Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 60

Abigaili na Daudi

Abigaili na Daudi

JE! UNAMJUA mwanamke huyu mzuri anayekuja kumlaki Daudi? Jina lake ni Abigaili. Ni mwenye akili nzuri, naye anamzuia Daudi asifanye ubaya. Lakini kabla ya kujifunza hayo, tuone ni mambo gani yamekuwa yakimpata Daudi.

Daudi akiisha kumkimbia Sauli, anajificha katika pango. Ndugu zake na wengine wa jamaa yake wanajiunga naye huko. Karibu jumla ya watu 400 wanamwendea, Daudi anakuwa kiongozi wao. Kisha Daudi anamwendea mfalme wa Moabu na kusema: ‘Tafadhali ruhusu baba na mama yangu wakae nawe mpaka nione yatakayonipata.’ Baadaye Daudi na watu wake wanaanza kujificha vilimani.

Ni baada ya hayo kwamba Daudi akutana na Abigaili. Nabali mume wake ni mtu tajiri mwenye mashamba. Ana kondoo 3,000 na mbuzi 1,000. Nabali ni mchoyo. Lakini Abigaili mkewe ni mwenye sura nzuri sana. Pia, anajua kutenda mema. Wakati mmoja hata aliokoa jamaa yake. Na tuone ilivyokuwa.

Daudi na watu wake wamemtendea mema Nabali. Wamelinda kondoo zake. Basi siku moja Daudi anatuma watu wake wakamwombe Nabali awasaidie. Watu wa Daudi wanamwendea Nabali wakati yeye na wasaidizi wake wanakata manyoya ya kondoo. Ni siku ya karamu, naye Nabali ana chakula kingi kizuri. Basi watu wa Daudi wanamwambia hivi: ‘Sisi tumekutendea mema. Hatukuiba kondoo wako ye yote, ila tumesaidia kuwachunga. Basi, tafadhali, utupe chakula kidogo.’

‘Siwezi kuwapa chakula watu kama ninyi,’ Nabali anasema. Anasema kwa njia mbaya sana, na kumtukana Daudi. Watu hao wanaporudi na kumwambia Daudi, Daudi anakasirika sana. ‘Jivikeni panga zenu!’ awaambia watu wake. Nao wanaanza safari kwenda kuua Nabali na watu wake.

Mmoja wa watu wa Nabali, waliosikia matusi ya Nabali, anamwambia Abigaili yaliyotokea. Mara hiyo Abigaili anatayarisha chakula. Anakiweka juu ya punda wake, anapokutana na Daudi njiani, ainama na kusema: ‘Tafadhali, bwana, usimwangalie mume wangu yule Nabali. Yeye ni mpumbavu, anafanya mapumbavu. Hii ni zawadi. Tafadhali ichukue, utusamehe yaliyotokea.’

‘Wewe ni mwanamke mwenye akili,’ Daudi ajibu. ‘Umenizuia nisimwue Nabali na kumlipa kwa choyo yake. Basi nenda zako kwa amani.’ Baadaye, Nabali anapokufa, Abigaili anakuwa mke wa Daudi.