Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hadithi ya 63

Sulemani Mfalme Mwenye Akili

Sulemani Mfalme Mwenye Akili

SULEMANI ni kijana anapokuwa mfalme. Anampenda Yehova, na anafuata shauri zuri la Daudi baba yake. Yehova anapendezwa na Sulemani, na usiku mmoja anamwambia katika ndoto hivi: ‘Sulemani (Solomono), ungependa nikupe nini?’

Sulemani ajibu: ‘Yehova Mungu wangu, mimi ni mchanga sana na sijui kutawala. Basi unipe hekima (akili) ya kutawala watu wako vizuri.’

Yehova anapendezwa na ombi la Sulemani. Asema: ‘Kwa sababu umeomba akili wala si maisha marefu wala mali, nitakupa akili nyingi kuliko watu wote. Lakini nitakupa mali na utukufu pia, ingawa hukuomba hivyo.’

Muda mfupi baadaye wanawake wawili wanamfikia Sulemani wakiwa na tatizo gumu. ‘Mwanamke huyu anakaa nami nyumba moja,’ mmoja wao aeleza. ‘Nikazaa mtoto wa kiume, siku mbili baada ya hapo naye akazaa mtoto wa kiume. Ndipo usiku mmoja mtoto wake akafa. Lakini nilipokuwa nimelala, akamweka mtoto wake aliyekufa karibu nami akamchukua mtoto wangu. Nilipoamka na kumtazama mtoto aliyekufa, nikaona si mtoto wangu.’

Ndipo yule mwanamke mwingine anasema: ‘Sivyo! Mtoto aliye hai ndiye wangu, na aliyekufa ndiye mtoto wake!’ Mwanamke wa kwanza naye ajibu hivi: ‘Sivyo! Mtoto aliyekufa ndiye wako, na aliye hai ndiye wangu!’ Wanawake hao wanagombana hivyo. Sulemani atafanya nini?

Anaitisha upanga. Unapoletwa, anasema: ‘Mkate mtoto huyo aliye hai vipande viwili, umpe kila mwanamke nusu yake.’

‘Sivyo!’ mama wa kweli analia. ‘Tafadhali usiue mtoto. Mpe yeye!’ Lakini mwanamke yule mwingine anasema: ‘Usimpe wala mmoja wetu; mkate tu vipande viwili.’

Mwishowe Sulemani anasema hivi: ‘Usimwue mtoto! Mpe huyo mwanamke wa kwanza. Ndiye mama yake wa kweli.’ Sulemani anajua hivyo kwa sababu mama wa kweli ampenda mtoto sana sana hata anataka kumpa mwanamke mwenzake asiuawe. Watu wanaposikia namna Sulemani alivyotatua tatizo hilo, wanafurahi kuwa na mfalme huyo mwenye akili.

Wakati wa kutawala kwake Sulemani, Mungu anawabariki watu kwa kuufanya udongo uzae ngano na shayiri tele, zabibu na tini na vyakula vingine. Watu wanavaa mavazi mazuri na kuishi katika nyumba nzuri. Kila mtu ana kila kitu kizuri kwa wingi.