Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 35

Yehova Anatoa Sheria Zake

Yehova Anatoa Sheria Zake

KARIBU miezi miwili baada ya Waisraeli kuondoka Misri, wanakuja kwenye Mlima Sinai unaoitwa pia Horebu. Ni pale pale ambapo Yehova alisema na Musa katika mti mdogo uliowaka moto. Watu wanapiga kambi hapa na kukaa kidogo.

Watu wanapongojea chini, Musa apanda mlima. Katika mlima, Yehova anamwambia Musa kwamba Yeye anataka Waisraeli wamtii na kuwa watu Wake wa pekee. Musa anaposhuka, anawaambia Waisraeli maneno ya Yehova. Watu hao wanasema kwamba watamtii Yehova, kwa sababu wanataka kuwa watu wake.

Sasa Yehova anafanya mwujiza. Anafanya kilele cha mlima kitoke moshi, na kufanyiza ngurumo yenye sauti kubwa. Pia anawaambia watu hivi: ‘Mimi ni Yehova Mungu wenu niliyewatoa Misri.’ Kisha anawaamuru hivi: ‘Usiabudu miungu mingine isipokuwa mimi.’

Mungu anawapa Waisraeli amri nyingine tisa, au sheria. Watu wanaogopa sana. Wanamwambia Musa hivi: ‘Wewe sema na sisi, kwa sababu Mungu akisema na sisi huenda tukafa.’

Baadaye Yehova anamwambia Musa hivi: ‘Njoo kwangu mlimani. Nitakupa mabamba mawili ya mawe ambapo nimeandika sheria ninazotaka watu washike.’ Tena Musa anapanda mlimani. Anakaa huko muda wa siku 40 mchana na usiku.

Mungu ana sheria nyingi nyingi za kuwapa watu. Musa anaziandika sheria hizo. Pia Mungu anampa Musa mabamba mawili ya mawe. Juu ya hayo, Mungu mwenyewe ameandika sheria 10 alizowaambia watu wote. Zinaitwa Amri Kumi.

Amri Kumi ni sheria za maana. Hata sheria nyingine nyingi ambazo Mungu anawapa Waisraeli ni za maana. Moja ya hizo sheria ni hii: ‘Inakupasa umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote, kwa akili zako zote, kwa nafsi yako yote na nguvu zako zote.’ Nyingine ni hii: ‘Inakupasa umpende jirani yako kama unavyojipenda.’ Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, alisema kwamba hizo ndizo sheria mbili zilizo kubwa kuliko zote ambazo Yehova aliwapa watu wake Waisraeli. Baadaye tutajifunza mambo mengi juu ya Mwana wa Mungu na mafundisho yake.