Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 75

Wavulana Wanne Babeli

Wavulana Wanne Babeli

MFALME Nebukadreza anachukua Waisraeli wote wenye elimu kuwapeleka Babeli. Kisha mfalme huyo achagua kati yao vijana wenye sura nzuri na akili zaidi. Wanne kati ya hao ni wavulana hawa unaoona. Mmoja ni Danieli, wengine watatu wanaitwa na Wababeli, Shadraka, Meshaki na Abed’nego.

Nebukadreza anafanya mpango wa kufundisha vijana hao watumikie katika jumba lake la kifalme. Wakiisha kufundishwa kwa miaka mitatu ndipo atachagua tu wenye akili zaidi wamsaidie kuamua mambo magumu. Mfalme huyo anataka wavulana wawe na nguvu na afya wanapofundishwa. Basi anaagiza watumishi wake wawape wote chakula kilekile kizuri na divai nzuri ambayo jamaa yake wanapata.

Ebu mtazame kijana Danieli. Unajua analomwambia Ash’penazi mtumishi mkuu wa Nebukadreza? Danieli anamwambia kwamba hataki kula vitu vinono katika meza ya mfalme. Lakini Ash’penazi anahangaika. ‘Mfalme ameamua mtakachokula na kunywa,’ asema. ‘Msipoonekana wenye afya kama vijana wengine, huenda akaniua.’

Basi Danieli anamwendea mlinzi aliyewekwa na Ash’penazi kuwa msimamizi wake na wa rafiki zake watatu. ‘Tafadhali utujaribu kwa siku 10,’ asema. ‘Utupe mboga tule na maji tunywe. Kisha utulinganishe na vijana wengine wanaokula chakula cha mfalme, uone mwenye sura bora.’

Yule mlinzi akubali kufanya hivyo. Zinapomalizika siku 10, Danieli na rafiki zake watatu wanaonekana wenye afya kuliko vijana wengine wote. Basi mlinzi huyo awaruhusu waendelee kula mboga.

Mwishoni mwa miaka mitatu vijana wote wanapelekwa kwa Nebukadreza. Akiisha kusema nao wote, mfalme anaona Danieli na rafiki zake watatu kuwa wenye akili zaidi. Basi anawachukua wamsaidie katika jumba la kifalme. Wakati wowote mfalme anapouliza Danieli, Shadraka, Meshaki na Abed’nego maulizo magumu, wanajua mara 10 kuliko makuhani au watu wenye akili.