Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 76

Yerusalemu Unaharibiwa

Yerusalemu Unaharibiwa

SASA ni zaidi ya miaka 10 tangu Mfalme Nebukadreza alipowapeleka Waisraeli wote wenye elimu Babeli. Na sasa angalia yanayotokea! Yerusalemu unachomwa. Waisraeli ambao hawakuuawa wanapelekwa Babeli kama wafungwa.

Kumbuka, manabii wa Yehova walisema ingekuwa hivyo ikiwa watu wangeendelea kuwa wabaya. Lakini Waisraeli hawakuwasikiliza manabii hao. Waliendelea kuabudu miungu ya uongo badala ya Yehova. Basi watu hao wanafaa kuadhibiwa. Twajua hivyo kwa sababu nabii wa Mungu Ezekieli anatuambia mabaya ambayo Waisraeli walikuwa wakifanya.

Je! unamjua Ezekieli? Ni mmoja wa vijana ambao Mfalme Nebukadreza alipeleka Babeli miaka 10 iliyopita kabla ya uharibifu huo mkubwa wa Yerusalemu. Danieli na rafiki zake watatu, Shadraka, Meshaki na Abed’nego pia walipelekwa Babeli wakati uo huo.

Wakati Ezekieli angali huko Babeli, Yehova anamwonyesha mabaya yanayotendeka Yerusalemu katika hekalu. Yehova anafanya hivyo kwa mwujiza. Ezekieli kwa kweli yuko Babeli, lakini Yehova anamruhusu aone kila kitu kinachotendeka hekaluni. Ezekieli anaona mambo ya kuchukiza!

‘Tazama machukizo ambayo watu wanafanya humu hekaluni,’ Yehova amwambia Ezekieli. ‘Zitazame kuta zenye picha za nyoka na wanyama wengine. Watazame Waisraeli wanaoviabudu!’ Ezekieli anaona vitu hivyo na kuandika yanayotendeka.

‘Unaona wanayofanya kisiri viongozi Waisraeli?’ Yehova anamwuliza Ezekieli. Ndiyo, anaona hayo pia. Kuna wanaume 70, wote wanaabudu miungu ya uongo. Wanasema: ‘Yehova hatuoni. Ameiacha nchi.’

Kisha Yehova anamwonyesha Ezekieli wanawake katika lango la kaskazini la hekalu. Wameketi hapo wakiabudu Tamuzi, mungu wa uongo. Watazame wanaume hao penye mwingilio wa hekalu la Yehova! Wako karibu 25. Ezekieli anawaona. Wanainama kuelekea mashariki na kuabudu jua!

‘Watu hawa hawaniheshimu,’ asema Yehova. ‘Wanafanya mabaya hata kwenye hekalu langu!’ Hivyo Yehova anaahidi hivi: ‘Wataona ukali wa hasira yangu. Sitawahurumia watakapoharibiwa.’

Miaka mitatu tu Yehova akiisha kumwonyesha Ezekieli mambo hayo, Waisraeli wanamwasi Mfalme Nebukadreza. Wanakwenda kupigana nao. Baada ya mwaka mmoja na nusu Wababeli wanavunja kuta za Yerusalemu na kuchoma mji kabisa. Watu wengi wanauawa au kupelekwa kama wafungwa Babeli.

Kwa nini Yehova ameruhusu uharibifu huu mkubwa uwapate Waisraeli? Ndiyo, kwa sababu hawakumsikiliza Yehova na hawakutii sheria zake. Hiyo inatuonyesha lazima ya kutimiza sikuzote maneno ya Mungu.

Kwanza watu wachache wanaruhusiwa kukaa katika nchi ya Israeli. Mfalme Nebukadreza anaweka Gedalia Myahudi asimamie watu hao. Lakini Waisraeli fulani wanamwua Gedalia. Sasa watu wanaogopa kwamba Wababeli watakuja kuwaharibu wote kwa sababu ya ubaya huo. Basi wanamlazimisha Yeremia awafuate, nao wanakimbilia Misri.

Nchi ya Israeli inaachwa bila watu wo wote. Hakuna anayekaa katika nchi hiyo kwa miaka 70. Ni tupu kabisa. Lakini Yehova anaahidi kurudisha watu wake kwenye nchi hiyo baada ya miaka 70. Sasa, watu wa Mungu katika Babeli wanapatwa na nini? Ebu tuone.