Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 84

Malaika Anatembelea Mariamu

Malaika Anatembelea Mariamu

MWANAMKE huyu mwenye sura nzuri ni Mariamu (Maria). Ni Mwisraeli, anayekaa mjini Nazareti. Mungu anajua ni mtu mzuri sana. Ndiyo sababu amemtuma malaika wake Gabrieli akaseme naye. Unajua habari ambayo Gabrieli amekuja kumwambia Mariamu? Ebu tuone.

‘Habari ya kushinda, wewe mwenye kupendelewa mno,’ Gabrieli anamsalimu. ‘Yehova yuko nawe.’ Mariamu hajapata kuona mtu kama huyu. Anapata wasiwasi, kwa sababu hajui maana ya salamu yake. Mara hiyo Gabrieli anatuliza wasiwasi wake.

‘Usiogope, Mariamu,’ asema. ‘Yehova amependezwa nawe sana. Ndiyo maana atakufanyia ajabu moja. Upesi utazaa mtoto. Utamwita jina Yesu.’

Gabrieli anazidi kueleza hivi: ‘Mtoto huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Mungu Aliye Juu Zaidi. Yehova atamfanya mfalme, kama Daudi. Lakini Yesu atakuwa mfalme milele, na ufalme wake hautakwisha!’

‘Yote hayo yanawezekana namna gani?’ Maria auliza. ‘Hata kuolewa sijaolewa. Sijakaa na mwanamume, sasa nizaeje mtoto?’

‘Nguvu za Mungu zitakuja kwako,’ Gabrieli ajibu. ‘Hivyo mtoto huyo ataitwa Mwana wa Mungu.’ Kisha anamwambia Mariamu hivi: ‘Kumbuka Elisabeti wa ukoo wako. Watu walisema ni mzee mno hawezi kuzaa watoto. Lakini atazaa mwana karibuni. Unaona basi, hakuna la kumshinda Mungu.’

Mara hiyo Mariamu asema: ‘Mimi ni mtumishi wa Yehova! Na iwe kwangu kama ulivyosema.’ Kisha malaika aenda zake.

Mariamu afanya haraka kumtembelea Elisabeti. Elisabeti anaposikia sauti ya Mariamu, kitoto tumboni mwa Elisabeti kinaruka kwa furaha. Elisabeti anajawa na roho ya Mungu, halafu anamwambia Mariamu hivi: ‘Wewe ni mbarikiwa sana kati ya wanawake.’

Mariamu yuko karibu kuolewa na Yusufu (Yosefu). Lakini Yusufu anapopata habari kwamba Mariamu atazaa mtoto, anasita kumwoa. Ndipo malaika wa Mungu anamwambia hivi: ‘Usiogope kumwoa Mariamu. Maana ni Mungu aliyempa mwana.’ Basi Mariamu na Yusufu wanaoana, na kungojea Yesu azaliwe.