Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 45

Kuvuka Mto Yordani

Kuvuka Mto Yordani

TAZAMA! Waisraeli wanavuka Mto Yordani! Lakini maji yako wapi? Kwa kuwa mvua nyingi zinaanguka wakati huo wa mwaka, mto huo ulijaa maji sana dakika chache zilizotangulia. Lakini sasa maji yamekauka! Waisraeli wanavuka katika nchi kavu kama walivyovuka Bahari Nyekundu! Maji yote hayo yalikwenda wapi? Ebu tuone.

Ulipofika wakati Waisraeli wavuke Mto Yordani, Yehova alikuwa amemwagiza Yoshua awaambie watu hivi: ‘Makuhani wabebe sanduku la agano watutangulie. Watakapoweka miguu yao katika maji ya Mto Yordani, maji yatasimama.’

Basi makuhani hao wanachukua sanduku la agano, wakilibeba mbele ya watu. Wanapofika Yordani, makuhani wanaingia moja kwa moja ndani ya maji. Maji yanatembea kwa nguvu sana na Mto una kilindi kirefu sana. Lakini mara miguu yao inapokanyaga maji, maji hayo yanaanza kusimama! Ni mwujiza huo! Upande wa juu wa mto, Yehova amekusanya maji kama ziwa. Kwa muda mfupi mto hautakuwa na maji tena!

Wale makuhani wanaobeba sanduku la agano wanaingia moja kwa moja katikati ya mto mkavu. Unaweza kuwaona katika picha? Wanaposimama humo, Waisraeli wote wanavuka moja kwa moja Mto Yordani katika nchi kavu!

Kila mtu akiisha kuvuka, Yehova anamwagiza Yoshua awaambie wanaume hodari 12 hivi: ‘Ingieni mtoni mahali wanaposimama makuhani walio na sanduku la agano. Chagueni mawe 12, myapange pamoja mahali mtakapolala nyote usiku huu. Kisha, wakati ujao, watoto wenu watakapouliza maana ya mawe hayo, mwambie kwamba maji yalisimama wakati sanduku la agano la Yehova lilipovuka Yordani. Mawe hayo yatawakumbusha mwujiza huo!’ Pia Yoshua anasimamisha mawe 12 mahali walipokuwa wamesimama makuhani katika bonde la mto.

Mwishowe Yoshua anawaambia makuhani wanaolichukua sanduku la agano hivi: ‘Pandeni mtoke Yordani.’ Na mara wanapopanda, mto unaanza kutiririka maji tena.