Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 55

Mvulana Mdogo Anamtumikia Mungu

Mvulana Mdogo Anamtumikia Mungu

JE! HUYU si kivulana mzuri? Jina lake ni Samweli. Na mwanamume anayeweka mkono wake juu ya kichwa cha Samweli ni Eli, kuhani mkuu wa Israeli. Yule ni Elkana, baba ya Samweli, Hana mama yake wanaompeleka Samweli kwa Eli.

Samweli ana miaka minne au mitano tu. Lakini atakaa katika hema ya Yehova pamoja na Eli na makuhani wengine. Kwa nini Elkana na Hana wanamtoa Samweli mtoto amtumikie Yehova hemani? Ebu tuone.

Miaka michache kabla ya hayo, Hana huyo alihuzunika sana. Hakuweza kuzaa mtoto, naye alitaka mtoto sana sana. Basi siku moja Hana alipotembelea hema ya Yehova, alisali hivi: ‘Ee Yehova, usinisahau mimi! Ukinipa mwana, nakuahidi kukupa huyo akutumikie maisha yake yote.’

Yehova akajibu sala ya Hana, na baada ya miezi fulani akamzaa Samweli. Hana akampenda kivulana wake, akaanza kumfundisha habari za Yehova akiwa bado mdogo sana. Akamwambia mumewe hivi: ‘Upesi Samweli akiisha kuacha kunyonya, nitampeleka hemani akamtumikie Yehova huko.’

Ndivyo tunavyoona Hana na Elkana wakifanya katika picha hii. Na kwa vile Samweli amefundishwa vizuri na wazazi wake, anafurahia kumtumikia Yehova katika hema ya Yehova. Kila mwaka Hana na Elkana wanakuja kuabudu katika hema hii ya pekee, na kumtembelea kivulana wao mdogo. Na kila mwaka Hana anamletea Samweli vazi jipya ambalo amemshonea.

Miaka inapita, na Samweli anazidi kutumikia katika hema ya Yehova. Yehova na watu wanampenda. Lakini Hofni na Finehasi, wana wa Eli kuhani mkuu si wazuri. Wanafanya mabaya mengi, wanazuia wengine pia kumtii Yehova. Ingempasa Eli awaondoe katika ukuhani, lakini hawaondoi.

Kijana Samweli hakubali kuacha kumtumikia Yehova kwa sababu ya mabaya yanayoendelea hemani. Lakini kwa vile watu wachache sana ndio wanaompenda Yehova, Yehova ameacha kusema na mwanadamu yeyote. Inakuwa hivi wakati Samweli anapokuwa mkubwa kidogo:

Samweli amelala hemani anapoamshwa na sauti. Anajibu hivi: ‘Mimi hapa.’ Anaamka na kumkimbilia Eli, akisema: ‘Uliniita, nimekuja.’

Lakini Eli anajibu: ‘Sikukuita; nenda kalale.’ Samweli anarudi kulala.

Tena anaitwa mara ya pili: ‘Samweli!’ Samweli anaamka na kumkimbilia Eli tena. ‘Uliniita, nimekuja,’ asema. Lakini Eli anamjibu: ‘Sikukuita, mwanangu. Kalale tena.’ Samueli arudi kulala.

‘Samweli!’ sauti yaita mara ya tatu. Samweli amkimbilia Eli. ‘Nimekuja, maana umeniita sasa,’ anasema. Sasa Eli anajua kwamba ni Yehova anayeita. Amwambia Samweli hivi: ‘Nenda kalale tena, na akiita tena, useme: “Sema, Yehova, maana mtumishi wako anasikiliza.”’

Ndivyo Samweli anasema Yehova anapoita tena. Kisha Yehova amwambia Samweli kwamba ataadhibu Eli na wanawe. Baadaye Hofni na Finehasi wanakufa katika kupigana na Wafilisti, Eli anaposikia yaliyotokea anaanguka, anavunja shingo yake na kufa pia. Neno la Yehova latimia.

Samweli anakuwa mkubwa, na kuwa mwamuzi wa mwisho wa Israeli. Anapozeeka, watu wanamwomba hivi: ‘Chagua mfalme wa kututawala sisi.’ Samweli hataki kufanya hivyo, kwa kuwa Yehova ndiye mfalme wao. Lakini Yehova anamwambia asikilize watu hao.