Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HADITHI YA 92

Yesu Anafufua Wafu

Yesu Anafufua Wafu

MSICHANA unayeona hapa ana miaka 12. Yesu anamshika mkono, na mama na baba yake wamesimama karibu naye. Unajua sababu gani wanafurahi? Acha tuone.

Baba ya msichana ni mtu wa maana jina lake Yairo. Siku moja binti yake anakuwa mgonjwa, analazwa. Lakini haponi. Anazidi kuwa mgonjwa. Yairo na mke wake wanasumbuka sana, kwa sababu binti yao atakufa. Ni binti yao mmoja tu. Basi Yairo aenda kumtafuta Yesu. Amesikia miujiza ambayo Yesu anafanya.

Yairo anapomwona Yesu, watu wengi wamemzunguka. Lakini Yairo anapita katikati ya watu wengi na kuanguka miguuni pa Yesu. ‘Binti yangu ni mgonjwa sana sana,’ asema. ‘Tafadhali, njoo umponye,’ aomba. Yesu anamwambia atakuja.

Wanapotembea, watu wengi wanazidi kukaribia. Mara moja Yesu anasimama. ‘Nani amenigusa?’ auliza. Yesu alisikia nguvu imemtoka, hivyo anajua mtu fulani amemgusa. Lakini nani? Ni mwanamke ambaye amekuwa mgonjwa sana muda wa miaka 12. Alikuwa amekuja akakamata mavazi ya Yesu, akaponywa!

Hii inamtuliza Yairo, maana anaona namna Yesu anavyoweza kumponya mtu kwa urahisi. Lakini mjumbe anafika. ‘Usimsumbue Yesu tena,’ amwambia Yairo. ‘Binti yako amekufa.’ Yesu anasikia hayo na kumwambia Yairo: ‘Usiwe na wasiwasi, atapona.’

Mwishowe wanapofika nyumbani kwa Yairo, wanakuta watu wakilia kwa huzuni kuu. Lakini Yesu awaambia: ‘Msilie. Mtoto hakufa. Analala usingizi tu.’ Lakini wanamcheka Yesu, maana wanajua amekufa.

Ndipo Yesu anachukua baba na mama ya msichana na mitume wake watatu ndani ya chumba ambamo mtoto amelala. Anamshika mkono na kusema: ‘Amka!’ Anakuwa hai, kama unavyoona hapa. Anaamka na kutembea! Ndiyo maana mama na baba yake wanafurahi sana sana.

Huyu siye mtu wa kwanza kufufuliwa na Yesu. Yule wa kwanza anayesemwa na Biblia ni mwana wa mjane anayekaa mjini Naini. Baadaye, Yesu anafufua Lazaro pia, ndugu ya Mariamu na Martha. Wakati Yesu atakapokuwa mfalme aliyewekwa na Mungu, atafufua watu wengi sana. Hatuwezi kufurahia hilo?