maana ya ndoto zake.

Mwishowe yule mnyweshaji anakumbuka Yusufu. Anamwambia Farao hivi: ‘Nilipokuwa gerezani alikuwako mtu huko aliyeweza kuniambia maana ya ndoto.’ Farao anaagiza Yusufu atolewe gerezani mara moja.

Farao anamsimulia Yusufu ndoto zake hivi: ‘Niliona ng’ombe saba wanono na wazuri. Kisha nikawaona ng’ombe saba waliokonda sana. Na wale waliokonda wakawala ng’ombe wanono.’

‘Katika ndoto yangu ya pili niliona masuke saba yenye kujaa nafaka zilizoiva, yakikua katika bua moja. Kisha nikaona masuke saba membamba, yaliyokauka sana ya nafaka. Na yale masuke membamba ya nafaka yalianza kumeza masuke mazuri saba ya nafaka.

Yusufu anamwambia Farao hivi: ‘Maana ya ndoto zile mbili ni moja. Wale ng’ombe saba wanono na masuke saba ya nafaka yenye kujaa ni miaka saba, na wale ng’ombe saba waliokonda na masuke ya nafaka membamba saba ni miaka mingine saba. Kutakuwako miaka saba ya chakula kingi katika Misri. Kisha itakuwako miaka saba ya chakula kidogo sana.’

Basi Yusufu anamwambia Farao hivi: ‘Mchague mtu mwenye akili awe msimamizi wa kukusanya chakula wakati wa miaka mizuri saba. Hapo watu hawatakufa njaa wakati wa miaka mibaya saba inayofuata ya chakula kidogo.’

Farao anapenda wazo hilo. Anamchagua Yusufu akusanye chakula, na kukiweka akiba. Yusufu anakuwa mkuu katika misri, wa pili kwa Farao.

Miaka minane baadaye, wakati wa njaa kuu hiyo, Yusufu anaona watu fulani wakija. Unawajua? Ala, ni ndugu zake wakubwa 10! Yakobo baba yao amewatuma Misri kwa sababu chakula ni kidogo kule Kanaani. Yusufu anawajua ndugu zake, lakini wao hawamjui. Unajua sababu? Yusufu amekuwa mkuu, amevaa mavazi ya pekee.

Yusufu anakumbuka kwamba alipokuwa mvulana aliota ndoto akiona ndugu zake wakija kumpigia magoti. Unakumbuka ulisoma habari hiyo? Hivyo Yusufu anafahamu kwamba ni Mungu aliyemtuma aende Misri, kwa sababu nzuri. Unadhani Yusufu anafanya nini? Na tuone.