Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 26

Ayubu ni Mwaminifu kwa Mungu

Ayubu ni Mwaminifu kwa Mungu

UNAMSIKITIKIA mgonjwa huyu? Anaitwa Ayubu (Yobu). Mwanamke huyu ni mke wake. Unajua anamwambia Ayubu nini? ‘Mtukane Mungu ufe.’ Tuone sababu anasema hivyo, na sababu Ayubu aliteswa sana.

Ayubu alimwamini na kumtii Yehova. Alikaa katika nchi ya Usi, karibu na Kanaani. Yehova alipenda Ayubu sana. Lakini mtu mmoja alimchukia. Unamjua?

Ni Shetani Ibilisi. Kumbuka, Shetani ni yule malaika mbaya anayemchukia Yehova. Alishawishi Adamu na Hawa wasitii Yehova. Alifikiri anaweza pia kushawishi kila mtu asitii Yehova. Je! aliweza? Hapana. Wafikirie wanaume na wanawake wengi waaminifu ambao tumejifunza habari zao. Unaweza kutaja majina ya wangapi?

Yakobo na Yusufu wakisha kufa huko Misri, Ayubu akawa ndiye mtu mwaminifu sana kwa Yehova katika dunia yote. Yehova alitaka kujulisha Shetani kwamba hawezi kushawishi kila mtu afanye mabaya. Akasema hivi: ‘Tazama Ayubu. Ni mwaminifu sana kwangu.’

Shetani akapinga hivi: ‘Ni mwaminifu kwa sababu unambariki tena ana vitu vizuri vingi. Lakini ukivichukua, atakutukana.’

Yehova akasema: ‘Haya, vichukue. Mfanyie Ayubu mambo yote mabaya. Tutaona kama atanitukana. Lakini usimwue.’

Kwanza, Shetani akaongoza watu waibe ng’ombe za Ayubu na ngamia, na kondoo zake zikauawa. Akaua wana 10 na binti zake katika upepo mkali. Kisha, Shetani akapiga Ayubu kwa ugonjwa huo mbaya sana. Ayubu aliteswa sana. Ndiyo sababu mke wake alimwambia: ‘Mtukane Mungu ufe.’ Ayubu hakufanya hivyo. Rafiki watatu wa uongo wakaja kumwambia ana maisha mabaya. Lakini Ayubu aliendelea kuwa mwaminifu.

Yehova alifurahi sana na kumbariki Ayubu, kama unavyoona katika picha hii. Alimponya ugonjwa wake. Ayubu akawa na watoto wengine wazuri 10, ng’ombe, kondoo na ngamia wengi mara mbili kuliko zamani.

Je! utakuwa mwaminifu kwa Yehova sikuzote kama Ayubu? Ukiwa hivyo, Mungu atakubariki wewe pia. Utakaa milele wakati dunia yote itafanywa nzuri sana kama bustani ya Edeni.