Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 83

Kuta za Yerusalemu

Kuta za Yerusalemu

ANGALIA kazi inayofanywa hapa. Waisraeli wanajenga kuta za Yerusalemu. Mfalme Nebukadreza alipoharibu Yerusalemu miaka 152 iliyopita, aliangusha kuta na kuchoma malango ya mji. Waisraeli hawakujenga tena kuta waliporudi kutoka Babeli.

Unadhani watu waliona namna gani kukaa humo miaka yote hiyo bila kuta kuzunguka mji wao? Hawakujiona salama. Adui zao wangeweza kuingia kwa urahisi na kuwashambulia. Lakini sasa mwanamume huyu Nehemia anasaidia watu wajenge tena kuta. Unamjua Nehemia?

Nehemia ni Mwisraeli kutoka mji wa Shuʹshani, wanaokaa Mordekai na Esta. Nehemia alifanya kazi katika jumba la mfalme. Labda alikuwa rafiki mzuri wa Mordekai na Malkia Esta. Lakini Biblia haisemi Nehemia alimtumikia Mfalme A·has·u·eʹro, mume wa Esta. Alimtumikia Mfalme Ar·ta·ksase, aliyefuata.

Kumbuka, Ar·ta·ksase ni mfalme yule mzuri aliyempa Ezra fedha apeleke Yerusalemu kwenda kutengeneza hekalu la Yehova. Lakini Ezra hakujenga kuta za mji zilizobomoka. Na tuone ilivyokuwa hata Nehemia akafanya kazi hiyo.

Imekuwa miaka 13 tangu Ar·ta·ksase alipompa Ezra fedha za kutengeneza hekalu. Nehemia sasa ni mnyweshaji wa Mfalme Ar·ta·ksase. Maana yake anamnywesha mfalme divai, na kuona kwamba hakuna mtu anayejaribu kumpa mfalme sumu. Hiyo ni kazi ya maana sana.

Basi, siku moja Hanani ndugu ya Nehemia na watu wengine kutoka nchi ya Israeli wanakuja kumtembelea Nehemia. Wanamwambia habari ya kutaabika kwa Waisraeli, na namna kuta za Yerusalemu zingali zimebomoka. Nehemia anahuzunika sana, naye amwomba Yehova juu ya hilo.

Siku moja mfalme anaona kwamba Nehemia ana huzuni, anauliza: ‘Sababu gani una huzuni?’ Nehemia anasema Yerusalemu umeharibika sana na kuta zimebomoka. ‘Wataka nini?’ mfalme auliza.

‘Unipe ruhusa niende Yerusalemu,’ Nehemia asema, ‘nikajenge upya kuta hizo.’ Mfalme Ar·ta·ksase ni mwema sana. Akubali Nehemia aende, kisha amsaidia kupata mbao za kujengea. Mara Nehemia akiisha kufika Yerusalemu, anawaambia watu mipango yake. Wanapenda wazo hilo, na kusema: ‘Na tuanze kujenga.’

Adui za Waisraeli wanapoona ukuta unafika juu, wanasema: ‘Tutakwenda kuwaua, na kuzuia ujenzi.’ Lakini Nehemia anasikia habari hiyo, kisha awapa wafanya kazi panga na mikuki. Ndipo awaambia hivi: ‘Msiogope adui zenu. Piganieni ndugu zenu, watoto wenu, wake zenu, na nyumba zenu.’

Watu wanakuwa hodari sana. Wanaziweka silaha zao tayari mchana na usiku, wanaendelea kujenga. Basi kwa muda wa siku 52 tu kuta zinamalizika. Sasa watu wanajisikia salama ndani ya mji. Nehemia na Ezra wawafundisha watu sheria ya Mungu, na watu wafurahi.

Lakini mambo hayako namna yalivyokuwa kabla Waisraeli hawajapelekwa Babeli wakiwa wafungwa. Watu wanatawalwa na mfalme wa Ajemi na yawapasa wamtumikie. Lakini Yehova ameahidi kutuma mfalme mpya, na mfalme huyo ataletea watu amani. Ni mfalme gani huyo? Ataletea dunia amani namna gani? Miaka 450 yapita kabla ya kupata habari zaidi. Halafu mtoto wa maana sana azaliwa. Lakini hiyo ni hadithi nyingine.