Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 30

Mti Mdogo Unaowaka

Mti Mdogo Unaowaka

MUSA alikuwa amekwenda mpaka kwenye Mlima wa Horebu ili atafute majani ya kondoo zake. Akaona mti mdogo ukiwaka moto, lakini haukuteketea!

‘Hii ni ajabu,’ Musa akawaza. ‘Nitakaribia zaidi nione vizuri.’ Alipokaribia, sauti ikatoka katika mti huo mdogo ikisema: ‘Usije karibu zaidi. Ondoa viatu vyako, kwa sababu unasimama mahali patakatifu.’ Mungu alikuwa akisema kupitia kwa malaika, hivyo Musa akafunika uso wake.

Kisha Mungu akasema: ‘Nimeyaona mateso ya watu wangu huko Misri. Basi nitawaokoa, nami nanakutuma wewe ukawatoe watu wangu Misri.’ Yehova alikusudia kuwapeleka watu wake kwenye nchi nzuri ya Kanaani.

Lakini Musa akasema: ‘Mimi ni mtu tu. Nifanyeje hivyo? Nikienda nao Waisraeli wataniuliza, “Nani aliyekutuma?” Nitasema nini?’

‘Utasema hivi,’ Mungu akajibu. ‘“YEHOVA Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakoo amenituma kwenu.”’ Yehova akaongezea: ‘Hilo ndilo jina langu milele.’

‘Lakini kama hawaniamini nikisema umenituma, hapo itakuwaje,’ Musa akajibu.

‘Nini hicho mkononi mwako?’ Mungu akauliza.

Musa akajibu: ‘Fimbo.’

‘Itupe chini,’ Mungu akasema. Musa alipoitupa chini, fimbo ikawa nyoka. Kisha Yehova akamwonyesha Musa muujiza mwingine. Akasema: ‘Ingiza mkono wako katika vazi lako.’ Musa akaingiza, na alipoutoa mkono wake, ulikuwa mweupe kama theluji! Mkono huo ulikuwa kama umepatwa na ugonjwa mbaya unaoitwa ukoma. Kisha Yehova akampa Musa uwezo wa kufanya mwujiza wa tatu. Halafu akamwambia hivi: ‘Utakapofanya miujiza hii Waisraeli wataamini kwamba nimekutuma.’

Baada ya hayo Musa akaenda nyumbani na kumwambia Yethro hivi: ‘Tafadhali uniruhusu nirudi kwa watu wangu huko Misri nione wa hali gani.’ Basi Yethro akamwambia Musa, kwa heri, naye Musa akaanza safari ya kurudi Misri.