Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 57

Mungu Anamchagua Daudi

Mungu Anamchagua Daudi

UNAWEZA kuona yaliyotokea? Mvulana huyu amemwokoa mwana-kondoo mdogo asiliwe na dubu. Dubu huyo alikuja akamchukua mwana-kondoo amle. Lakini mvulana huyo akafuatia, akamwokoa mwana-kondoo katika kinywa cha dubu. Dubu aliporukia mvulana, alimkamata na kumwua! Wakati mwingine aliokoa kondoo mmoja asiliwe na simba. Je! huyo si mvulana hodari? Unajua ni nani?

Ni kijana Daudi. Anakaa katika mji wa Bethlehemu. Babu yake ni Obedi, mwana wa Ruthu na Boazi. Unawakumbuka? Baba ya Daudi ni Yese. Daudi anachunga kondoo za baba yake. Daudi alizaliwa miaka 10 baada ya Yehova kuchagua Sauli awe mfalme.

Unafika wakati Yehova anapomwambia Samweli hivi: ‘Chukua mafuta ya pekee uende nyumbani kwa Yese huko Bethlehemu. Nimechagua mmoja kati ya wanawe awe mfalme.’ Samweli anapomwona Eliabu mwana mkubwa wa Yese, anasema hivi: ‘Bila shaka huyu ndiye Yehova amechagua.’ Lakini Yehova anamwambia: ‘Usitazame urefu na uzuri wake. Sikumchagua awe mfalme.’

Basi Yese anamwita Abinadabu mwanawe na kumpeleka kwa Samweli. Lakini Samweli anasema: ‘Hapana, Yehova hakumchagua wala huyu.’ Tena, Yese amleta Shama mwanawe. ‘Hapana, Yehova hakuchagua wala huyu,’ asema Samweli. Yese ampelekea Samweli wanawe saba, lakini Yehova hachagui yeyote kati yao. ‘Je! wavulana ni hawa tu?’ Samweli auliza.

‘Bado kuna mdogo wao,’ Yese asema. ‘Lakini yeye anachunga kondoo.’ Daudi anapoingizwa, Samweli anamwona kuwa kivulana mzuri. ‘Huyu ndiye,’ Yehova asema. ‘Mmwagie mafuta.’ Samweli anafanya hivyo. Utafika wakati Daudi atakapokuwa mfalme wa Israeli.